Kiswahili Paper 3 Questions and Answers - MECS Cluster Joint Pre Mock Exams 2021/2022

Share via Whatsapp

KISWAHILI
KARATASI YA 3
(FASIHI)

MAAGIZO:

  1. Jibu maswali manne pekee.
  2. Swali la kwanza ni la lazima.
  3. Maswali hayo mengine matatu yachaguliwe kutoka sehemu nne zilizobaki; yaani; Riwaya, Tamthilia, Ushairi na Hadithi Fupi.
  4. Usijibu maswali mawili kutoka sehemu moja.

SEHEMU A: FASIHI SIMULIZI
(LAZIMA)

  1.          
    1. Tumia kifungu kifuatacho kujibu maswali yanayofuata.
      Nyumbani mwetu mna papai lililoiva lakini siwezi kulichuna – Ndugu wa kiume asimuoe nduguye wa kike.
      1. Bainisha kipera kinachorejelewa. (ala. 1)
      2. Andika shughuli moja ya kijamii na moja ya kiuchumi ambazo huedelezwa katika jamii ya utungo huu. (ala. 2)
      3. Eleza dhima nne za kipera kinachorejelewa katika jamii yako. (ala 4)
      4. Wewe ni mwasilishaji wa kipera hiki jukwaani. Eleza mambo matatu ambayo utayazingatia katika uwasilishaji wake. (ala. 3)
    2. Umepewa jukumu la kukusanya data kuhusu michezo ya watoto ukitumia hojaji.
      1. Eleza manufaa matano ya kutumia mbinu hii. (ala. 5)
      2. Eleza changamoto tano za kutumia mbinu hii . (ala. 5)

SEHEMU B: RIWAYA
A.Matei:Chozi la Heri
Jibu swali la 2 au la 3

  1. ‘….unajikokota nyumbani,moyoni ukiamini kwamba ng’ombe akivunjika mguu malishoni hujikokota zizini kusaidiwa,kwamba hata kosa lako likawa kubwa vipi,teke la kuku halimuumizi mwanawe…Halafu unaloambiwa ni,Umeipaka mashizi familia hii….
    1.          
      1. Eleza muktadha wa dondoo hili. (ala.4)
      2.  Andika nafsi ya usimulizi iliyotumiwa katika dondoo hili. (ala. 2)
      3. Fafanua toni ya dondoo hili. (ala. 2)
      4. Bainisha mbinu mbili za kimtindo zinazojitokeza katika dondoo hili. (ala. 2)
    2. Fafanua umuhimu wa usimulizi wa msemaji wa dondoo hili katika kujenga riwaya hii. (ala. 10)
  2. “Jua linalochomoza halina ule wekundu wa jua la matlai ambao huleta haiba ya uzawa wa siku yenye matumaini. Naona wingu kubwa angani likitembea kwa kedi na madaha na kulifunika jua… Mawingu yaliyoshiba yakataka kutapika yanagooka, yanakaribiana,kupigana busu na kusababisha mwanguko wa matone mazito ya mvua…”
    1.          
      1. Bainisha aina za taswira na umuhimu wake zinazojitokeza katika dondoo hili. (ala. 6)
      2. Tambua mbinu nyingine ya kimtindo inayojitokeza katika dondoo hili. (ala. 2)
    2. Eleza umuhimu wa matukio anayokumbuka Ridhaa kabla ya kuchomeka kwa jumba na familia yake. (ala.12)

