Kiswahili Paper 3 Questions and Answers - KCSE 2022 Mock Exams Set 1

Share via Whatsapp

MAAGIZO;

  • JIBU MAWSALI MANNE
  • SWALI LA KWANZA NI LA LAZIMA
  • USIJIBU MASWALI MAWILI KATIKA SEHEMU MOJA
  • KILA SWALI LINA ALAMA 20.

SEHEMU YA A
SWALI LA KWANZA

Soma shairi lifuatalo kisha jibu maswali yanayofuatia.

Tusitake kusimama, bila kwanza kutambaa
Au dede kuwa hima , kabula hatujakaa
Tutakapo kuchutama, kuinama inafaa
Tujihimu kujinyima, makubwa kutoyavaa

Tusitake kuenenda , guu lisipokomaa
Tujizonge na mikanda, inapochangiza njaa
Na mazuri tukipenda , ni lazima kuyandaa
Tujiase kujipinda , kujiepusha na balaa.

Tusitake uvulana , au sifa kuzagaa
Tukishikiye nyonga sana, tunuiyapo kupaa
Kama uwezo hapana , tutolee dagaa
Tujiase hicho kina, maji yanapojaa

Tusitake vya wenzetu ,walochuma kwa hadaa
Wanaofyatua vitu, na kisha vikasambaa
Uwezo hatuna katu, umaskini fazaa
Tujihimu kula vyetu, siendekeza tamaa.

Mtaka kuiga watu , hufata kubwa rubaa
Vyao vijalie kwetu , vifaa vingi vifaa
Tunamezwa na machatu, tusibakishwe dhiraa
Tujihimu kilo chetu, hata kama twapagaa.

Maswali;

  1. Tambua mkondo wa shairi hili.(alama 2)
  2. Tambua bahari ya shairi kwa kuzingatia ;
    1. vina
    2. mishororo
    3. Vipande kaitika kila mshororo.( alama 6)
  3. Ni nini dhamira ya shairi hili.(alama 2)
  4. Thibitisha shairi hili ni la kiarudhi. (alama 4)
  5. Kwa kutolea ithibati ni ni uhuru gani wa ushairi uliotumika katika shairi hili.(alama 4)
  6. Eleza dhima urudiaji katika shairi hili.(alama 2)

SEHEMU YA B RIWAYA:CHOZI LA HERI NA ASSUMPTA MATEI
Jibu swali la 2 au la 3.

  1.  
    1. … haya imekuandama tangu usiku ukimtongoza fulani; siku za kuchora ramani ya Afrika kwa vyanda vya miguu hadi sasa? Ama ni hizo mvi unaficha ? Nasikia ile mid-life crisis ikawashika wazee ndiyo hivyo;
      1. Weka dondoo hili kwenye muktadha wake. (alama 4)
      2. Tambua mbinu zozote tatu za kimtindo kwenye dondoo hili.(alama 4)
      3. Jadili sifa zozote sita za msemewa katika dondoo hili.(alama 6)
    2. Sauna amechangia vipi katika kuendeleza ploti katika Riwaya ya Chozi la Heri.(Alama 6)
  2. Tambua mandhari yoyote manne na umuhimu wake katika Riwaya ya chozi la Heri. (alama 20)
    SEHEMU YA C: TAMTHILIA YA KIGOGO
    Jibu swali la 4 au la 5.
  3. Mwandishi wa tamhtilia ya Kigogo amefanikisha katika kutumia ishara ili kufanikisha maudhui.(alama 20)
  4. ”Mimi sili makombo kama kelbu!Nilishakunywa chai ya mke wangu nikaridhika.”
    1. Eleza muktadha wa dondoo hili.(alama 4)
    2. Jadili umuhimu wa msemaji katika tamthilia hii.(alama 6)
    3. Wanasagamoyo wamefanywa kelbu kula makombo.Thibitisha kauli hii.(alama 20)

SEHEMU YA D. HADITHI FUPI
Jibu swali la 6 au la 7.

