KCSE 2015 Kiswahili Karatasi ya Tatu with Marking Scheme

Share via Whatsapp

SEHEMU A : FASIHI SIMULIZI.

  1. Lazima
    1. Soma ufungo ufuatao kisha ujibu maswali.
      Hadithi ya Jabari inasimuliwa na jamii nyingi. Jabari alizaliwa kashika mkuki mkononi. Mawio ambayo kilio chake, ambacho kwa kweli kilikuwa mngurumo, kilipopasua anga, nyota kubwa ilianguka kutoka mbinguni. Ulimwengu mzima uliltetemeka na kutwaa giza.
      Hata kabla mama mtu hajampa ziwa, Jabari alikuwa amevuvumuka na kuwa ghulamu wa miraba minne. Haikuchukua muda, hata vita kati ya jamii ya Sule na Suna vikaanza; kikosi cha Sule cha wapiganaji mia moja kikawajia vijana wa Suna kwa sime na nyuta. Jabari aliwakabili kwa konde moja pekee, akakirambisha dongo kita kizima.
      1. Bainisha kipera cha utungo huu.    (alama 1)
      2. Toa sababu mbili za kudhibitisha jibu lako la (i) hapa juu.    (alama 1)
      3. Eleza manufaa sita ambayo jamii itapata kwa kukirithisha kipera hiki kwa vizazi vijavyo. (alama 6)
    2. Soma ufungo ufuatao kisha ujibu maswali.
      Ndimi Mwimo mdumishaji ukoo
      Ndimi ndovu mtetemesha ardhi
      Aliyepigana vita, ukoo kauni
      Ziliporindima zangu nyayo
      adui alinywea, mafahali na mitamba akatukabidhi
      Kwenye misitu sikuwa na kifani
      Paa na hata visungura
      vilijikabidhi kwangu
      kwa kuinusa tu mata
      Nani aliyewahi
      ngomani kunipiku?
      Makoo hawakunisifu, wakalia nikaha?
      Kwenye nyanja za michuano
      nani angedhubutu, ndaro kunipiga?
      Sikuwabwaga chini, kwa yangu maozi, hata kabla hatujavaana?
      1. Andika aina ya sifo hii.   (alama 1)
      2. Bainisha shughuli mbili za kiuchumi na mbili za kijamii zinazoendelezwa na jamii inayosawiriwa na utungo huu.   (alama 2)
      3. Eleza mambo matano ambayo yanaweza kuzigatiwa ili kufanikisha uwasilishaji wa utungo huu.  (alama 5)
    3. Eleza faida nne za matumizi ya nyimbo katika uwasilishaji wa ngano. (alama 4) 

SEHEMU B: RIWAYA
K. Walibora: Kidagaa Kimemwozea.
Jibu swali la 2 au la 3

  1. "Moyo ulimpapa na kijasho chembamba kumtekenya juu ya mwanzi wa pua. Akahisi uchungu wa mwiba wa kujidunga."
    1. Eleza muktadha wa dondoo hili. (alama 4)
    2. Huku ukirejelea riwaya hii, fafanua kwa kutoa hoja nane, namna anayelengwa na kauli hii alivyojidunga miiba. (alama 16)
  2.    
    1. "Imani ni kielelezo cha vijana waliowajibika." Thibitisha kauli hii kwa kurejelea mifano kumi kutoka Kidagaa Kimemwozea.    (alama 10)
    2. "Nadhani Mzungu pale alipo hana budi kumtambua ukomavu wa Mwafrika katika kila sekta ya maisha."
      Onyesha kinyume katika kauli iliyopigiwa mstari kwa kurejelea uongozi wa Tomoko. (alama 10)

SEHEMU C: TAMTHILIA
T.Arege: Mstahiki Meya
Jibu swali la 4 au la 5

  1. "Kushindana naye ni kama kushindana na ndovu. Utapasuka."
    1.    
      1. Eleza muktadha wa dondoo hili.  (alama 4)
      2. Bainisha tamathali moja ya usemi inayojitokeza katika dondoo hili.(alama 2)
    2. Kwa kurejelea hoja saba, thibitisha kwamba kushindana na anayerejelewa na kauli hii ni sawa na kushindana na ndovu. (alama 14)
  2. " Wahenga wanasema dawa ya adui ni kummegea unachokula."
    1.    
      1. Andika swala linalodekezwa na kauli iliyopigiwa mstari. (alama 2) 
      2. Jadili hoja nane zinazoonyesha namna suala hili linavyozorotesha hali ya maisha Cheneo. (alama 8)
    2. Jadili jinsi vyombo vya usalama vilivyotumiwa kuuendeleza uongozi wa Cheneo. (alama 10)

SEHEMU D: USHAIRI
Jibu swali la 6 au la 7.