SEHEMU C: TAMTHILIA
P. KEA: KIGOGO
JIBU SWALI LA 4 AU LA 5

  1. “Ya kale hayaachi kunuka. Na uuchunge sana ulimi wako usikutome kwenye bahari mchafukoge usi…” “ nisiyoimudu mbizi yake.”
    1. Eleza muktadha wa dondoo hili. (ala. 5)
    2. Bainisha vipengele vitatu vya kimtindo katika doindoo hili. (ala. 3)
    3.      
      1. Andika suala linalodokezwa na kauli iliyopigiwa mstari. (ala. 2)
      2. Jadili hoja kumi zinazoonyesha namna suala hili linavyojitokeza tamthiliani. (ala. 10)
  2.         
    1. Jadili jinsi vyombo vya dola vilivyotumiwa kuuendeleza uogozi wa Sagamoyo. (ala.12)
    2. Eleza umuhimu wa maelekezo ya jukwaani katika tamthilia hii. (ala. 8)

SEHEMU YA D: USHAIRI
Jibu Swali La 6 au la 7

  1. Soma Shairi hili kisha ujibu maswali yanayofuata.

    Dhamiri yangu.
    Dhamiri imenifunga shingoni.
    Nami kama mbuzi nimefungwa
    Kwenye mti wa utu. Kamba ni fupi
    Na nimekwishachora duara.
    Majani niwezayo kufikia yote nimekula.
    Ninaona majani mengi mbele yangu
    Lakini siwezi kuyafikia: kamba, kamba.

    Oh! Nimefungwa kama mbwa.
    Nami kwa mbaya bahati, katika
    Uhuru kupigania, sahani ya mbingu
    Nimeipiga teke na niigusapo kwa mdomo
    Mbali zaidi inakwenda na siwezi tena
    Kuifikia na hapa nilipofungwa
    Nimekwisha pachafua na kuhama siwezi.

    Kamba isiyoonekana haikatiki,
    Nami sasa sitaki ikatike, maana,
    Mbuzi wa kamba alipofunguliwa, mashamba
    Aliharibu na mbwa aliuma watu.
    Ninamshukuru aliyenifunga hapa
    Lakini lazima nitamke kwa nguvu “Hapa nilipo sina uhuru”

    1. Taja mambo manne ambayo mshairi analalamikia. (alama 4)
    2. Kwa nini mshairi haoni haja ya yeye kuwa huru? (alama 2)
    3. Eleza maana ya mshororo ufuatao kama ulivyotumiwa katika shairi. “Kamba isiyoonekana haikatiki.” (alama 2)
    4. Taja na utoe mifano ya aina mbili za tamathali zilizotumika katika shairi hili. (alama 4)
    5. Kwa kutoa mifano miwili, eleza jinsi matumizi ya mishata yanavyojitokeza katika shairi hili. (alama 4)
    6. Andika ubeti wa pili kwa lugha nathari. (alama 4)

  2. Said A. Mohamed: Mbele ya Safari

    1. Ilipoanza safari, ilianza kwa dhiki
      Tulishikana kwa ari, kwenda safari ya haki
      Tukawa ni majabari, nyoyo zisitaharuki
      Tukajizatiti

    2. Njaa ikawa thabiti, na kiu kutamalaki
      Nasi tulitia dhati, tusijali kuhiliki
      Ingawa mbele mauti, dhila na mingi mikiki
      Tukajizatiti

    3. Huu mwisho wa safari, tukaambiwa ni haki
      Shangwe kwetu na fahari, utumwa hatuutaki
      Kuwa mbele ya safari, juhudi iliyobaki
      Tukajizatiti

    4. Ile ilikuwa ndoto, mwisho wake mafataki
      Nguvu zimechomwa moto, sahala ‘mekuwa dhiki
      Wagombania kipato, utashi haukatiki
      Na kutabakari

    5. Msafara ukasita, kwenye mlima wa haki
      Kijasho kinatuita, mlima haupandiki
      Basi sote ‘kijipeta, kukikwea kima hiki
      Twataka hazina

    6. Tukiwa migongo wazi, tukainama kwa shaki
      Tukawa’chia ukwezi, kialeni wadiriki
      Wakapanda bila kazi, kuteremsha miliki
      Wakaitapia

    7. Wakafikia makazi, ya pumbao na ashiki
      Huko wakajibirizi, kwenye raha lakilaki
      Wakaisahau ngazi, ya umma ulomiliki
      Mbele ya safari

