Monday, 13 March 2023 12:08

Kiswahili Questions and Answers - Class 8 Mid Term Exams Term 1 2023 Set 3

Share via Whatsapp

Soma vifungu vifuatavyo. Vina nafasi 1 mpaka 15. Kwa kila nafasi umepewa majibu manne hapo. Jaza kila pengo kwa kuchagua jawabu lifaalo zaidi.

Nilisikia kuwa Zakayo alikuwa seremala aliyejulikana kijijini __1__. Samani __2__ mara kwa mara ziliwafaa na kuwapendeza wengi. Ungefika katika__3__ yake, usingekosa kupata __4__ waliofika ama kujionea __5__ kununua fanicha. Kila mmoja alifahamu kuwa ufanisi __6__ haukuja hivihivi tu. La hasha! Alikuwa mja mwenye kujituma na __7__. Daima alifahamu kuwa ___8___.

       A                   B              C               D 
 1.   pote   mote   chote   kote 
 2. zilizotengeneza    zilizotengenezwa    alizotengeneza   alizotengenezwa 
 3.  majilisi   makavazi   maabara   karakana 
 4.  watu anuwai   umati wa watu   mlolongo wa watu   safu ya watu 
 5.  au   wala  ila  bali
 6.  yake  huu  huo  hiyo
 7.  kulaza damu   kujitolea mhanga    kula mwande   kufa moyo 
 8.  mgaagaa na upwa hali wali mkavu   simba mwenda pole ndiye mia nyama   mkono mmoja hauchinji ng'ombe   mwana wa mhunzi asiposana huvukuta


Kila mtoto ana uwezo wa __9__ mambo mengi sana ikiwa atapewa nafasi inayofaa. Si vyema __10__ watoto kwa madai kuwa ni wa kike au wa kiume. Jinsia __11__ kutumika kama kigezo cha kuamua uwezo wa mtoto. Siku hizi, si __12__ kuwaona binadamu wa kike au kiume wakifanya kazi sawa. Hapo zamani, watu wangeshangaa kumpata mwanamke akifanya kazi ya __13__; yaani kufua vyuma. __14__ limekuwa jambo la kawaida kwani uwezo wao __15__ katika kazi za aina zote.

          A          B          C            D 
 9.   kutekeleza   kutendesha   kutelekeza   kutekelezwa 
 10.   kuwapendelea   kuwabagua   kuwatunukia   kuwashauri 
 11.  haufai   haifai   halfai   hamfai 
 12.  kawaida  muhimu   ajabu   rahisi 
 13.  ujume   unajimu   uhandisi   uhunzi 
 14.  Hiki   Huu   Hii   Hili 
 15.  unadhihirika  unadidimia  unadunishwa   unadhihirisha 

 

Kuanzia nambari 16 hadi 30 jibu kulingana na maagizo. 

