Wednesday, 05 July 2023 13:31

Kiswahili Questions and Answers - Grade 6 End Term Exams Term 2 2023 Set 1

Share via Whatsapp

Swali la 1 hadi la 5

Soma mazungumzo haya kisha ujibu maswali:

GRADE6KISWAHILISET1ET22023Q1

Kaka Mbweha: (Akicheka kwa kejeli) Bi. Ngiri, mkulima hodari wa mihogo anayeheshimika katika kanda ki, hujambo?

Bi. Ngiri: (Akihema kwa uchovu, mzigo alio nao kichwani unaonekana kumlemea) Sijambo, lakini nina swali. Unacheka nini? Ama ndio njia yako ya kumfariji anayetaka kuchanika kwenye mpini siku nzima?

Kaka Mbweha: (Anacheka zaidi) Ati kuchanika kwenye mpini? Wachapa kazi kama mimi hawana haja ya kujichosha. Wanafanya kazi kwa kutumia akili.

Bi. Ngiri: (Kwa dharau) Mhhh! Heri nyinyi mabingwa wa kutumia akili. Sisi wengine inabidi tujikaze kisabuni ili tupate riziki.

Kaka Mbweha: (Akionyesha kushangaa) Nyinyi wengine! Wewe na kina nani? Je, huna habari kwamba rafikiyo Sungura hapandi wala kuvuna lakini daima ana shibe?

Bi. Ngiri: (Kwa sauti ya chini) Hayo ya Sungura hayanihusu ndewe wala sikio. Isitoshe, unavyoona nimechoka. Shamba langu la mihogo liko umbali wa kilomita kumi na tano kutoka kwangu. Bado nina mlima mmoja wa kukwea ndipo nifike. Kaka Mbweha: Haya basi niazime vipande viwili vya mihogo. Nitarejesha nitakapovuna.

Bi. Ngiri: Kaka Mbweha, umesahau kuwa tayari una deni langu la mihogo? Lipa hilo kwanza.

Kaka Mbweha: (Kwa unyenyekevu) Nitalipa tu.

Bi. Ngiri: Utanilipa mihogo ilhali hukuvuna? Unastahili kufanya kazi kwa bidii. Kumbuka ajizi ni nyumba ya njaa.

  1. Bi. Ngiri anasifika kwa sababu gani?
    A. Bidii
    B. Ukulima
    D. Urafiki
  2. Wachapa kazi kama mimi hawana haja ya kujichosha.' Kauli hii inaonyesha tabia gani ya Kaka Mbweha?
    1. Yeye ni mvivu
    2. Ana jitihada kazini
    3. Ana akili
    4. Ana ukarimu
  3. Maneno, 'Tujikaze kisabuni yametumika katika mazungumzo. Ni tamathali gani ya lugha?
    1. Kitendawili
    2. Methali
    3. Nahu
    4. Tashbihi
  4. Wahusika katika mazungumzo haya ni _____
    1. watu
    2. Mifugo
    3. wanyamapori
    4. ndege
  5. Kisawe cha neno kukwea kwa mujibu wa kifungu hiki ni nini?
    1. Kupanda
    2. Kushuka
    3. Kuteremka
    4. Kupumzika

Swali la 6 hadi la 9

Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali.
                                                                   GRADE6KISWAHILISET1ET22023Q6

Siku moja mimi na sahibu yangu Dan tulikuwa tukipalilia mimea kwenye mradi wetu shuleni, Tulipiga gumzo huku tukiipinda migongo yetu. Ghafla bin vuu, sahibu yangu Dan alipasua ukemi. Alikuwa amejidunga kwenye mguu wake wa kulia! Bila kupoteza muda, nilikimbia hadi kwenye ofisi ya mwalimu wa zamu na kumuarifu kilichokuwa kimetokea. Bi Okero, aliyekuwa mwalimu wa zamu alichukua hatua mara moja. Aliwaita maskauti wapatao watatu tukaandamana nao.

Tulipofika alipokuwa ameketi Dan, Bi Okero aliwaelekeza maskauti jinsi ya kumpatia majeruhi huduma ya kwanza. Walichukua kitambaa safi na kufunga jeraha. Damu ilipokoma kutoka waliosha lile eneo kwa maji safi yaliyotiwa chumvi. Kisha walifunga kidonda bandeji na kumpeleka Dan kwenye zahanati iliyokuwa karibu. Tangu siku hiyo niliamua kujiunga na chama cha maskauti.