    8. Na hazina yetu sote, kuishusha hawataki
      Wamo wanatema mate, kwa umati halaiki
      Imezima nia yote, kiza hakitakasiki
      Mbele ya safari

      1. Eleza safari inayorejelewa katika shairi hili. (alama 2)
      2. Onyesha kinaya cha safari inayozungumziwa. (alama 6)
      3. Taja na ueleze bahari mbili za shairi hili ukizingatia: (alama 4)
        1. Mizani;
        2. Vina.
      4. Andika ubeti wa saba kwa lugha ya nathari. (alama 4)
      5. Eleza umuhimu wa aina mbili za uhuru wa kishairi zilizotumiwa katika ubeti wa sita.(alama 4)

SEHEMU E: HADITHI FUPI
A Chokocho na D Kayanda;Tumbo lisiloshiba na hadithi nyingine
“Masharti ya Kisasa”

  1. “ …alihisi koo yake imefumba na hamu ya chakula imepotea. Ikabidi akamatekamate kile chakula tu.Mwisho akaona hana haja ya kujilazimisha. Akaamua kukiacha kama kilivyo. Akanawa na kuondoka hapo mezani na kuketi juu ya sofa. Akajidai kutazama televisheni…”
    1. Eleza muktadha wa dondoo hili. (ala. 4)
    2. Bainisha taswira zinazojitokeza katika dondoo hili. (ala. 3)
    3. Eleza sifa tatu za mrejelewa (ala. 3)
    4. Kwa kurejelea hadithi eleza mambo kumi yaliyochangia mrejelewa kuwa kuwa katika hali hiyo. (ala. 10)

MAAKIZO

  1.        

      1. Kitendawili……………….. 1*1=1
      2. Shughuli ya kijamii………….. kilimo/ukulima.
        Shughuli ya kiuchumi………….ndoa ama nikahi.
        (2*1=2)
      3. Dhima ya kipera hiki:
        • kuelimisha
        • kuburudisha
        • kukuza uwezo wa kukumbuka
        • kukuza uwezo wa kufikiri
        • kutanguliza tanzu nyingine za kifasihi
        • kukashifu tabia hasi katika jamii
        • kukuza utangamano
        • kukuza udadisi
        • kuwajuza wanajamii kuhusu mazingira yao.
        • Kukuza ubunifu
        • Kukuza uzalendo.
        • Kuhifadhi historia.
          (4*1=4)
      4. Mambo ya kuzingatia katika uwasilishaji ;
        • Sauti inayosikika.
        • Awe mbunifu.
        • Aweze kukumbuka.
        • Aielewe lugha ya hadhira yake.
        • Aufahamu utamaduni wa hadhira yake.
        • Awe mcheshi.
        • Awe jasiri.
        • Arejelee mifano halisi katika jamii.
        • Aielewe hadhira.
        • Awe mfaraguzi.
        • Kuishirikisha hadhira.
          3*1=3.
    1. Hojaji
      1. Manufaa ya hojaji.
        • Ina gharama ya chini Zaidi ikilinganishwa ma njia nyinginezo.
        • Mtafiti anaweza idadi kubwa ya watoaji habari kwa kipindi kifupi kwa maana hojaji zinaweza zikatumiwa watu hao kwa njia kama vile posta.
        • Inaweza kutumiwa katika mahojiano kama mwongozo. Mhoji anaweza kuitumia katika mahojiano kufidia udhaifu wa mhojiwa.
        • Humpa mhojiwa muda wa kuwazia maswali na kuyafanyia uchunguzi kabla ya kuyajibu.
        • Hazina athari za mtafiti kwa sababu aghalabu zinapojazwa mtafiti hayupo. Mhojiwa hujaza habari za kweli bila kushinikiwa kuchukua mtazamo Fulani kutokana na kuwepo kwa mtafiti.
        • Zinaweza kubadilishwa kulingana na kiwango cha wajazaji/wahojiwa.
          5*1=5.
      2. Changamoto za hojaji.
        • Maswali yenye utata husababisha fasiri mbalimbali ambazo hufanya matokeo yasitegemeke.
        • Huenda wengine wasikamilishe kujaza hojaji,hivyo kumhini mtafiti habari anazotaka.
        • Hojaji ikiwa ndefu sana huenda baadhi ya watu wakakataa kuijaza.
        • Hojaji wazi huwa ngumu sana kwa mtafiti kuchanganua data. Uchanganuzi huchukua muda mrefu.
        • Huenda wahojiwa wasijaze mambo ya kweli. Si rahisi kwa mtafiti kuthibitisha iwapo habari zilizojazwa ni za kweli.
        • Wahojiwa wanaweza kuchelewa kutuma hojaji zao, hasa hojaji zilizotumwa kwa posta.
        • Zinaweza kujazwa tu na watu waliosoma,hivyo kuwatenga wengine ambao labda wangetoa habari za kutegemeka.
        • Kwa vile mtafiti,hakabiliani na mhojiwa ana kwa ana ,hawezi akapata sifa za uwasilishaji wa vipera vya fasihi simulizi kama vile toni na kidatu.
          5*1=5
  2.          
    1.    
      1. Msemaji ni Zohali.
        Anazungumza na umu, kairu, chandachema na mwanaheri/ wanafunzi wenzake.
        Katika bweni la shule/ shule ya upili ya tangamano.
        Baada ya kupata uja uzito akiwa shuleni.
        4*1=4
      2. Nafsi ya pili
        1*2=2
      3. Toni ya uchungu/ hasira/malalamiko
        1*2=2
      4.      
        • D. Methali………… ng’ombe akivunjika mguu malishoni hujikokota zizini kusaidiwa.
        • Msemo………………….. teke la kuku halimuumizi mwanawe.
        • Jazanda/istiara……….. teke la kuku-adhabu ya mzazi/ umeipaka mashizi familia hii.
        • Usimulizi…………….. kisa chote kimesimuliwa.
        • Taswira mwendo- hujikokota zizini.
          (za kwanza 2*1=2)

