Kiswahili Questions and Answers - Form 4 Mid Term 1 Exams 2023

Share via Whatsapp
MAAGIZO    
  • Jibu maswali yote.
  • Majibu yaandikwe kwa lugha ya Kiswahili.
  1. UFAHAMU  (ALAMA 15)
    Soma taarifa ifuatayo kisha ujibu maswali uliyopewa.

    Taifa la Kenya limekuwa  na tatizo la njaa kwa muda mrefu na hili ni tatizo ambalo hutokea mwaka baada ya mwaka. Kuna sababu kadhaa ambazo zimelifanya tatizo hili likithiri. Wananchi wengi hutegema ukulima kujipatia pato pamoja na chakula. Jambo hili limekuwa shida kubwa kwa vile kilimo hutegemea mvua isiyotabirika. Watabiri wa hali ya hewa huwashauri wakulima wapande mbegu zitakazohimili jua lakini mvua nayo inakuwa nyingi na kuharibu mimea.

    Bidhaa za ukulima kama mbegu za kupanda, mbolea, dawa za kunyunyizia na zinginezo, zimekuwa ghali. Kuna sehemu kubwa ya ardhi ambayo ni kame na haiwezi kutumika kwa kilimo. Mazao yanayotolewa shambani hayahifadhiwi vizuri. Mengine yanaharibikia shambani na mengine yanavamiwa na wadudu kiasi kwamba hayawezi kutumika.

    Tatizo lingine ni vita vya kikabila. Kabila tofauti zinapopigana, watu huhama na kuacha mashamba ilhali wengine huchoma maghala ya chakula. Wafanyabiashara pamoja na serikali huwanunulia wakulima mazao yao kwa bei ya chini sana mpaka wanakosa shauku ya kuyashughulikia mashamba yao.  Siku hizi wakulima hawashughuliki tena kuzuia mmomonyoko wa udongo. Hivyo mvua inaponyesha rotuba yote inachukuliwa. Serikali haina sera mwafaka za kukabiliana na njaa. Hii ndiyo sababu sehemu zingine kama Turkana na Marsabit zimekabiliwa na njaa kwa muda mrefu.

    Tatizo hili linaweza kutatuliwa ikiwa wakulima wataelimishwa juu ya mbinu bora za ukulima. Pia wakulima waishio katika sehemu ambazo hazina mvua ya kutosha wapewe mbegu ambazo zitahimili kiangazi. Ukulima wa kunyunyuzia mimea maji unafaa kuzingatiwa. Mazao yanayotolewa shambani yahifadhiwe vizuri kwa kuwekwa dawa za kuwaua wadudu.

    Sehemu kubwa za ardhi ambazo hazitumiwi zitolewe kwa kilimo. Ni muhimu wakulima waelimishwe kuhusu jinsi ya kuzuia mmomonyoko wa udongo na umuhimu wake. Wakulima wanunuliwe mazao yao kwa bei nafuu ili wajibidiishe katika kazi yao. Serikali inafaa iwe na sera mwafaka ili iweze kutatua tatizo hilo ambalo limekuwa ni janga kuu.
    MASWALI  
    1. Eleza mbinu tano zinazoweza kutumiwa kutatua tatizo kuu linalozungumziwa. (al 5)
    2. Fafanua matatizo mbalimbali yanayolikumba Taifa la Kenya. ( al 4)
    3. Onyesha ukulima ulivyo uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa la Kenya (al 2)
    4. Vita vya kikabila husababisha njaa. Dhibitisha kwa mujibu wa kifungu. ( al 2)
    5. Eleza maana ya maneno haya kama yaliyotumika katika kifungu. (al 2)
      1. Kukabiliana
      2. Janga
  2. UFUPISHO (ALAMA 15)
    Sawia na inavyotumika katika kukuza uchumi, teknolojia haiwezi kuepukika katika malezi enzi hizi na zijazo. Watalaamu wa malezi dijitali wanasema ingawa wazazi wanafaa kuhakikisha watoto wao wanakingwa na hatari za mtandao, unaweza kutumiwa kukuza talanta zao.

    Kulingana na mtaalamu wa malezi, wazazi wanaweza kutumia mitandao ya kijamii kukuza vipawa vya watoto wao huku wakihakikisha usalama wao. Watoto wanaweza kutumia mitandao kuandika blogu au kujifunza kupiga, kutangaza na kuuza picha na video. Wanaweza kunoa vipawa vyao katika michezo pia. Hivyo basi, wazazi wanapaswa kuwahimiza waingie katika mtandao na kuwa wabunifu.