  1.  
    1. Elezea matatizo yanayowakabili wanafunzi katika azma yao katika kupata elimu kwa kuzingatia Hadithi ya ‘Mtihani wa maisha’.(alama 10)
    2. Fafanua shibe inavyowamaliza Waafrika katika hadithi ya ‘Shibe Inatumaliza’
  2.  
    1. ”Jijini ni kuzuri.Kuna majumba makubwa , utapanda magari mazuri ya marafiki zetu, utakula vyakula vitamu na kupewa nguo za fahari.Utapelekwa shule kusoma na kuandika.”
      1. Jadili mukadha wa dondoo hili. (alama 4)
      2. Eleza taswira zinazojitokeza katika dondoo kwa kutoa mifano. (alama 3
      3. Aliyoambiwa msemewa ni kinyume cha yaliotokea .Eleza.(alama 8)
      4. Wahusika mbalimbali katika dondoo hili wametumia njia nyingi kukabiliana na matatizo yanayowakumba.Zijadili.(Alama 5)

SEHEMU YA E. FASIHI SIMULIZI

  1. Ulumbi ni nini? (alama 2)
  2. Eleza sifa za mlumbi(alama 6)
  3. Fafanua aina zozote sita za wahusika katika Fasihi Simulizi.(alama 6)
  4. Taja mambo ambayo huzingatiwa kufanikisha uwasilishaji wa ngano katika Fasihi Simulizi.(alama 6) 

MARKING SCHEME

SEHEMU YA A

SWALI LA KWANZA

Soma shairi lifuatalo kisha jibu maswali yanayofuatia.
Tusitake kusimama, bila kwanza kutambaa
Au dede kuwa hima , kabula hatujakaa
Tutakapo kuchutama, kuinama inafaa
Tujihimu kujinyima, makubwa kutoyava
 
Tusitake kuenenda , guu lisipokomaa
Tujizonge na mikanda, inapochangiza njaa
Na mazuri  tukipenda , ni lazima kuyandaa
Tujiase kujipinda , kujiepusha na balaa.
 
Tusitake uvulana , au sifa kuzagaa
Tukishikiye nyonga sana, tunuiyapo kupaa
Kama uwezo hapana , tutolee dagaa
Tujiase hicho kina, maji yanapojaa
 
Tusitake vya wenzetu ,walochuma kwa hadaa
Wanaofyatua vitu, na kisha vikasambaa
Uwezo hatuna katu, umaskini fazaa
Tujihimu kula vyetu, siendekeza tamaa.
 
Mtaka kuiga watu , hufata kubwa rubaa
Vyao vijalie kwetu , vifaa vingi vifaa
Tunamezwa na machatu, tusibakishwe dhiraa
Tujihimu kilo chetu, hata kama twapagaa.
 
Maswali;
  1. Tambua mkondo wa shairi hili.(alama 2)
    • Hili ni shairi la arudhi-la kimapokeo. - alama 2
  2. Tambua bahari ya shairi kwa kuzingatia;
    1. Vina
      • Ni shairi la ukara kwani  vina vya kati vinabadilika badilika na vya mwisho havibadiliki.-(alama 2)
    2. mishororo
      • Ni shairi la tarbia-lina mishororo minne katika kila ubeti (alama 2
    3. Vipande kaitika kila mshororo
      • Hili ni shairi la mathinawi-kila mshororo una vipande viwili (alama 2)
  3. Ni nini dhamira ya shairi hili.(alama 2)
    • Dhamira ya shairi hili ni tahadhari dhidi ya tama ya kuiga watu wengine kabla ya kupata vitu tunavyovitaka. (alama 2)
  4. Thibitisha shairi hili ni la kiarudhi. (alama 4)
    • Lina mishororo minne katika kila ubeti
    • Lina vipande viwili katika kila mshororo
    • Lina vina 
    • Limegawika katika beti     alama 4
  5. Kwa kutolea ithibati ni  ni uhuru  gani  wa ushairi uliotumika katika  shairi hili.(alama 4)
    • tabdila-kabula-kabla, tushikiye-tushikie, tunuiyapo-tunuiapo
    • inkisari-walochuma-waliochuma, siendekeze-tusiendekeze, kujepusha-kujiepusha
    • mazda-kuenda-kwenda
    • kikale-vijaile-vimejaa
    • kuboronga sarufi-au dede kuwa hima-au kuwa hima wakati tungali dede, kuinama inafaa-inafaa kuinama
      zozote 4*1=4
  6. Eleza dhima urudiaji  katika shairi hili.(alama 2)
    • urudiaji wa sauti-/a/ kuleta rithimu ya shairi na urari wa vina
    • urudiaji wa neno –tusitake –kusisitiza ujumbe
    • urudiaji wa silabi-tu-rithimu  katika shairi
      zozote 2*1=2