    2. Umuhimu wa usimulizi wa Zohali.
      • Kuonyesha matatizo ya vijana – zohali anashindwa kujidhibiti na kuambulia uja uzito akiwa shuleni.
      • Kujenga maudhui ya malezi- babake zohali anamdhalilisha zohali na kumfanya atoroke nyumbani/mtawa pacha anamlea zohali na mtoto wake.
      • Kusawiri matatizo ya watoto wa mitaani- anatumia gundi ili kujisahaulisha matatizo yake.
      • Kukashifu ukiukaji wa haki za kibinadamu- zohali anapigana na watu wanaotaka kumnyanyasa kimapenzi.
      • Kubainisha nafasi ya dini katika malezi- wakfu wa mama paulina unamtunza zohali na mtoto wake.
      • Kuhimiza mshikamano wa kijamii- vijana wa mtaani ndio wanaompelekea zohali kwa wakfu wa mama paulina wanapona kwamba yu karibu kujifungua.
      • Athari za mapenzi kabla ya ndoa- kupachikwa mimba, kukaa shuleni muda mrefu, kufukuzwa shuleni.
        5*2=10.

  3. SWALI LA TATU.
    1.      
      1. Aina za taswira.
        • Taswira oni- kama jua linalochomoza halina ule wekundu wa jua la matlai/ naona wingu kubwa angani.
        • Taswira mwendo- yanagooka/yanakaribiana/mwanguko.
        • Taswira mguso- kupigana busu.
        • Taswira hisi- akitembea kwa kedi na madaha.
          4*1=4

          Umuhimu;
        • Msimulizi Kaizari anaonyesha hali ya ukosefu wa tumaini kambini humu.
        • Hali ya kuhofisha.
          2*1=2
      2. Tashhisi/uhuishi/uhuishaji. Kama mawingu yaliyoshiba.
        (2*1=2; mbinu 1, mfano 1).