  1. Dan alikuwa akifanya nini alipoumia?
    1. Akifyeka
    2. Akinyunyizia mimea maji
    3. Akiondoa magugu shambani kwa jembe
    4. Akikata matawi ya mimea
  2. Je, ni nini kisichoonyesha kwamba Bi Okero anawajibika?
    1. Alikuwa katika zamu.
    2. Alichukua hatua mara moja.
    3. Aliwaelekeza maskauti kumpa majeruhi huduma ya kwanza.
    4. Alijiunga na chama cha maskauti.
  3. Kisawe cha zahanati ni nini?
    1. Hospitali
    2. Kliniki
    3. Dispensari
    4. Wadi
  4. Bi Okero aliwaelekeza maskauti jinsi ya kumpatia majeruhi huduma ya kwanza.' Je, majeruhi ni nani?
    1. Mgonjwa mahututi
    2. Mtu aliyejeruhiwa
    3. Mtu aliyepata nafuu
    4. Kiongozi wa maskauti

Swali la 10 hadi la 12

Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali.
                                           GRADE6KISWAHILISET1ET22023Q10

Baraka alikuwa kiongozi wa kijiji cha Mwanga. Kiongozi huyu alijulikana kwa ushauri wake kwa wanakijiji. Ushauri huu ulilenga zaidi njia bora za kuwekeza. Aliwapenda wanakijiji wake nao wakampenda kwa sababu ya uongozi wake mzuri.

Baraka na wanakijiji walifanya mikutano mara kwa mara. Katika mikutano hii walijadili njia mbalimbali za kuendeleza miradi katika kijiji chao.Umuhimu wa elimu ulisisitizwa. Kwa hivyo, wazazi na walezi waliwapeleka watoto wao shuleni bila kulazimishwa. Walitambua kuwa elimu inaleta heri maishani.

Wakulima walipewa mafunzo kuhusu kilimo bora. Walifundishwa kuhusu kilimo biashara. Walifundishwa kuhusu umuhimu wa kupanda mbegu zinazofaa kwa kila msimu. Waliwekeza katika kilimo wakapata mavuno tele. Wanakijiji walipata chakula cha kutosha. Mavuno ya ziada yaliuzwa. Wanakijiji hawa walipata faida kubwa. Kutokana na pesa walizopata waliendeleza kilimo. Isitoshe, walianzisha miradi ya ufugaji kuku, nyuki na
sungura.

Wafanyabiashara nao walipata maarifa ya kuboresha biashara zao. Walianzisha vikundi vya kuweka akiba na kukopeshana pesa. Biashara zao zikaimarika.

Sifa za kijiji cha Mwanga zilienea kote. Wageni kutoka vijiji jirani walikuja kujifunza jinsi ya kujiendeleza. Baraka na wanakijiji waliwapokea na kuwapa maarifa ya kuwekeza.

  1. Baraka alijulikana sana kwa sababu gani?
    1. Uwekezaji
    2. Upendo
    3. Mawaidha
    4. Uongozi
  2. Kwa nini wazazi waliwapeleka watoto wao shuleni?
    1. Umuhimu wa elimu ulisisitizwa katika mikutano
    2. Walilazimishwa na Baraka
    3. Walianzisha miradi
    4. Watoto walijipeleka
  3. Wafanyabiashara walianzisha vikundi vya kuweka akiba na kukopeshana pesa.' Neno akiba lina maana gani?
    1. Pesa za ziada anazopata mtu baada ya kuuza kitu.
    2. Pesa anazochukua mtu kutoka kwa mwingine ili alipe baadaye.
    3. Pesa anazopata mtu baada ya kufanya biashara.
    4. Pesa zinazowekwa kwa sababu ya matumizi ya baadaye.

Swali la 13 hadi la 15

Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali.

                                                  GRADE6KISWAHILISET1ET22023Q13

Ng'ombe ni mnyama ambaye anafugwa na binadamu. Mnyama huyu ana manufaa tele kwetu. Kwanza kabisa, huchinjwa ili tupate nyama. Ngozi yake hutumiwa kutengeneza bidhaa kama vile viatu na kanda zinazofungwa viunoni.

Ng'ombe jike hutupatia maziwa. Tunayatumia maziwa kupikia chai na pia kuyanywa. Jibini, ambacho ni chakula kitamu kwetu, hutengenezwa kutokana na maziwa yayo hayo. Mbali na nyama, ngozi na maziwa, Ng'ombe pia huuzwa. Fedha zinazotokana na mauzo hayo huweza kutumika kutimiza mahitaji mbalimbali. Fahali nao huenda wakatumika kulima mashambani. Isitoshe, tunaipata samadi kutoka kwa Ng'ombe. Samadi huweza kutumiwa kama mbolea.