SEHEMU YA B RIWAYA:CHOZI LA HERI NA ASSUMPTA MATEI
Jibu swali la 2 au la 3.

  1.  
    1. … haya imekuandama tangu usiku ukimtongoza fulani; siku za kuchora ramani ya Afrika kwa vyanda vya miguu hadi sasa? Ama ni hizo mvi unaficha ? Nasikia ile mid-life crisis ikawashika wazee ndiyo hivyo;
      1. Weka dondoo hili kwenye muktadha wake. (alama  4)
        • Msemaji  ni Terry mawazoni mwa Ridhaa.
        • Msemewa ni Ridhaa 
        • Ridhaa yuko kwenye mawazo uwanjani wa ndege wa Rubaa
        • Anakumbuka maisha yake mkewe na aila yake huku akimngoja Mwangeka awasili anayetoka ng’ambo.
      2. Tambua mbinu zozote tatu za kimtindo kwenye dondoo hili.(alama 4)
        • Taswira mwono-kuchora Ramani ya Afrika
        • Maswali balagha-Hadi sasa?
        • Kuchanganya ndimi-mid-life crisis
        • Mbinu rejeshi-Ridhaa kukumbuka yaliotokea kitambo.
      3. Jadili sifa zozote sita  za msemewa katika dondoo hili.(alama 6)
        • Ni mwenye bidii-alisoma hadi akahitimu kuwa daktari
        • Ni mkarimu-aliwafadhili kimasomo wapwa wa Mzee Mkedi
        • Ni mwajibikaji –alitafuta njia mbadala ya kuchimba misala badala ya kutumia sandarusi
        • Ni mbaraza-alikuwa na uhusiano mzuri na Bibi yake Terry na wanawe
        • Ni mlezi mwema-aliwasomesha watoto wake hadi Mwangeka akahitimu chuo kikuu
        • Mshauri mzuri-anamshauri Mwangeka aoe tena baada ya kumwomboleza bibi yake kwa muda.
          Swali funge-za kwanza 6*1=6
          Kadiria jibu la mwanafunzi
    2. Sauna amechangia vipi katika kuendeleza ploti katika Riwaya ya Chozi la Heri.(Alama 6)
      • Anapata mimba baada ya kubakwa na babake wa kambo Maya
      • Mamake anamkanya kutompaka babake wa mashuzi
      • Amalazimisha kuavya mimba
      • Baadaye Sauna anaamua kutoroka kutoka kwao
      • Anajiingiza kwa biashara haramu na bibi  Kangara ya ulanguzi wa watoto
      • Anapata kazi kwa akina Mwaliko na baada ya mama yao Naomi na baba yao Lunga Kiriri kuaga awamwiba Mwaliko na Dick na kuwaingiza katika biashara haramu
      • Baadaye Sauna na bi Kangara wananaswa na mkono mrefu wa serikali na kutiwa mbaroni
        Zozote sita=6
  2. Tambua mandhari  yoyote manne  na umuhimu wake  katika Riwaya  ya chozi la Heri. (alama 20)
    1. Nyumbani kwa Ridhaa 
      • Kuzua maudhui ya vifo- aila yake innangamizwa
      • Maudhui ya utani-alivyotaniana na mkewe Terry
      • Ushirikina- Ishara zilizoonyesha maafa-mlio wa bundi
      • Ukabila-Mzee Kedi kuangamiza kwa sababu ni’ mfuata mvua’
      • Kuzua tabia ya wahusika –Mzee Kedi –mkabila
    2. Msitu wa Mamba
      • Kuendeleza ploti-Kaizari anasimulia yaliowakuta baada ya kutawazwa kwa Mwekevu
      • Kudhihirisha matatizo yanayowakumba wakimbizi wa ndani kwa ndani kama njaa, maradhi, makaazi duni, ukosefu wa vyoo, vifo vya watoto