    2. UMUHIMU WA MBINU REJESHI HAPA NI;
      1. Kuonyesha ushirikina katika jamii hii. Kama Ridhaa anatishwa na milio ya bundi.
      2. Kuonyesha utu na hekima ya terry-anamtuliza mumewe na kumwabia hafai kuwa na wasiwasi.
      3. Kuonyesha ukatili wa mzee kedi-anaichoma familia ya Ridhaa licha ya rai ya Terry kwamba asiwaue wao ni majirani.
      4. Kuonyesha hali ya kutofikiwa kwa malengo ya baada ya uhuru- Tila anaifananisha wahafidhina na mtoto wa miaka hamsini(ukur6).
      5. Kuonyesha ukoloni mamboleo- wageni ndio wanaoamua kinachokuzwa na wahafidhina. Kampuni za kigeni ndizo zinazofadhili uchimbaji wa madini faida zinaendea wageni(ukur6)
      6. Kuonyesha uhafidhina wa mamake ridhaa –anasema wanaume hawafai kulia (ukur6)
      7. Kuonyesha kuzinduka kwa Tila- anamkabili babake kuhusu maswala ya uongozi na jamii anapotoka shuleni.ukur67.
      8. Kuonyesha uhasama wa kikabila /kiukoo- kama Ridhaa anapotengwa na wenzake shuleni ukur 10, vikaratasi vikihadharisha gharika itakayokujaukur12.
      9. Kuonyesha usuli wa aila ya ridhaa- jinsi walivyohama kutoka kitovu chao (ukungu) na kuhamia msitu wa heri(ukur8-9)
      10. Kuonyesha swala la umiliki wa ardhi-swala la kumiliki kawa ardhi wa kibinafsi haukusisitizwa kabla ya mkoloni 9ukur9)
      11. Kuonyesha bidii ya Ridhaa-licha ya kuwa na changamoto nyingi walipohamia msitu wa heri, Ridhaa anatia bidii masomoni na kuhitimu kama daktari. Aidha alikuwa mkurugenzi wa mashirika mbalimbali.(ukur11)
      12. Kuonyesha mabadiliko aliyoleta ridhaa kwa raia wa msitu wa heri- kuwaletea maji ya mabomba ,kupanda miti nkukur12-13
      13. Kuonyesha mshikamano wa kijamii-mzee kedi alivyomsaidia Ridhaa kupata shamba;jinsi Ridhaa alivyowasomesha wapwaze mzee kedi(ukur11)
      14. Kuonyesha ufisadi---jinsi mabwanyenye walivyotoa milungura hadharani ili nyumba zao zisibomolewe.ukur13
      15. Kuonyesha ukatili wa serikali- familia zao zinaachwa bila makao nyumba zao zinapobomolewa bila fidia yoyote. Aidha Ridhaa anabomolewa majumba yake yote matatu ukur13.
      16. Kuonyesha uhusiano mwema katika familia ya Ridhaa-kama uhusiano wa Ridhaa na Terry ukur2; uhusiano wake na Becky.ukur5.

  4.        
    1. Msemaji wa kauli ya kwanza ni kenga.
      Msemaji wa kauli ya pili ni sudi
      Walikuwa katika karakana ya soko la chapakazi.
      Kenga anapomkanya sudi dhidi ya kumpinga hadharani.
      Sudi anamkejeli kenga anapomtisha.
      5*1=5