  1. Soma shairi lifuatalo kisha ujibu maswali.
    Daima alfajiri na mapema
    Hunipitia na jembe na kotama
    Katika njia iendayo kondeni
    Kama walivyofanya babuze zamani;
    Nimuonapo huwa anatabasamu
    Kama mtu aliye na kubwa hamu 
    Kushika mpini  kutokwa jasho
    Ili kujikimu kupata malisho.
    Anapotembea anasikiliza 
    Videge vya anga vinavyotumbuiza
    Utadhani huwa vimengojea
    Kwa usiku kucha kuja kumwimbia;
    Pia pepo baridi kumpepea
    Rihi za maua zikimletea
    Nao umande kumbusu miguu;
    Na miti yote hujipinda migongo
    kumpapasa, kumtoa matongo;
    Na yeye kuendelea kwa furaha
    kuliko yeyote ninayemjua
    Akichekelea ha ha ha ha ha ha ...
    Na mimi kubaki kujiuliza
    Kuna siri gani inayomliwaza?
    Au ni kujua au kutojua?
    Furaha ya mtu ni furaha gani
    katika dunia inayomhini? 
    Ukali wa jua wamnyima zao
    Soko la dunia lamkaba koo;
    Dini za kudhani zamsonga roho
    Ayalimia matumbo ya waroho;
    Kuna jambo gani linamridhisha?
    Kama si kujua ni kutojua
    Laiti angalijua, laiti angalijua!
    (T.Arege)
    1. Eleza hali ya mzungumziwa katika shairi hili. (alama 4)
    2. Huku ukitoa mifano, onyesha aina mbili za uhuru wa kishairi uliotumiwa katika shairi hili. (alama 2)
    3. Fafanua aina tatu za taswira ukirejelea ubeti wa pili. (alama 3)
    4. Eleza umuhimu wa maswali ya balagha katika shairi hili. (alama 2)
    5. Bainisha vipengele vifuatavyo vya kimtindo katika shairi hili: (alama 3)
      1. tashhisi
      2. kinaya
      3. tashbihi
    6. Eleza toni ya shairi hili.  (alama 2)
    7. Bainisha nafsineni katika shairi lifuatalo. (alama 1)
    8. Changanua muundo wa shairi hili. (alama 3)
  2. Soma shairi lifuatalo kisha ujibu maswali.
    T.Arege: Mwili
    Leo kitaka nifike, natamani, ila wauma mwili
    Kwa kazi nihusike, samahani, unahiliki mwili
    Napenda nihesabike, makundini, ila huwezi mwili.
    Vitisho pamwe kelele, nanavicha, kwa nafsi na mwili
    Ule ugonjwa utimile, umechacha, na kuudhili mwili
    Msikose simile, magalacha, si gurudumu mwili.
    Lakini kamwe haiwi, kuvipata, vipande vyake mwili
    Sihofu kupata mawi, sitajuta, kupigania mwili
    Hata kufutwa sikawi, nitakita, kidete nao mwili.
    Kazi ninaithamini, ni hakika, akilini na mwili
    Ila kamwe siamini, kusagika, damu, jasho na mwili
    Uwele hususani, kioneka, nguvu hitishi.
    1. Eleza dhamira ya mtunzi wa shairi hili. (alama 4)
    2. Fafanua mbinu nne za lugha zilizotumiwa katika shairi hili. (alama 8)
    3. Eleza toni ya shairi hili. (alama 2)
    4. Ni nani anayezungumziwa na nafsineni katika shairi hili? (alama 1)
    5. Eleza bahari ya shairi hili kwa kurejelea vipande.(alama 1)
    6. Andika ubeti wa mwisho kwa lugha nathari. (alama 3)