      • Kudhihirisha usawa miongoni mwa watu ambao awali walikuwa na nyadhifa mbalimbali ; maskini kama Makiwa na  matajiri kama Ridhaa na Kaizari
      • Kusawiri jinsi ukabila huasambaratisha ndoa- Selume
      • Kuonyesha juhudi zinazofanywa  kukabiliana na matatizo;
        Vyoo-ujenzi wa long-drop
        Njaa- vyakula vya msaada kutoka kwa mashirika
      • Kudhihirisha matatizo yanayotokana na vururgu baada ya uchaguzi jinsi yalivyosimuliwa na Kaiari
      • Kituo cha Mwanzo mpya
      • Kuonyesha changamoto zina zokumba hospitali za umma-Selume  anashangaa mama alivyoweza kustahimili matatizo kama vile ukosefu wa glavu hospitalini
      • Kuangazia suala la ufisadi-dawa zilizotegemewa hospitali zinauzwa na wasimamizi wa hospitali –Ruzuku kutolewa kwa wasiostahili
      • Kuendeleza ploti-Kupitia sadfa –kituo kinakamilika wakati Selume anajiuzulu anapata kazi katika kituo hiki na mkondo wa maisha yake kubadilika.
      • Kuonyesha ukosefu wa uwajibikaji wa wasimamizi wa taasisi za umma-Hospitali haijalipia umeme
      • Kuonyesha migogoro inayosababishwa na tama ya rasilimali-Mgonjwa analemazwa  katika mapigano ya kung’ang’ania ardhi
    3. Mandhari ya shule ya  Upili  ya Tangamano
      • Kuendeleza ploti wakati wasichana hawa wanavyohadithiana matatizo waliokumbana katika maisha yao
      • Ufaafu wa anwani kila msichana anapata heri katika shule hii kama Zohali
      • Madhui ya ukarimu-Mtawa Pacha alivyomsaidia Zohali na Kitoto chake
      • Umu naye kupitia kwa shule hii ana matumaini ya kusoma hali kuwa wakili wa kutetea haki za watoto
      • Kuibua tabia za wahusika wengine-Mamake Zohali alishindwa kumsaidia Zohali alipopata ujauzito mpaka akatoroka kwa sababu ya kazi nyingi.
      • Shuleni na masimulizi yao yanaibua toni ya matumaini- kwamba kuna maisha zaidi ya matatizo walioyapitia awali
    4. Mandhari katika uwanja wa ndege
      • Chozi la heri –kwamba hata ingawa familia yake ililiangamia katika moto-Mwanawe Mwangeka yu hai kwa sababu alikuwa ughaibuni
      • Mbinu rejeshi-Ridhaa analivyokumbuka siku ya kuhawailishwa kutoka Msitu wa Mamba hakuwa na matumaini ya maisha bora kwani hakuwa na mwenzi wala mtoto wa kuendea.
      • Ukabila –kupitia kwa Ridhaa selume hakujua ataenda wapi kwani mumewe alikuwa ameoa msichana wa kikwao.
      • Sifa ya Ridhaa –mfariji-alimkumbusha Selume kuwa angalau mtoto wake Srah alikuwa hai na salama kwa babake ilhali yeye familia yake ilikuwa imeangamia
      • Alipata mafunzo ya umuhimu wa kutangamana na watu wakiwa wakimbizi-thamani ya binadamu.
      • Ni katika Msitu wa Mamba  Ridhaa alipata ushauri nasaha na kuweza kukabiliana na  tatizo lake la shinikizo la damu  lililotokana na mshutuko wa kupoteza jamaa yake na mali yake kwa dafrao moja.