    2. Methali-ya kale hayaachi kunuka.
      Msemo/nahau- uuchunge ulimi wako.
      Jazanda/sitiari- usikutome kwenye bahari ya mchafukonge.
      Kejeli/stihizai- nisiyoimudu mbizi yake.
    3.      
      1. Vitisho
        1*2=2
      2.      
        • Wanasagamoyo wanatishwa kwa kurushiwa vijikaratasi wahame kama Siti na Hashima.
        • Majoka anatumia polisi kuwatisha wanasagamoyo.
        • Majoka anamtishia chopi kuwa atamwaga unga wake kwa kutoamrisha polisi kutawanya waandamanaji.
        • Majoka anatishia kufunga runinga ya mzalendo kwa kupeperusha maandamano.
        • Kenga anapomtisha sudi anapokataa vishawishi vyake kwa kumwaambia auchunge ulimi wake.
        • Majoka anapomwabia Husda asimfanye amuumize.
        • Tunu anapomwabia majoka kuwa watalipa kila tone la damu walilomwaga sagamoyo.
        • Bi hashima anasema viongozi/majoka amewatia hofu sana. Wanaishi kwa woga mwingi sana.
        • Tunu anapokumbuka tukio la zamani la mzee marara akimfukuza akitaka mkufu wake.
        • Mamapima /Asiya anapowafukuza akina tunu katika kibanda chake.
        • Majoka anapomwambia mkuu wa polisi ,Kingi kuwa amemfuta kazi mara moja.
  5.                         
    1.  Vyombo vya dola vinaendeleza uongozi kwa namna zifuatazo;
      (Viongozi, askari, sharia, katiba, vyombo vya habari,washauri,wahuni,vikaragosi,jela/gereza).
      • Askari wanatawanya wafanyakazi wanapogoma na hivyo kudhibiti upinzani.
      • Majoka anaendeleza propaganda kuhusu kujitolea kwa uongozi wake.
      • Kenga anamshauri majoka kumwangamiza mpinzani wake Jabali, anaangamiza upinzani.
      • Majoka anatumia vyombo vya habari kuimarisha uzalendo kama sauti ya mjumbe.
      • Majoka anatumia wahuni kumuumiza Tunu. hii ilikuwa njia ya kumdhibiti.
      • Aidha majoka anatumia wahuni kueneza uvumi kuwa Sudi na Ashua ndio wasiowinda nafasi ya Tunu.
      • Katiba inayopaswa kuhakikisha usalama inampa majoka mamlaka ya kukabiliana na wanaotetea haki, hivyo kumdumisha mamlakani.
      • Washauri na vikaragosi wanafaidika na uongozi wa majoka kama kugawiwa ardhi, kandarasi ili kuendelea kumuunga majoka mkono.
      • Mzee kenga anatumia vitisho ili kuwadhibiti wapinzani wa majoka kama anamtisha sudi.
      • Askari wanawaua vijana watano wakati wa maandamano hii ni njia ya kujidumisha mamlakani.
      • Wimbo wa uhuru unatumiwa kumsifu majoka; unamminia sifa ili azidi kupata umaarufu Zaidi.
      • Chopi anatumiwa na majoka kumdhulumu Ashua anapofungiwa katika seli.
      • Majoka anamfungia Ashua ili amshurutishe Sudi amchongee kinyago.
      • Majoka anatumia mapendeleo katika nafasi za kazi kwa wanaomuunga mkono kama kenga ambaye ni binamuye.
      • Uongozi wa majoka unasambaza vikaratasi vinavyowataka baadhi ya wanasagamoyo wahame kama vile akina siti.
      • Majoka anapomwambia sudi kwamba anatumai hakuna aliyeuawa na polisi .Hataki kujipaka matope tena ,hii ni njia ya kujidumisha mamlakani.
        12*1=12