SEHEMU E: HADITHI FUPI
K. Walibora na S.A Mohammed (Wah): Damu nyeusi na hadithi Nyingine.
"Mizizi na Matawi" (A.Abdullah Ali)

  1.    
    1. "Mwisho, naomba sote tusameheane kwa dhati."
      1. Fafanua muktadha wa dondoo hili.  (alama 4)
      2. Jadili umuhimu wa hotuba ya mzungumzaji katika hadithii hii. (alama 8)
    2. Onyesha jinsi hadithi, "Mke wangu" ilivyotumia kinaya kufanikisha ujumbe wake. (alama 8)


MARKING SCHEME

  1. Nasaba Bora na Majisifu wanashindwa kufuata mafundisho ya kidini waliyorithishwa na baba yao. Wanashindwa hata kuhusiana vyema kama ndugu.
  2. Fao anakosa kujidhibiti kama mtaalamu. Anahusiana kimapenzi na mwanafunzi wake na kumtunga mimba.
  3. Wazazi wa Fao wanaendeleza upujufu wa thamani ya mitihani, wanamlipia Fao kufanyiwa mtihani.
  4. Mwafrika anashindwa hata kutunza rasilimali aliyoachiwa na Mzungu. Nasaba Bora anayaachia ovyo makochi nyumbani mwake.
  5. Nasaba Bora anaonyesha kutokomaa kwa kuhusiana kimapenzi na Lowela na mwishowe kusababisha kuwehuka kwa bintiye Mashaka.
  6. Wasomi kama vile Majisifu badala ya kuendeleza utafiti, wanaufifilisha kwa kuiba miswada - anamwibia Amani.
  7. Nasaba Bora, badala ya kupigana na ukatili, ndiye anayeuendeleza. Anampiga Amani bila ithibati tosha kwamba anamwendea kinyume.
  8. Uongozi unashindwa kuwahakikishia raia usalama. Nasaba Bora anawatuma
    watu kuchoma nyumba ya akina Imani.
  9. Viongozi wanaendeleza dhuluma kwa waliopigania uhuru. Matuko Weye hajafidiwa kwa athari za Vita vya Dunia.
  10. Viongozi wanafifilisha vipawa vya vijana badala ya kuvikuza. Chwechwe Makweche licha ya kuiletea nchi sifa, anatelekezwa anapoumia mguu.
  11. Viongozi wanaendeleza ukiukaji wa haki za watoto. Nasaba Bora anampagaza Amani malezi ya Uhuru, anakitupa kitoto hicho mlangoni mwa kibanda cha Amani, licha ya baridi kali.
  12. Nasaba Bora anaendeleza matumizi mabaya ya mali ya umma. Anawataka raia kutoa pesa ampeleke mwanawe Madhubuti kwa masomo ng'ambo.
  13. Balozi, badala ya kumshauri vyema na kumkosoa Nasaba Bora, anamsifu kiongo, anasema kwamba Tomoko ina viongozi mashujaa wanaojali masilahi ya raia.
  14. Uongozi wa zahanati unawatelekeza wagonjwa. DJ anatelekezwa hadi anatoroka kutafuta matibabu badalia.
  15. Viongozi wanaendeleza udikteta; wanaongoza kwa vitisho. Tunaambiwa kwamba anenalo Nasaba Bora ndilo sheria.
  16. Wakuu wa mashirika ya kitaifa wanaendelea kuwasifu viongozi kupitia vyombo vya habari badala ya kuwakosoa. Majisifu alihakikisha kuwa jina la Nasaba Bora limetokea katika gazeti la Tomoko leo.
  17. Majisifu anashindwa kujidhibiti kama mwanataaluma; analewa hadi analala mitaroni.
  18. Viongozi wanabadhiri pesa zilizotengewa ujenzi wa hospitali na kusababisha kujengwa kwa zahanati tu. Wanaathiri vibaya utoaji wa huduma za afya.
  19. Viongozi wanatumia pesa zilizokusudiwa udhamini wa elimu ya watoto maskini kuwapeleka watoto wa familia tajiri kama vile Fao na Madhubuti kwa masomo ng'ambo.
  20. Viongozi wanapuuza afya ya wanyama wa kufugwa. Nasaba Bora hayachanji majibwa yake.
  21. Nasaba Bora anakosa uwajibikaji kwa raia. Anampita mama anayejifungulia njiani.
  22. Viongozi kuendeleza mauaji - chichiri na mame/mani.
  23. Viongozi kuwafungia raia bila hatia. Amani - uchochezi, Imani na Amani, Yusufu. Matuko Weye.
  24. Majisifu ni msomi lakini anashindwa kujiandalia mhadhara, uwasilishaji wake unatibuka kule Wangwani.
    10 x 1 = 10 Tanbihi: Dondoo limetolewa uk 124.
  1.    
    1.    
      1. Ni maneno ya Diwani III (Bw. Kheri)
      2. Anamwambia Siki.
      3. Wamo nyumbani mwa Diwani III.
      4. Siki amekuja kumwona Diwani III.
      5. Diwani III anamwambia Siki kwamba kuna mikutano ambayo yeye Diwani III hashirikishwi lakini anaamrishwa kutekeleza yaliyoafikiwa katika mikutanao hiyo.
      6. Siki anamwambia kwamba anastahili kukataa kutekeleza, ndipo Diwani III anasema haya.