SEHEMU YA C: TAMTHILIA YA KIGOGO
Jibu swali la 4 au la 5.

  1. Mwandishi wa tamhtilia ya Kigogo  amefanikisha katika kutumia ishara ili kufanikisha maudhui.(alama 20)
    • Fimbo ya Kenga yenye kichwa cha nyoka ni ishara ya jinsi alivyokuwa katili kwa raia.
    • Kitendo cha Majoka cha kuzungumza na babu yake anapozirai ni ishara kuwa wafu walikuwa wakimwita madhali ndiye aliyekuwa amewaua.
    • Majoka kuvaa mkufu  wa  shingoni wenye kidani cha umbo la swila ni ishara namna Majoka alivyokuwa hatari kwa maisha ya raia wa Sagamoyo.
    • Kilio na machozi mengi ndani ya ziwa lililofunika  damu ni ishara ya raia waliouliwa na Majoka wanalilia hali yao.
    • Kutojaa kwa raia ilivyo kawaida katika mkutano wa kudumisha sherehe za Uhuru pamoja na siku ya kuzaliwa kwa Majoka kutokana na uongozi wake dhalimu.
    • Hali ya Majoka kujiona ndani ya ziwa lililofurika damu ni ishara ya mauaji mengi ya raia aliyokuwa  akitekeleza katika uongozi wake.
    • Damu ya Jabali anayoiona Majoka ikitiririka  mikononi mwake akiwa amezirai ni ishara kuwa ndiye aliyemuua Jabali.
    • Bastola ya Majoka n silaha au chombo cha kuwatishia watawaliwa na watetezi wa  dhidi ya maovu ya kiongozi.
    • Chai ya mkandaa-kinywaji cha watu maskini.
    • Nyoka –kuashiria ushirikina na ukatili wa Majoka.
    • Chai ya maziwa –kinywaji cha  watu tajiri.
    • Chombo cha safari ya angani huashiria uongozi au madaraka.Majoka ni mojawapo wa marubani  yaani yeye ndiye kiongozi ambaye huwalaghai anawaongoza.
    • Embe lililoiva kupita kiasi ni ishara ya kuzorota kwa uchumi wa Sagamoyo.
    • Gari la kifahari la Kenga-hali ya utajiri wa kupindukia na ubepari.
    • Hoteli za kifahari-huashiria sherehe ya tabaka la juu.
    • Kinyago –kuashiria hali ya viongozi kupenda uluwa. Kupenda makuu kwa kutaka majina ya watu wa mbari zao na zaidi kusifiwa milele kwani walipigania uhuru.
    • Kiti cha kifahari cha Majoka –kuashiria tabaka la juu kiuchumi, tabaka lenye starehe kutokana na utajiri wake.
    • Mbuyu ni makao ya shetani –kuashiria dhuluma za kiongozi –Kenga anawahutubia wananchi chini ya mti wa mbuyu.
    • Ndoto ya Tunu-ufunuo wa madhila ya wapiginiaji /wanajamii wakati a uongozi  uliopita  wa babake Majoka , Marar bin Ngao.
    • Pombe ni ishara ya utovu wa maadili katika jamii.
    • Redio-kuashiria maendeleo ya kiteknolojia yanayotumiwa na viongozi kujikuza wenyewe.
    • Televisheni-ishara ya maendeleo katika uwanja wa mawasiliano.Ni kinaya kwa sababu hatuoni maendeleo haya ya kimawasiliano yakichangia kuboresha hali za maisha ya  mwananchi  wa kawaida.
    • Soko chafu-ni ishara ya uozo wa kimaadili wa kisiasa.