    Wataalamu wanasema wazazi wanaowaruhusu watoto wao kuanza kutalii mtandao kwa lengo la kukuza talanta zao huwa wanawapa ufunguo wa ufanisi wa maishani. Mtaalamu mmoja kwa jina Aluoch alieleza kuwa, kukumbatia mtandao ni njia moja ya mtoto wako kuweka rekodi ya ufanisi wake. Iwe ni picha wakipokea zawadi, wakishiriki na kushinda mechi au wakiwa kwenye hafla muhimu kwa maisha yao. Jambo hili linaweza kuwatia moyo kukuza talanta zinazoweza kuwafaa katika maisha yao ya baadaye.

    Hata hivyo, wazazi wanafaa kuchunguza na kupitisha chochote watoto wao wanapakia au kuchapisha kwenye mtandao ili wasihatarishe maisha yao na ya familia zao. Ni muhimu kuwa makini ili watoto wasiandike maelezo au kuchapisha chochote kinachoeleza wanakoishi, wanakosemea au wanakoshinda wakicheza. Vitu vinazoweza kuepukwa ni kama sare za shule, picha zinazoonyesha nyumba yako au anwani ya nyumba au chapisho lolote linalotangaza watakakokuwa na wakati watakuwa hapo.
    Maswali 
    1. Fupisha aya tatu za kwanza.  ( maneno 80-85). (alama 9, moja ya mtiririko)
      Matayarisho 
      Jibu
    2. Fupisha aya ya nne.  (maneno 35-40) (alama 4, moja ya mtiririko)
      Matayarisho
      Jibu
  3. MATUMIZI YA LUGHA (ALAMA 40)
    1. Andika sauti zanye sifa zifuatazo: (al 2)
      1. Kipasuo, si ghuna cha ufizi
      2. Kikwamizo, ghuna cha ufizi
      3. Nazali,  ghuna ya kaakaagumu
      4. Irabu ya mbele, juu,  tandazwa
    2. Tunga neno lenye sauti mwambatano ya ufizi. (al 1)
    3. Kwa kutoa mifano, eleza tofauti ya silabi wazi na funge. (al 2)
    4. Andika sentensi ifuatayo katika umoja. (al 2)
      Tukipanda ndizi hizi vyema, vijiji hivi vitakuwa na vyakula vya kutosha.
    5. Tunga sentensi yenye muundo ufuatao (al 2)
      KN(W+V) + KT (t+ s)
    6. Ainisha viambishi awali na tamati katika neno  lifuatalo. ( al 2)
      Ulijuaje
    7. Onyesha na kutoa mifano, miundo miwili ya nomino katika ngeli ya KI-VI. ( al 2)
    8. Yakinisha sentensi hii katika nafasi ya pili. ( al 1)
      Wasiposoma kwa bidii hawatapita mtihani.
    9. Akifisha sentensi ifuatayo. (al 3)
      tafadhali nipe maji ninywe nina kiu mkimbizi alimwambia
    10. Andika sentensi ifuatayo katika hali ya udogo umoja. ( al 1)
      Ngoma hizo zao zilipasuliwa na vijana wale.
    11. Tunga sentensi moja ukitumia vitenzi vifuatavyo katika kauli ya kutendua. ( al 2)
      1. Funga
      2. Chomeka
    12. Unda vivumishi kutokana na vitenzi vifuatavyo kisha utunge sentensi ukitumia vivumishi ulivyotunga. ( al 2)
      1. Cheka
        Kivumishi…………………………………………………………………………………
        Sentensi……………………………………………………………………………………
      2. Pika
        Kivumishi………………………………………………………………………………….
        Sentensi…………………………………………………………………………………….
    13. Tumia neno hadi katika sentensi kama kihusishi cha: (al 2)
      1.   wakati
      2. mahali
    14. Tambua aina za vielezi katika sentensi ifuatayo: (al 2)
      Kipusa mrembo sana alitembea kitausi shuleni jana.
    15. Huba ni kwa penzi, heshima ni kwa …………………na ruhusa ni kwa ….………. (al 1)
    16. Tambua aina za vitenzi katika sentensi ifuatayo. (al 2)
      Kijana aliyekuwa hapa ndiye mtoto wake.
    17. Tambua shamirisho na chagizo katika sentensi ifuatayo. (al 3)
      Vijana hawa hulipiwa karo mapema.
    18. Changanua sentensi ifuatayo kwa kielelezo cha jedwali. (al 2)
      Zawadi nzuri niliyomtunuku mwanawe ilimpa furaha tele.
    19. Tunga sentensi mbili ukitumia neno “komaa” kama: (al 2)
      1. Kivumishi
      2. Nomino
    20. Ainisha virai katika sentensi ifuatayo; (al 3)
      Ndovu amelala kando ya mti.
    21. Tunga sentensi moja kudhihirisha maana tofauti za maneno; Fuma (al 1)
  4. ISIMU JAMII (ALAMA 10)
    1. Soma makala yafuatayo kisha ujibu maswali.
      Ahabu: Likizo ilikuwa fupi tumerudi kwa vitabu sasa.
      Munini: Huu ni wakati wa kipindi cha lala salama, lazima tujikaze.
      Ahabu: Usemavyo ni real.
      Munini: Bidii ndiyo itakayotuokoa.
      Ahabu: Ulimaliza ile assignment. Maze mimi nilishindwa.
      Munini: Shsss… ndo huyo mwalimu.
      Bw. Juma: Nani hao wanaongea?  Nyamazeni! Tumekuja hapa kusoma sio kupiga kelele.