    2. UMUHIMU WA MAELEKEZO YA JUKWAANI;
      • Kueleza mienendo na miondoka ya wahusika km majoka anapotaka kumkumbatia Ashua ukur19.
      • Kutoa maelezo kuhusu wasifu wa wahusika ,mavazi, lugha, ishara, uso, nk km majoka anapouvaa mkufu wake wenye kidani cha swila shingoni.
      • Kutoa m,aelezo kuhusu mandhari /mahali pa mchezo . km soko la chapakazi, majoka resort.
      • Hufafanua matendo mbalimbali yanayotokea jukwaani . km sauti za shangwe, vifijo na nderemo zinasikika kwa mbali ukur85.
      • Hueleza wasifu wa mazingira km mazingira machafu ya soko la chapakazi.
      • Hueleza maleba ya wahusika .
      • Hutoa vielekezi kwa jinsi ya kuandaa jukwaa kwa ajili ya uigizaji.
      • Hutoa maelezo ya jinsi ya kutumia na mchango wa viambata jukwaa vingine.
      • Hutoa tathmini ya matendo au lugha ya wahusika kama vile kuonyesha wapi pana kinaya nk.
        8*1=8

  6. Dhamiri yangu.
    1.      
      • kufungwa kama mbuzi.
      • kunyimwa uhuru.
      • alipofungwa pameharibika.
      • angependa kuhama lakini hawezi.
      • kuna chakula/majani mengi mbele yake lakini hayafikii.
      • ufupi wa kamba.
      • upungufu wa chakula/njaa.
        (Za kwanza 4 x 1 = 4)
    2. Amekwishazoea hali yake/hapendi kuonekana tofauti/hana msimamo wake/hataki kuleta madhara. ( 1x2)
    3. Dhamiri iliyo akilini mwake ndiyo iliyomfunga.hajafungwa na yeyote/amejifunga na nafsi yake. (1x2)
    4. Tamathali
      • Tashbihi – kama mbuzi.
      • istiara – sahani ya mbingu.
      • jazanda – mti wa utu.
      • Tasfida – nimekwisha pachafua.
      • Takriri/uradidi – kamba kamba.
      • Nidaa/siahi – Oh!
      • Tashihisi/uhuishi – Dhamiri imenifunga.
      • Taswira – kamba fupi.
      • Tanakuzi – anataka kufunguliwa lakini hataki.
      • kinaya – Namshukuru aliyeifunga.
        (Za kwanza 2x2 = 4)
        (atoe mifano mwafaka)
    5. Mishata: Mishororo ambayo maana yake haijakamilika bali hukamilika katika mshororo unaofuata k.m.
      • Nami kwa mbaya bahati, katika
      • Nimepiga teke na nigusapo kwa mdomo
      • Nami sitaki ikatike maana
      • Mbuzi wa kamba alipofunguliwa mashamba
      • Mbali zaidi inakwenda na siwezi tena
        (zozote 2x2 = 4)
    6. Nimefungwa kama mbwa na kwa bahati mbaya katika kutaka kuondoka pale nimeipiga teke sahani ya mbingu ambayo imeenda mbele na siwezi kuifikia na pale nilipofungiwa ni pachafu.
      (4 x 1 = 4)
  7.          
    1. kupigania uhuru/haki/kujiendeleza kiuchumi.
      walishiriki/walisimama/walitaka milki pamoja
      (Kutaja 1) (Kueleza 1) (1x2 = 2)
    2. kinaya
      1. viongozi kujinufaisha ¬– raia maskini.
      2. viongozi raha – raia dhiki.
      3. viongozi kudharau raia – kuwatemea mate.
      4. raia kupigania uhuru – kutofaidika.
      5. kutoafikia maazimio – milki ya haki.
      6. walianza safari pamoja – mwishowe wanabaguliwa . (6 x 1 = 6)
    3.          
      1. mizani – msuko – mshororo wa mwisho umefupishwa.
      2. vina – ukara – vina vya kati vinabadilika vya tamati vinatiririka.
        (Kutaja 1 kueleza 1 ) (2x2=4)
    4. Mshairi analalamika kuwa viongozi walipofikia hali nzuri ya maisha tamaa ilizidi huku wakiwa na starehe za kila aina huku wakiwasahau waliowapa nafasi za uongozi ili kufikia hali yao ya sasa. (4 x 1 = 4)