    • Sumu ya nyoka –ishara ya dawa ya kulevya na masaibu yanayotokana na kunyanyaswa kwa wafanyikazi wa tabaka la chini na viongozi.
    • Kinyago cha mwanamke- kuonyesha kuwa mwanamke pia ana uwezo wa kuwa kiongozi.
    • Keki- ni ishara ya rasilimali za nchi- ambapo wananchi wanapata makobo tu huku mgao mkubwa ukiwaendea viongozi
    • Maziara kujaa-kuashiria kuuawa kwa watu wengi  chini ya uongozi wa Mjoka.
    • Uvundo sokoni-kuashiria kutowajibika kwa viongozi katika kusafisha soko hata baada ya kuchukua kodi-
      Zozote 20*1=20
  2. ”.Mimi sili makombo kama kelbu!Nilishakunywa chai ya mke wangu nikaridhika.”
    1. Eleza mukatadha wa dondoo hili.(alama 4)
      • Msemaji ni Sudi
      • Msemewa ni  Boza na Kombe
      • Wakiwa katika karakana ya uchongaji  Katika Soko la Chapakazi
      • Ni baada ya Sudi kususia makombo ya keki iliyotolewa  na Kenga kwa kuwa alijua kulikokuwa keki kubwa.
    2. Jadili umuhimu wa msemaji  katika tamthilia hii.(alama 6)
      • Kuendeleza ploti-Anapotumia simu yake ya rununu kama redio kumsikiza matangazji kuhusu sherehe ya kuadhimisha uhuru
      • Kukuza maudhui ya uzalendo-pamoja na Tunu kutetea haki za wananchi
      • Kukuza sifa za wahusika wengine-Ashua ni kigeugeu anapota kumtaliki  akiwa kizuizini
      • Anaendeleza ukosefu wa kazi-baada yake kuhitimu kama mwana sharia bado hajapata kazi ya taaluma yake
      • Ni kielelezo cha wananchi wazalendo-anakataa kuchonga kinyago baada ya kuamrishwa na Kenga ili afaidike peke yake-
      • Ni kielelezo cha watetezi wa haki katika jamii- anashirikiana na Tunu kutetea haki za wanasagamoyo dhidi ya uongozi dhalimu wa Majoka.
        Hoja zozote 6*1=6
    3. Wanasagamoyo wamefanywa kelbu kula makombo.Thibitisha kauli hii.(alama 10)
      • Wanasagamoyo wanafungiwa  soko ambalo lilikuwa  adimu kwao 
      • Wanasagamoyo wanapandishiwa bei ya bidha a katika kioski ya soko
      • Vijana wanauawa wakati wa migomo
      • Wanasagamoyo wanafungiwa vyombo vya habari na mitandao ya kijamii
      • Wanasagamoyo wanarushiwa vijikaratasi vya kuwataka kuhama Sagamoyo-Siti na Kombe
      • Walimu wanaongezewa mishahara na kupandishiwa kodi wakati huo huo
      • Majoka ananyakuwa soko la Chapa kazi kwa lengo la kujenga Hoteli yake ya kifahari.
      • Majoka anawagawia vikaragosi wake ardhi –Kenga
      • Majoka anafungulia  biashara ya ukataji wa miti na kusababisha ukame kwa sababu ya kukauka kwa mito na maziwa.
      • Pombe haramu inawafisha walevi baada ya mama Asiya kupewa kibali na Majoka kuiuza.
        zozote10*1=10

SEHEMU YA D. HADITHI FUPI
Jibu swali la 6 au la 7.