  1. Ni manufaa mangapi ya ng'ombe yaliyotajwa katika kifungu hiki?
    1. Saba
    2. Sita
    3. Kumi
    4. Matano
  2. Kulingana na kifungu hiki ni ng'ombe yupi hutumiwa kulima?
    1. Wa kike
    2. Wa kiume
    3. Ndama
    4. Wa kike na wa kiume
  3. Kati ya vitu hivi ni gani hatupati kutoka kwa ng'ombe wa kiume?
    1. Samadi
    2. Nyama
    3. Ngozi
    4. Maziwa

Swali la 16 hadi la 20

Soma kifungu kifuatacho. Kina nafasi 16 mpaka 20. Kwa kila nafasi umepewa majibu manne. Chagua jibu lifaalo zaidi kati ya yale uliyopewa.

Timu ya Bingwa ilishinda mechi ya fainali. Ushindi ___16__ ulitokana na ushirikiano au __17___  waokatika mazoezi. Wachezaji wote walikuwa wenye bidii ___18__ mchwa. Baada ya mechi, wachezaji waliondoka uwanjani wakishangiliwa  na ___19___ Timu pinzani ___20__ wao katika kwamba imepoteza mechi hiyo.

   A
 16  yao  wao   kwao  mwao 
 17  utaratibu  utengano  umoja   uzalendo 
 18  kama kama vile   kwa sababu   kuliko
 19  refa  golikipa   walinzi   mashabiki 
 20  haijaamini haitaamini   haiamini   haikuamini 

 

Swali la 21 hadi la 30

Chagua jibu sahihi.

  1. Chagua sentensi ambayo ina maneno yenye silabi tatanishi.
    1. Uga ule umenyunyiziwa unga wa chokaa.
    2. Sisi tunapenda kwenda pwani likizoni.
    3. Jungu alilopikia nyama juzi limesafishwa.
    4. Wale wamechuma maua na kuyauza mbali.
  2. Zifuatazo ni jozi za maneno. Ni jozi gani iliyo na vimilikishi?
    1. Huyu, yule
    2. Changu, lake
    3. Tatu, tele
    4. Bora, hodari.
  3. Chagua neno ambalo linapatikana katika ngeli ya U - I:
    1. Mkebe
    2. Mtoto
    3. Unywele
    4. Meza
  4. Katika kamusi, maneno hupangwa kulingana na herufi za alfabeti. Kati ya Maneno haya ni gani litakuja mwanzo?
    1. Gonga
    2. Ganda
    3. Gamba
    4.  Godoro
  5. Kati ya sentensi hizi, ni gani haina kiwakilishi?
    1. Mimi huenda shuleni kila siku.
    2. Huyu anasoma kwa bidi.
    3. Watano watapewa zawadi.
    4. Viatu vitatu vimeoshwa.
  6. Andika sentensi ifuatayo katika wingi. Wavu wa mvuvi unastahili kuwa na shimo kubwa.
    1. Nyavu za mvuvi zinastahili kuwa na shimo kubwa.
    2. Wavu wa wavuvi unastahili kuwa na mashimo makubwa.
    3. Nyavu za wavuvi zinastahili kuwa na shimo kubwa.
    4. Nyavu za wavuvi zinastahili kuwa na mashimo makubwa.
  7. Kanusha sentensi ifuatayo: Maseremala watatutengenezea madawati.
    1. Maseremala hawatatutengenezea madawati.
    2. Maseremala hawajatutengenezea madawati.
    3. Maseremala hawakututengenezea madawati.
    4. Maseremala hawatutengenezei madawati.
  8. Andika sentensi ifuatayo katika hali ya ukubwa. Mlango ulipakwa rangi ukapendeza.
    1. Malango yalipakwa rangi yakapendeza.
    2. Kilango kilipakwa rangi kikapendeza.
    3. Lango lilipakwa rangi likapendeza.
    4. Milango ilipakwa rangi ikapendeza.
  9. Umesimuliwa hadithi na mlezi wako. Sasa ni wakati wa kulala. Chagua maagano utakayotumia kumuaga mlezi wako.
    1. Kwaheri
    2. Alamsiki
    3. Buriani
    4. Safiri salama
  10. Chagua methali isiyohusu malezi.
    1. Mtaka cha mvunguni sharti ainame
    2. Mtoto akibebwa hutazama kisogo cha nina.
    3. Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.
    4. Asiyefunzwa na mamaye hufunzwa na ulimwengu

INSHA

Andika insha kuhusu:

Barua rasmi kwa mwalimu anayesimamia chama cha mazingira ukimwomba nafasi ya kujiunga na chama hicho.

MARKING SCHEME

  1. B
  2. A
  3. C
  4. C
  5. A
  6. C
  7. D
  8. C
  9. B
  10. C
  11. A
  12. D
  13. B
  14. B
  15. D
  16. B
  17. C
  18. A
  19. D
  20. A
  21. A
  22. B
  23. A
  24. C
  25. D
  26. D
  27. A
  28. C
  29. B
  30. A

 

 

 

Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Questions and Answers - Grade 6 End Term Exams Term 2 2023 Set 1.


Tap Here to Download for 30/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students