      Maswali
      1. Tambua sajili inayorejelewa katika kifungu hiki. (alama 1)
      2. Fafanua sifa nne za sajili hii kama zilivyojitokeza katika kifungu ( alama 4)
    2. Taja nadharia tatu zinazoeleza chimbuko la lugha ya Kiswahili. ( alama 3)
    3. Eleza istilahi zifuatazo katika isimu jamii (alama 2)
      1. Usanifishaji
      2. Lafudhi


MARKING SCHEME

  1.  
    1. Eleza mbinu tano zinazoweza kutumiwa kutatua tatizo kuu linalozungumziwa. (al 5)
      1. Kuwaelimisha wakulima kuhusu mbinu bora za ukulima
      2. Kuwapa wakulima mbegu zitakazohimili kiangazi
      3. Kuzingatia ukulima wa kunyunyuzia maji
      4. Uhifadhi mzuri wa mazao
      5. Ardhi itolewe kwa kilimo
      6. Wakulima waelimishwe kuhusu umuhimu wa kuzuia mmomonyoko wa udongo
      7. Mazao yanunuliwe kwa  bei nafuu
      8. Sera iwe na sera mwafaka za kukabiliana na tatizo hili la njaa                  (1x5) Hoja za kwanza tano
    2. Fafanua matatizo mbalimbali yanayolikumba Taifa la Kenya. ( al 4)
      1. Tatizo la njaa kwa sababu ya kutegema mvua isiyotabirika
      2. Tatizo la bidhaa za ukulima kuwa ghali
      3. Tatizo la vita vya kikabila
      4. Tatizo la bei duni ya mazao         (1x4) hoja zozote nne
    3. Onyesha ukulima ulivyo uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa la Kenya (al 2)
      • Ukulima hutegemewa na wananchi wengi kujipatia pato pamoja na chakula.  (2x1)
    4. Vita vya kikabila husababisha njaa. Thibitisha kwa mujibu wa kifungu. ( al 2)
      • Vita vinapotokea watu huhama na kuacha mashamba.
      • Kuchomwa na maghala ya chakula.       (1x2)
    5. Eleza maana ya maneno haya kama yaliyotumika katika kifungu. (al 2)
      1. Kukabiliana – Jitihada ya kutatua tatizo fulani
      2. Janga  -  maafa/taabu/balaa
  2. UFUPISHO (ALAMA 15)
    1. Fupisha aya tatu za kwanza.  ( maneno 80-85). (alama 9, moja ya mtiririko)
      1. Teknolojia haiwezi kuepukika katika malezi ya watoto
      2. Mtandao unaweza kukuza talanta za watoto
      3. Watoto wanafaa kukingwa na hatari za mtandao
      4. Wazazi wanaweza kutumia mitandao kukuza vipawa vya watoto
      5. Lazima wazazi wahakikishe usalama wa watoto wao
      6. Watoto waweza kuandika blogu, kujifunza kupiga, kutangaza na kuuza picha na video
      7. Watoto waweza kunoa vipawa katika michezo na kuhimiza ubunifu
      8. Wazazi wanaoruhusu watoto kutumia mtandao kuwapa ufunguo wa ufanisi maishani
      9. Mtandao husaidia mtoto kuweka rekodi ya ufanisi wake
      10. Rekodi hizi huwatia moyo kukuza talanta zinazoweza kuwafaa katika maisha ya baadaye.
    2. Fupisha aya ya nne.  (maneno 35-40) (alama 4, moja ya mtiririko)
      1. Wazazi wachunguze na kupitisha chochote watoto wanapakia au kuchapisha.
      2. Wafanye hivi ili wasihatarishe maisha yao na familia zao
      3. Wazazi wawe makini ili watoto wasiandike maelezo yanayoeleza wanakoishi
      4. Waepuke kutangaza vitu kama sare za shule, anwani au picha zao.
  3. MATUMIZI YA LUGHA (ALAMA 40)
    1. Andika sauti zanye sifa zifuatazo: (al 2)