  1.  
    1. Eleza  matatizo   yanayowakabili wanafunzi katika azma yao katika kupata elimu kwa kuzingatia Hadithi ya ‘Mtihani wa maisha’.(alama 10)
      • Kuanguka mtihani
      • Kutooelewa wanayosomeshwa
      • Wasiopita mtihani wnadharauliwa
      • Shinikizo kutoka kwa wazazi , marafiki kufanya vizuri katika mtihani
      • Kutembea mwendo mrefu kwenda shuleni
      • Kulinganishwa na ndugu zao waliofanya vizuri katika mtihani
      • Kulaumiwa na wazazi unapoanguka mtihani
      • Aibu ya kuanguka mtihani
      • Kukata tama maishani wanapofeli mitihani
      • Wazazi kuwaadhibu wanao wanapofeli mtihani
      • Baadhi ya walimu kuwadharau wanafunzi wasiofanya vizuri masomoni
    2. Fafanua Shibe inavyowamaliza Waafrika katika hadithi ya ‘Shibe Inatumaliza’(alama 10)
      • Bwana Mambo ana kazi isiyo maalumu serikalini lakini analipwa.
      • Mzee Mambo hijipakulia mshahara atakavyo
      • Magari ya serikali yanatumika katika sherehe ya kibinafsi ya Mzee Mambo
      • Anatumia pesa nyingi kutengeneza sherehe isiyo na maana
      • Vyakula (rasilimali) kwenye shereh vianliwa lakini walioviandaa hawajulikani
      • Wananchi wanatazama tu chakula kinapoliwa( rasilimali)
      • Mbura na Sasa wanakula chakula kilafi ,wanarudia mara tau( ubadhirifu wa mali ya umma)
      • Dj analipwa mamilioni ya mapesa kwa kuwa Dj katika sherehe hii
      • Dj ana duka la dawa ambalo mtaji wake ni Bohari kuu la dawa za serikali
      • Dj anapata huduma za serikali za muundomisingi zote bure ilhali wananchi hawazipati
      • Serikali haijali lawama inaporuhusu wananchi wake kuuziwa bidhaa mbaya kama mchele wa bsimati
      • Sasa na Mbura ni mawaziri katika wizara moja na hawajali
        Zozote 10*1=10
  2.  
    1. ”Jijini ni kuzuri.Kuna majumba makubwa , utapanda magari mazuri ya marafiki zetu, utakula vyakula vitamu na kupewa nguo za fahari.Utapelekwa shule kusoma na kuandika.”
      1. Jadili mukadha wa dondoo hili. (alama 4)
        • Msemaji ni Babake Bogoa
        • Wanoambiwa ni kina Sebu , Kazu ,Temu na Sakina
        • Wako katika club Pogopogo
        • Bogoa alikuwa anawasimulia yaliomfika kabla ya kutolewa kwao.
      2. Eleza taswira zinazojitokeza   katika dondoo kwa kutoa mifano. (alama 3)
        • Taswira oni-majumba makubwa makubwa
        • Taswira mwonjo-utakula vyakula vitamu
        • Taswira mwendo-utapelekwa shule
      3. Aliyoambiwa msemewa  ni kinyume cha yaliotokea .Eleza.(alama 8)
        Masaibu ya Bogoa
        • Kula kwa viage/sufuria wengine wakila kwa sahani
        • Kuchomwa kwa kijinga alipokuwa akioka maandazi halafu akalala
        • Kukatazwa asiende shule kama watoto  wengine
        • Kunyimwa ushirika  wa watoto wa Bi, Sinai, wasicheze pamoja
        • Kufanyishwa kazi ngumu kama kuteke maji, kuchanja kuni, kufua
        • Kuchapwa sana alipochelewa kurudi baada ya kupewa nafasi ya kutoka kidogo
        • Kutishiwa kukatwa ulimi iwapo angesema kwa yeyote yaliojiri humo nyumbani
        • Kunyimwa ushirika na wazazi wake walipokuja kumwona
        • Kulazimika kuamka mapema kama mtoto mdogo
        • Kula makoko ya chakula ua makombo
          Zozote 8*1=8
      4. Wahusika mbalimbali katika dondoo hili wametumia njia nyingi kukabiliana na matatizo yanayowakumba.Zijadili.(Alama 5)
        • Bogoa kupelekwa kulelewa kwa Bi. Sinai kwa sabau ya uamskini
        • Kuhama kwa Bogoa kutoka kwa Bi, Sinai ili kuyaepuka mateso
        • Bogoa kumwaga dukudku zake kwa kina Sebu ninjia ya kutoa kihoro cha aliyopatia kwa Bi.Sinai
        • Bogoa kutia bidii katika maisha yake kama sonara ili kujitoa katika hali ya uchochole
        • Bogoa alimwoa Sakina ili amwondolee upweke pale Tinya.
        • Bogoa kuwasemehe wazazi wake na bi.Sinai
          Zozote 5*1=5