        Tanbihi: Dondoo limetolewa uk.  4x1 = 4
        1. Tashbihi - kushindana naye ni kama kushindana na ndovu.
        2. Sitiari - utapasuka - utaumia/utaathirika vibaya.
        3. Taswira - mnyonge kushindana na mwenye nguvu.
          1 x 2 = 2
          Kutaja - 1
          Mfano - 1
    2.    
      1. Meya ana uwezo wa kutoa ahadi za uongo na kuaminika. Anadanganya kwamba dawa zimeagizwa, zi njiani na hali sivyo.
      2. Meya ana washauri wengi ambao wanamsikiliza. Raia/mtu mmoja tu hawezi kushinda.
      3. Matumizi ya vyombo vya dola. Watu wanapogoma au kulalamikia haki wanatawanywa na askari.
      4. Washauri wengine wa Meya kama vile mhubiri na Bili wana uhitaji na tamaa, hivyo hawawezi kumpinga Meya.
      5. Meya anawatenga washauri wanaopigania haki (k.v. Diwani) za wanyonge, kwa kudadisi mambo, hivyo anaishia kutoa uamuzi anaopendelea yeye.
      6. Ana mamlaka ya kisheria (Mayors Act na Riot Act) ambayo yanampa idhini ya kumchukulia hatua yeyote anayempinga. Meya anayatumia mamlaka haya vibaya/kujidumisha uongozini.
      7. Uwajibikaji wa pamoja unawafanya hata madiwani wanaoweza kumpinga Meya kutofanikiwa, kwani wale wengi huwa wamelitia sahihi alitakalo Meya.
      8. Hata Meya akiwadhulumu raia, wanamrudisha uongozini kwa kumpigia kura.
      9. Meya hana upinzani kutoka kwa wasomi kwani wanachelea kujihusisha na siasa. Siki anaiona siasa kuwa mchezo mchafu.
      10. Meya anatumia vitisho. Anadai kwamba wapo wasio na kazi, hivyo wataajiriwa.
      11. Anabuni kamati nyingi na kuwatia viongozi awatakao (wenye ushawishi) ili wamuunge mkono. (Katiba imempa mamlaka hayo)
      12. Ana mamlaka ya kutumia pesa/kupangia matumizi ya pesa au rasilimali za baraza. Anawaongezea mshahara walinda usalama ili waendelee kuulinda uongozi wake dhidi ya wapinzani. Anampa mhubiri sadaka ili amuunge mkono.
        Anawapeleka watoto wake ng'ambo ili kuepuka elimu duni.
      13. Ana nyenzo za kushawishi. Anatumia vyombo vya habari kueneza propaganda kuusifu na kuuondoa uongozi wake lawamani na kuibua hisia za kizalendo. Anataka idhaa ya kitaifa icheze nyimbo za kizalendo.
      14. Anawaondoa wanakandarasi wa awali ambao anahofia watapinga mipango yake/ana uwezo wa kuangamiza upinzani.
      15. Hata mji unapojaa uvundo yeye ana wafanyakazi kama vile Dida wa kunadhifisha kwake.
      16. Ndiye anayeamua kuhusu mikutano ya kuamulia masuala ya kisera, hivyo ana uwezo wa kuwatenga wapinzani wake kama vile Diwani III.
      17. Ndiye pekee mwenye jukumu la kuamua kuhusiana na matumizi ya viwanja vya umma hivyo anawagawia wanaomuunga mkono.
      18. Hata akitenda uhalifu ana nyenzo za kuuficha. Diwani (1) anaotoka na fimbo kisha kusemekana kwamba kumetokea vurugu fimbo ikaibiwa.
        7 x 2 = 14
  2.    
    1.    
      1. Ufisadi/kuhonga - Kummegea - kumgawia
        1 x 2 = 2
      2. Tanbihi: Dondoo limetolewa nk.27
      3. Meya anaidhinisha kuongezewa mishahara kwa madiwani ili wamuunge mkono. Hazina ya baraza inamomonyolewa zaidi. Madiwani hawampi ushauri wa kweli - uongozi unaanguka.