      1. Kipasuo, si ghuna cha ufizi  /t/
      2. Kikwamizo, ghuna cha ufizi /dh/
      3. Nazali,  ghuna ya kaakaagumu /ny/
      4. Irabu ya mbele, juu,  tandazwa /i/
    2. Tunga neno lenye sauti mwambatano ya ufizi. ndwele (al 1)
    3. Kwa kutoa mifano, eleza tofauti ya silabi wazi na funge. (al 2)
      • Silabi wazi- silabi wazi huishia kwa irabu. Kwa mfano, ba-ba
      • Silabi funge- silabi funge huishia kwa konsonanti. Kwa mfano. Dak-ta-ri
    4. Andika sentensi ifuatayo katika umoja. (al 2)
      Tukipanda ndizi hizi vyema, vijiji hivi vitakuwa na vyakula vya kutosha.
      • Nikipanda ndizi hili vyema, kijiji hiki kitakuwa na chakula cha kutosha
    5. Tunga sentensi yenye muundo ufuatao (al 2)
      KN(W+V) + KT (t+ s)
      • Yule hodari ndiye aliyenifunza.
    6. Ainisha viambishi awali na gtamati katika neno  lifuatalo. ( al 2)
      Ulijuaje
      U-li-ju-a-je
      SwaF42023MT1Q3f
    7. Onyesha na kutoa mifano, miundo miwili ya nomino katika ngeli ya KI-VI. ( al 2)
      • ki-vi    kwa mfano; kiti-viti
      • ch-vy kwa mfano; chakula - vyakula
    8. Yakinisha sentensi hii katika nafasi ya pili. ( al 2)
      Wasiposoma kwa bidii hawatapita mtihani.
      • Ukisoma kwa bidii utapita mtihani
    9. Akifisha sentensi ifuatayo. (al 2)
      tafadhali nipe maji ninywe nina kiu mkimbizi alimwambia
      • “Tafadhali nipe maji ninywe. Nina kiu.” Mkimbizi alimwambia.
    10. Andika sentensi ifuatayo katika hali ya udogo umoja. ( al 1)
      Ngoma hizo zao zilipasuliwa na vijana wale.
      • Kigoma hicho chake kilipasuliwa na kijijana kile.
    11. Tunga sentensi moja ukitumia vitenzi vifuatavyo katika kauli ya kutendua. ( al 2)
      1. Funga
      2. Chomeka
        • Jibu: Mama alifungua mlango na kuchomoa ufunguo.
          (kadiria sentensi ya mwanafunzi)
    12. Unda vivumishi kutokana na vitenzi vifuatavyo kisha utunge sentensi ukitumia vivumishi ulivyotunga. ( al 2)
      1. Cheka
        Kivumishi mcheshi
        Sentensi Mtoto mcheshi hupendwa na wengi.
      2. Pika
        Kivumishi mpishi
        Sentensi Mama mpishi amepika chakula kitamu.
    13. Tumia neno hadi katika sentensi kama kihusishi cha: (al 2)
      1. wakati
      2. mahali
        • Wanafunzi walifunga safari ya  Nairobi hadi Mombasa kutoka asubuhi hadi jioni.
    14. Tambua aina za vielezi katika sentensi ifuatayo: (al 2)
      Kipusa mrembo sana alitembea kitausi shuleni jana.
      • Sana - kielezi cha namna halisi
      • Kitausi – kielezi cha namna mfanano
      • Shuleni – kielezi cha mahali
      • Jana – kielezi cha wakati
    15. Huba ni kwa penzi, heshima ni kwa  adabu na ruhusu ni kwa udhuru (al 1)
    16. Tambua aina za vitenzi katika sentensi ifuatayo. (al 2)
      Kijana aliyekuwa hapa ndiye mtoto wake.
      • Aliyekuwa – kitenzi kishirikishi kikamilifu
      • Ndiye – kitenzi kishirikishi kipungufu
    17. Tambua shamirisho na chagizo katika sentensi ifuatayo. (al 3)
      Vijana hawa hulipiwa karo mapema.
      • Shamirisho kipozi – karo