SEHEMU YA E. FASIHI SIMULIZI

  1. Ulumbi ni nini? (alama 2)
    • Ni uhodari wa kutumia lugha kwa ufundi wa kipekee.
  2. Eleza sifa za mlumbi(alama 6)
    • Mkamamavu
    • Mcheshi
    • Mwenye kumbukumbu nzuri
    • Mbunifu
    • Mwenye kuielewa hadhira
    • Mwenye ufasha wa lugha
    • Mfaraguzi
    • Mwenye kuelewa mazingira ya hadhira yake
    • Mwenye uwezo wa kushirikisha hadhira
    • Mbaraza
      (Mwanafunzi asitaje hoja tu-aelezee)(alama 8)
  3. Fafanua aina zozote sita za wahusika katika Fasihi Simulizi.(alama 6)
    • Fanani-anayetunga  na kuwasilisha Fasihi Simulizi
    • Hadhira-kusiliza , kutazama , kushiriki kwa kuimba, kuuliza maswali, kutegua vitendawili, kupiga makofi nk.-kuna hadhira tui na hai
    • Wanyama wanofanya kama binadamu na kuwakilisha sifa kama vile ujanja ,ulaghai, tama na ujinga na kuna wale wanaobakia wanyama tu.
    • Binadamu
    • Mazimwi na majitu-viumbe wenye matendo na maumbile ya kutisha kama vile jicho kubwa moja, vichwa viwili au zaidi, nusu mtu na nusu mnyama wenye tama liyokithiri ya kuweza kumeza kila kitu, kuhifadhi na kutunza binadamu anayewapendeza.
    • Wahusika vitu visivyo na uhai kama mawe, miti, vijaluba, vibuyu-hutumiwa kuibua imani za kidini za jamii husika.
    • Mizimu-roho za waliokufa  ambao hutembea na huathiri binadamu
    • Miungu-viumbe wenye uwezo mkubwa dhidi ya binadamu na hutumika sana katika mighani na visasili
      Swali funge=za kwanza 6*1=6
  4. Taja mambo ambayo huzingatiwa kufanikisha uwasilishaji wa ngano katika Fasihi Simulizi.(alama 6)
    • Lazima kuwe na fanani
    • Kuwe na hadhira
    • Pawepo na ngano yenyewe ya kughanwa
    • Pawe na pahali pa kuaghania ngano yenyewe
    • Mganaji awe na uwezo wa kuiteka makini ya hadhira kutoka ulimwengu halisi hadi wa kubuni
    • Fanani awe na uwezo wa kuishirikisha hadhira wakati  wote wa usimulizi ili kuondoa ukinaifu
    • Kiimbo-aweze kupandisha nakushikisha sauti ili kuibua hisia tofauti tofauti
    • Awe mfaraguzi
    • Awe jasiri wa kuweza kusimulia hadithi yake bila uoga
      Zozote6*1= 6         
Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Paper 3 Questions and Answers - KCSE 2022 Mock Exams Set 1.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?