      4. Meya akamgawia Bili viwanja vinne. Bili anaishia kumpa ushauri wa kupotosha. Bili anaiba fimbo ya Meya.
      5. Meya anaifisidi hazina ya baraza kwa kumpeleka Bili na familia yake kwa burudani.
      6. Bili anamshauri Meya amwambie mwanakandarasi alishtaki baraza ili apewe fidia kwa kukatizwa kwa kandarasi Meya atapate fungu lake pia. Analifukarisha baraza,
      7. Meya anaunda kamati nyingi ili kuwahonga madiwani wanaomuunga mkono. Anaishia kushauriwa kufanya maamuzi yasiyo ya busara - anakataa kuwasikiliza wafanyakazi, mji unajaa uvundo, wageni wanaahirisha safari, uongozi wa Meya unaanguka.
      8. Meya anamhonga mhubiri kwa sadaka ili aendelee kumwombea. Mhubiri anashindwa kumkosoa Meya, uongozi unaanguka.
      9. Meya anamlipa Bili kwa huduma ambayo kwa kweli hajatoa. Huu unakuwa mzigo kwa hazina ya baraza.
      10. Raia wanachukua hongo kutoka kwa viongozi, wanawachagua na kuendeleza uongozi mbaya. Meya anamwambia Siki kwamba hata akitaka uongozi mara nne, tano na sita atapewa, kwani ana akili na uwezo wa ushawishi.
      11. Ufisadi unamfanya Meya kumshirikisha Bili katika maamuzi muhimu ya Baraza, na hali Bili si mfanyakazi wa Baraza. Bili anaishia kumpotosha Meya.
      12. Meya anaidhinisha Diwani I na Diwani II kulipwa overtime na hali hawajafanya lolote. Anaishia kumpa Bili upenyu wa kushauri wauze fimbo ya Meya.
      13. Ufisadi unamfanya Diwani I (Bwana Usalama ) kufanikisha wizi wa fimbo ya Meya. Anatoka nayo, kisha anatangaza kwamba kulitokea rabsha ikaibwa.
      14. Ufisadi unawafanya Meya, Diwani I, Diwani II na Bili kutotoa siri kuhusu njama ya kuiba fimbo ya Meya. Baraza linapata hasara.
      15. Meya anaidhinisha kutotozwa kodi kwa madiwani kwa kutaka wamuunge mkono. Hili linalinyima baraza pato na kuzidisha nakisi ya fedha.
      16. Meya anaifisidi mali ya umma kwa kumpeleka mkewe kujifungulia ng'ambo na wanawe pia kusomea ng'ambo. Anakosa kuboresha huduma za afya na elimu.
      17. Meya/Baraza linashughulikia masilahi ya kiafya ya madiwani kwa kutaka kuungwa mkono, na kuwapuuza wanyonge. Zahanati inakosa dawa, raia wanakufa; mf. Dadavuo.
      18. Meya anampa mhazili nafasi ya kazi licha ya kuwa hastahili. Anawanyima nafasi hiyo wanaostahili, k.v. wasomi.
      19. Diwani I na II wanamuunga Meya mkono kwa yote anayotaka ili wafaidi. Wanampotosha, uongozi unaanguka.
        8x1 = 8
    2. Vyombo vya usalama vinaendeleza uongozi kwa namna zifuatazo:
      1. Askari wanatawanya wafanyakazi wanapogoma, hivyo kudhibiti upinzani.
      2. Askari wanawatisha na kuwashinikiza watu wafanyakazi wakae nyumbani ili baraza lisipate picha mbaya ya ukosefu wa usalama.
      3. Madiwani wanatumiwa kupanga mikakati ya kumdumisha Meya mamlakani. Diwani I kwa mfano, anaendeleza propaganda kuhusu kujitolea kwa baraza kutetea demokrasia.
      4. Meya, ambaye anastahili kuwahakikishia raia usalama, unaidhinisha kuundwa kwa kamati zinazoongozwa na madiwani wenye ushawishi mkubwa. Hali hii inapuguza pingamizi.