      • Shamirisho kitondo – vijana hawa
      • Chagizo - mapema
    18. Changanua sentensi ifuatayo kwa kielelezo cha jedwali. (al 2)
      Zawadi nzuri niliyomtunuku mwanawe ilimpa furaha tele.
                                                                                                      S (changamano) 
                                               KN                                      KT
        N                  V                                 S  T                                    N                         V
       Zawadi        nzuri         niliyomtunuku   mwanawe  Ilimpa                          furaha                   tele 
    19. Tunga sentensi mbili ukitumia neno “komaa” kama: (al 2)
      1. Kivumishi - mkomavu
        • Mtu mkomavu hutoa maarifa
      2. Nomino – ukomavu
        • Ukomavu wake uliwasaidia watu sana
    20. Ainisha virai katika sentensi ifuatayo; (al 3)
      Ndovu amelala kando ya mti.
      • Ndovu - kirai nomino
      • Amelala - kirai tenzi
      • Kando ya mti - kirai husishi
    21. Tunga sentensi moja kudhihirisha maana tofauti za maneno; Fuma (al 1)
      • fuma- unda kitambaa kwa kupitisha nyuzi ndefu juu na chini kwa kutumia sindano
      • fuma- piga kwa kumrushia mtu mkuki au mshale
      • fuma – ona mtu ghafla akifanya jambo fulani
        sentensi; Alimfuma mnyama yule kwa mshale alipofumania akila mimea shambani.
  4.  ISIMU JAMII (ALAMA 10)
    1.  
      1. Tambua sajili inayorejelewa katika kifungu hiki. (alama 1)
        • Sajili ya shuleni/ darasani
      2. Fafanua sifa nne za sajili hii kama zilivyojitokeza katika kifungu ( alama 4)
        • Msamiati maalum mfano, mwalimu, kitabu
        • Lugha rasmi
        • Lugha ya utani na ucheshi baina ya wanafunzi
        • Lugha sanifu
        • Kubadili msimbo
        • Lugha ya kudadisi (mwanafunzi atoe mifano kutoka kwa kifungu)
    2. Taja nadharia tatu zinazoeleza chimbuko la lugha ya Kiswahili. ( alama 3)
      1. Kiswahili ni lugha ya mseto
        • Kwamba Kiswahili ni mchanganyiko wa lugha za waarabu, wahindi, waajemi na wenyeji wa pwani.
      2. Kiswahili ni kiarabu
        • Kwamba msamiati wa kiarabu ndio unapatikana katika lugha ya Kiswahili, hivyo basi Kiswahili ni kiarabu.
      3. Kiswahili ni mojawapo wa lugha za kibantu
        • Kwamba kuna ushahidi wa kiisimu na kihistoria. Msamiati kubwa unaopatikana katika lugha ya Kiswahili una asili ya kibantu.
    3. Eleza istilahi zifuatazo katika isimu jamii (alama 2)
      1. Usanifishaji
        • Ni uamuzi wa kuchagua lugha moja au mojawapo wa lahaja za lugha ili kuifanayia marekebisho ya kimatamshi, kisarufi, kimaana na kimaandishi ili itumike katika shughuli rasmi.
      2. Lafudhi
        • Ni ule upekee wa mzungumzaji katika lugha.
Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Questions and Answers - Form 4 Mid Term 1 Exams 2023.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?

Join our community on:

  • easyelimu app
  • Telegram
  • facebook page
  • twitter page
  • Pinterest