    5.                 
      1. Inkisari – Tukawa`chia – Tukawaachia – kutosheleza mizani.
      2. Kuboronga sarufi – kialeni wadiriki – wadiriki kialeni – urari wa vina.
      3. Tabdila – shaki – shaka – urari wa vina.
      4. Lahaja/kikale – kialeni - kileleni – upekee wa msamiati/mapigo ya kimziki.
        (za kwanza 2 x 2 = 4)
  8.              
    1.        
      1. Maelezo ya mwandishi/msimulizi.
      2. Anamrejelea Dadi.
      3. Alikuwa nyumbani kwake.
      4. Baada ya Kidawa kumletea chakula cha jioni ili ajitayarishe aende kazini usiku.
        4*1=4
    2.        
      1. Taswira hisi-alihisi koo yake imefumba na hamu ya chakula imempotea.
      2. Taswira mguso- akamatekamate kile chakula tu.
      3. Taswira mwendo-kuondoka hapo mezani.
      4. Taswira oni- akajidai kutazama televisheni.
        3*1=3
    3. Sifa za dadi.
      1. Mwenye bidii-aliwauza samaki akiwatembeza kwa baiskeli.
      2. Ana mapenzi ya dhati-anampenda kidawa.
      3. Mwenye wivu- anapomwona kidwa akijipodoa.
      4. Mwenye tuhuma/kushuku- anamshuku kidwa kuwa na uhusiano na mwalimu mkuu.
      5. Mwenye hasira/hamaki- anamkasirikia zuhura.
      6. Mvumilivu- anavumilia mitihani ya kidawa /masharti.
      7. Ni kigeugeu- anakubali mkataba wake na kidawa lakini baadaye anaanza kumfuata.
      8. Mtiifu- anamsaidia kidawa kazi za nyumbani.
        3*1=3
    4. Mambo yaliyochangia Dadi kuwa katika hali hiyo.
      1. Dadi anayakubali masharti ya kidawa ambayo baadaye yanamtatiza.
      2. Kidawa anapofanya kazi ya umetroni usiku.
      3. Kidawa anaposimama na wanaume na kuamkiana/ kuzungumza nao .hili halimfurahishi Dadi.
      4. Dadi hazifurahii kazi za nyumbani ambazo wanasaidiana na kidawa.
      5. Mapenzi ya dadi kwa mkewe kidawa yalimsababisha kutovunja masharti ya kisasa.
      6. Kwamba wanaume na wanawake mtaani kuamini kwamba dadi ametiwa maganjani na kudhibitiwa na mkewe.
      7. Kidawa anapofanya kazi ya kuuza kanzu viatu na khanga.
      8. Wakati kidawa hataki kukubali kuawa kazi za mwanamume ni za nje wala si za ndani.
      9. Masharti ya kisasa yanamzuia dadi kumkataza kidawa mambo asiyoyapenda.
      10. Bi zuhura kukataa kulipa pesa ili dadi ampatie samaki na kumdhihaki kuwa wengine(kidawa) wanapatiwa bure.
      11. Dadi anapodhani kwamba kidawa anajipodoa ili amfurahishe mwalimu mkuu.
      12. Kidawa anapomwabia dadi kuwa yeye hujipodoa kwa lengo la kuufurahisha moyo wake.
      13. Dadi alidhani angeumiliki na kuutawala uwanja wa mapenzi ya kidawa lakini anapewa masharti mengi.
      14. Dadi anapobaki na mwanawe shara wakati mkewe kidawa anaenda shuleni kufanya kazi ya umetroni.
      15. Dadi anaachiwa majukumu ambayo kwa kawaida yalikuwa ya wanawake kama kukuna nazi.
        (za kwanza 10*1) 
Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Paper 3 Questions and Answers - MECS Cluster Joint Pre Mock Exams 2021/2022.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?

Join our community on:

  • easyelimu app
  • Telegram
  • facebook page
  • twitter page
  • Pinterest