      5. Kinara wa usalama, (Diwani I) anamshauri Bwana Uhusiano Mwema kuandaa tamasha kwa vijana ili kupalilia uzalendo kwa uongozi na Meya. (vi) Madiwani wanatumia vyombo vya habari kuimarisha uzalendo.
      6. Diwali II anasema kwamba mashindano ya vijana yatapeperushwa moja kwa moja kupitia vyombo vya habari.
      7. Katiba, inayopaswa kuhakikisha usalama inampa Meya mamlaka ya kukabiliana na wanaotetea haki, hivyo kumdumisha mamlakani.
      8. Madiwani na walinda usalama wanaostahili kulinda haki za raia wanaongezewa mshahara ili kuendelea kumuunga Meya mkono.
      9. Baraza linamtenga Diwani III katika maamuzi mabaya ambayo linafanya ili kukinga dhidi ya pingamizi. Askari wa baraza wanalinda masilahi ya Meya. Hata wanaposikia kelele za jadhba ya maombi wanakuja mbio kumhudumia.
      10. Mkuu wa usalama (Diwani I) anatumia vitisho (kuwafuta kazi) ili kuwadhibiti wafanyakazi wasigome.
      11. Diwani I anatoka na fimbo ya Meya afisini na kudai kuwa kulitokea vurugu ikaibwa. Hili linawatoa viongozi lawamani.
      12. Meya anapokisia kwamba walinda usalama wakitumia nguvu watasababisha upinzani anaamuru kwamba hataki watu wauawe (uk.19). Hii ni njia ya kujidumisha mamlakani.
        10 x 1 = 10
  3.    
    1.    
      1. Mwenye tumaini/tamaa - kubwa hamu
      2. Mwenye bidii - alfajiri na mapema, kutokwa na jasho
      3. Anayeyafurahia mandhari - anapotembea anasikiliza videge...
      4. Mtulivu - kuna siri gani inayomliwaza?
      5. Aliyedhulumiwa - soko la dunia lamkaba koo.
      6. Anayesagika kwa kazi ngumu kuwafaidi wenye tamaa-ayalamia matumbo ya waroho.
      7. Aliyeridhika - kuna jambo gani?
        4x1=4
    2.    
      1. Inkisari - babuze - babu zake
      2. Kufinyanga sarufi/miundo ngeu ya kisintaksia - kubwa hamu - hamu kubwa
        2 x 1 = 2
    3.    
      1. Taswira mnuso/harufu - rihi ya maua
      2. Taswira mguso - kumpapasa, kumbusu miguu
      3. Taswira ya usikivu - anasikiliza videge
      4. Taswira ya mwendo - yeye kuendelea kwa furaha.
        3 x1 = 3
    4. Maswali ya balagha yametumiwa:
      1. Kudadisi hali - kuna siri gani inayomliwaza? Kuna jambo gani linamridhisha? Au ni kujua au kutojua?
      2. Kuonyesha hali ya kinyume, kutokubaliana na jambo Furaha ya mtu ni furaha gani, katika dunia inayomhini?
      3. Kuzindua - furaha ya mtu ni furaha gani katika dunia inayomhini?
        2 x1 = 2
    5.    
      1. Tashhisi - umande kumbusu, miti kumpapasa, kumtoa matongo, upepo kumpepea
      2. Kinaya - nafsineni inafurahi ilhali dunia inaihini.
      3. Tashbihi- kama mtu aliye na kubwa hamu
        3 x 1 = 3
    6.    
      1. Toni ya uchungu - Furaha ya mtu ni furaha gani katika dunia inayomhini?
      2. Toni ya kuajabia/kushangazwa na jambo - kuna jambo gani linamridhisha?
      3. Kuhuzunisha/masikitiko/kuhurumia - laiti angalijua.
        1 x 2 = 2 kutaja - 1
        kueleza - 1
    7. Nafsineni
      1. mtetezi wa haki/aliyezinduka/anayelalamikia dhuluma ya wanyonge.
      2. mtu anayemtazama mkulima akipita.
        1 x 1=1
    8. Shairi lina beti tatu.
      1. Kila ubeti una idadi tofauti ya mishororo na beti nyingine.
      2. Kila mshororo una kipande kimoja.
      3. Shairi halina mpangilio maalum wa vina.
      4. Idadi ya mizani katika mishororo inatofautiana.
        3x1=3
  4.    
    1.      
      1. Dhamira ya mtunzi ni kuonyesha kuwa kazi ni shughuli muhimu ila haiwezi kuzingatiwa zaidi ya afya.
      2. Kuonyesha kuwa ipo haja ya kuipa afya kipaumbele kwa kuvikataa vitisho vya wenye kazi/waajiri.
      3. Kuonyesha dhuluma wanazofanyiwa wafanyakazi- vitisho pamwe kelele Kuukosoa uongozi dhalimu- kufutwa sikawi.
      4. Kuzindua wafanyakazi.
        4 x 1 = 4
    2. Hoja zifuatazo kujadiliwa:
      1. Shairi linatumia Kiswahili (lahaja) sanifu.
      2. Kuna matumizi ya sitiari - si gurudumu mwili.
      3. Uhaishaji/tashhisi - ugonjwa umepewa sifa ya kutenda-mwili kuudhili
      4. Matumizi ya nahau - viraka kuutia (ub.3)
      5. Matumizi ya inkisari - huwezi - hauwezi, ngeushuruti - ningeushuruti, sikawi - sikawii, kivipichakiko - ukivipachiko.
      6. Urudiaji wa maneno - kila mshororo unaishia kwa neno: mwili. 
      7. Udondoshaji wa neno - vitisho, pamwe kelele - vitisho pamwe na.
      8. Tabdila - utimile - utimie.
      9. Mazida - ukaungilika - ukaungika.
        4x2 = 8 kutaja 1 mfano 1
    3. Toni ya:
      1. hasira - si gurundumu mwili
      2. ukali - sihofu
      3. machungu - wauma mwili
      4. kukashifu - vitisho pamwe kelele
        1 x 2 = 2
        kutaja 1 mfano 1
    4. Mwenye kazi/mwajiri
      1 x 1= 1
    5. Ukawafi - vipande vitatu katika kila mshororo.
      kutaja 1 mfano 1   1x2
    6. Mimi kwa hakika ninaithamini kazi kwa akili na mwili isipokuwa siamimi kwamba inafaa kuteseka kwa kila hali. Hasa ugonjwa unapohusika kutumia nguvu hakuwezi kunitisha/siwezi kuogopa kutumia nguvu kujitetea.
      3 x 1 = 3
  5.    
    1.    
      1.      
        1. Maneno haya yalisemwa na Bimkubwa aliyemlea Sudi.
        2. Alikuwa akiwaambia Sudi na mtumishi wake Bi Kudura.
        3. Walikuwa nyumbani kwa Bimkubwa alikoishi na Sudi.
        4. Ni baada ya Bimkubwa kutambua kwamba Sudi alikuwa mtoto wake Bi Kudura.
        5. Bi Kudura alimweleza Bimkumbwa namna aliyvomtupa mwanawe pipani.
        6. Bimkubwa alijitolea kumfichulia Sudi siri hii na kuwataka wote wasameheane.
          4x1 = 4
          Tanbihi - dondoo limetolewa u.k. 118
      2. Umuhimu wa hotuba ya Bimkubwa.
        1. Imemfumbulia Sudi fumbo kubwa alilotaka kulifumbua - alitamani kumjua babake na asili yake.
        2. Kufichua udanganyifu wa Bimkubwa kuhusu Sudi. Kila wakati alipoulizwa na Sudi alikokuwa babake alimdanganya alifariki na kumwacha akiwa na mimba ya Sudi.
        3. Kufichua siri ya namna Bimkubwa alivyomwokoa Sudi. Kusawiri suala la uanaharamu - changamoto za kupata mtoto nje ya ndoa.
        4. Kuonyesha maudhui ya utu. Bimkubwa alimlea Sudi na kumsomesha kama mwanawe wa kuzaa.
        5. Kuonyesha uwajibikaji - Bimkubwa kumlinda na kumtunza mwana aliyemwokota kama mtoto wake wa kuzaa. Kuonyesha kwamba ni muhimu kukiri makosa, Bimkubwa anakiri alimdanganya Sudi lakini kwa kutaka aishi kwa furaha.
        6. Kusisitiza umuhimu wa kuomba msamaha na kusameheana kwa dhati.
        7. Kuonyesha busara ya Bimkubwa. Bimkubwa alikuwa amemwandikia Sudi mwanawe nyumba walimokuwa wakiishi na baada ya kufichua siri aliahidi kuhama na kuwaachia pamoja na Bi Kudura.
        8. Kuchimuza uozo wa kijamii. Bi Kudura alimtupa mwanawe. Kuonyesha suala la haki za watoto - Bimkubwa kumlea Sudi baada ya kumwokoa.
        9. Kimuundo ni kitulizo. Suluhisho la mgogoro wa hadithini linachimuzwa pale tunapoona maridhiano ya mwana na mama, na kudokezewa mkondo wa maisha ya baadaye ya Bimkubwa
        10. Kuendeleza maudhui ya elimu. Sudi amesoma hadi chuo kikuu.
        11. Kuonyesha utu na uwajibikaji wa Sudi. Anamtunza vyema Bimkubwa.
        12. Kuonyesha bidii ya Sudi. Anasoma hadi chuo kikuu.
          8 x 1 = 8
    2.    
      1. Msimulizi kuwazia kwamba kwa vile Aziza hakusoma, hatakuwa mjuaji, atakuja kumdhibiti. Inatokea kwamba Aziza ndiye anayemdhibiti.
      2. Msimulizi anaikashifu tabia ya Fedhele; kuwa yu nje usiku na hali msimulizi yu palepale nje wakati huo.
      3. Msimulizi amesoma, na hali anafungwa na mawazo ya kizamani. Anamkashifu Fedhele na rafiki yake kwa kuandamana na kijana wa kiume.
      4. Ni Kinaya kwamba Msimulizi anawaza kwamba waliosoma ndio wenye utambuzi, lakini anakuja kugundua kwamba Aziza ana utambuzi wake mwenyewe ulioshinda wa wale waliosoma.
      5. Ni Kinaya kwamba Msimulizi anataka kumtia Aziza mjini/lakini hataki Aziza aambukizwe mambo ya mji(afanye wafanyavyo wana mji).
      6. Msimulizi alitaka kumfunza Aziza maisha ya kistaarabu lakini Aziza anaishia kumfunza kuwa mtu asiyefanya kazi si mume.
      7. Ni kinaya kwa waliosoma kungojea kujituma kwenye kazi duni kama vile uboi, huku wakidharau kazi kama vile ukwezi ambazo zingewaimarisha.
      8. Msimulizi kasoma, ila Aziza ana mawazo mapevu kumshinda. Hata anahisi kwamba Aziza kamzuga. Msimulizi anakataa kumwoa Seluwa kwa sababu ya kuwa kidomo, baadaye anakuja kumwoa Aziza ambaye anamdhbiti kwa maneno.
      9. Inatarajiwa kwamba Aziza anapoolewa atafuata utamaduni wa familia ya mume, lakini anashikilia utamaduni wa kwao.
      10. Msimulizi anakashifu kanzu fupi ya Fedhele na pia hapendezwi na wanaojigubika k.v. Salma.
      11. Msimulizi hataki kumwoa mwanamke aliyestaarabika kwa vile ndoa zao zimesambaratika ilhali yake inaishia kusambaratika na hali mkewe hajastaarabika.
Join our whatsapp group for latest updates

Download KCSE 2015 Kiswahili Karatasi ya Tatu with Marking Scheme.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?

Join our community on:

  • easyelimu app
  • Telegram
  • facebook page
  • twitter page
  • Pinterest