  1. Tambua aina za maneno yaliyopigiwa mistari.
    Ambaye alikamilisha kazi asubuhi amefurahi.
    1. kivumishi, nomino
    2. kivumishi, kielezi
    3. kiwakilishi, kielezi
    4. kiwakilishi, nomino
  2. Sentensi gani iliyotumia nomino ambata?
    1. furaha
    2. mbwakoko
    3. thureya ya nyota
    4. kitambaa
  3. Chagua maelezo ambayo ni sahihi.
    1. Mjume hufanya kazi ya kufua visu.
    2. Kinu na mchi hutumika kukunia nazi.
    3. Bomba la kutolea moshi jikoni huitwa dohani.
    4. Nyonga hupatikana kati ya goti na paja. 
  4. Koloni hutumika kwa njia gani?
    1. Kuunganisha sentensi mbili zinazokaribiana kimaana.
    2. Kuonyesha kuwa maneno yaliyokuwa yakisemwa hayakukamilika.
    3. Kuonyesha mwisho wa sentensi kamilifu.
    4. Kutanguliza orodha katika sentensi. 
  5. Sentensi gani ambayo ni sahihi kati ya sentensi zifuatazo?
    1. Maji chafu hayafai kunywewa.
    2. Taifa lenye linaendelea vizuri ni hili. 
    3. Mimea yote yalimea vizuri.
    4. Madaktari wamewatibu wagonjwa hao.
  6. Ugonjwa gani ambao hutokana na baridi kati ya magonjwa yafuatayo?
    1. saratani
    2. waba
    3. unyafuzi
    4. kichomi
  7. Chagua sentensi iliyo na kitenzi katika hali ya kufanyiza
    1. Aliyauza matunda yake katika soko la Kongowea.
    2. Tendo la kuwaoza wasichana wachanga limepigwa marufuku.
    3. Matunda yaliyooza yarnetupwa mbali.
    4. .Aliuliza swali hilo kwa wanafunzi wawil 
  8. Tambua matumizi ya 'kwa' kwenye sentensi ifuatayo.
    Alipofika kwa mjomba wake alipokelewa kwa furaha.
      1. kifaa, namna
    1. namna, ala
    2. kihusishi, matumizi
    3. kihusishi, jinsi
  9. Sentensi gani iliyotumia kivumishi kiashiria?
    1. Kalamu nzuri iliwekwa ndani ya mkoba.
    2. Nyumba yake imejengwa ikakamilika.
    3. Kijana mwenyewe atapewa kitabu hicho.
    4. Wanafunzi wengi wamepanda miti. 
  10. Onyesha sentensi iliyo katika hali timilifu.
    1. Ungefuata masharti ungekuwa mshindi.
    2. Hakuelewa kuwa usafi ni muhimu.
    3. Nguo hazijakauka kwa njia nzuri.
    4. Sitaki kujihusisha na matumizi ya dawa za kulevya.
  11. Tambua maamkuzi ambayo ni ya wakati ulio tofauti.
    1. umeshindaje 
    2. sabalheri 
    3. umeamkaje
    4. chewa
  12. Chagua ukanusho wa:
    Aliyewasili alipigiwa makofi. 
    1. Asiyewasili hakupigiwa makofi.
    2. Aliyewasili hajapigiwa makofi. 
    3. Aliyewasili hakupigiwa makofi. 
    4. Asiyewasili hajapigiwa makofi.
  13. Mwanzele alipokuwa akielekea nyumbani wakati wa jioni, kivuli chake kilikuwa nyuma yake. Je, nyumbani kwao ni upande gani wa dira?
    1. mashariki
    2. kaskazini
    3. kusini
    4. magharibi
  14. Tambua ukubwa wa;
    Mbuzi mwenye uso mdogo amelala chini ya mti.
    1. Buzi lenye juso dogo limelala chini ya jiti.
    2. Kibuzi chenye kijuso kidogo kimelala c hini ya kijiti.
    3. Kibuzi chenye kijuso kidogo kimelala chini cha kijiti.
    4. Buzi lenye juso dogo limelala chini la jiti.
  15. Mvulana ni kwa msichana kama vile jogoo ni kwa _______________________________.
    1. jimbi
    2. kikwara
    3. koo
    4. kipora

Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali yanayofuata.  

Ukiitathmini jamii yetu kwa makini, utagundua kuwa maovu yanazidi kuzagaa na kushamiri kote. Ni nadra sana kwa siku kumalizika bila kusikia habari za maovu kama vile ubakaji, mauaji, wizi, utapeli, vita na kadhalika. Wengi wamekuwa wakijisaili mara kwa mara ili kupata suluhu. Kuwategemea maafisa wa polisi nako kumekuwa kazi ya bure bilashi. Hii ni kwa kuwa polisi wenyewe nao wana matatizo yaliyowazidi nguvu. Kuna nyakati ambapo polisi huwafyatulia risasi na kuwaua raia wanaofaa kuwalinda. Ajabu iliyoje! Nyakati zingine, maafisa wa usalama huwaua jamaa zao na kujiua wao wenyewe. Hali ya polisi kuchukua hongo na kupuuza sheria imekuwa jambo la kawaida. Chambilecho marehemu babu yangu, Mola ailaze roho yake mahali pema peponi, baadhi ya maafisa wa usalama wamekuwa kama paka waliojukumishwa kuyatunza maziwa. Kazi yao ikawa kuyanywa bila kujali.

Je, maovu haya yanachangiwa na nini? Inadaiwa kuwa jambo la msingi ni kupanda kwa kiwango cha maisha. Wataalam wanasema kuwa kupata mahitaji ya kimsingi kama vile chakula, makazi na mavazi kumekuwa kama kumtafuta paka mweusi katika giza. Wengi wanapozidiwa na mzigo wa maisha, wanakata shauri kuiba, kuwatapeli wenzao au kuua ili wapate pesa za kuzikimu aila zao. Wengine nao huona kuwa kuwaua watoto na kujiua ni njia rahisi ya kujiondoa na kuwaondoa wapendwa wao katika ulimwengu huu wenye madhila na mizingile chungu nzima. Lile wanalofaa kujua ni kuwa njia hizo hazifai kabisa. Awali ya yote, ni jambo la busara kufahamu kuwa Mungu ndiye mwenye mamlaka juu ya uhai wa mja yeyote. Kujiua au kumwua mtu ni dhambi mbele ya mwenyezi Mungu. Maovu mengine kama vile wizi na utapeli humletea mtu majuto tele.

Sababu nyingine ni tamaa. Kuna wengi katika jamii ambao hawatosheki na kile wanachokipata. Kwa nini afisa wa polisi aliye na mshahara ajiingize katika shughuli za ufisadi? Kuna haja gani kwa gavana anayelipwa kitita cha pesa kupora mali ya umma? Daktari wa hospitali ya umma anaibaje dawa katika hospitali na kuziuza kama si kuongozwa na tamaa? Bila shaka, wanaongozwa na tamaa. Tamaa humfanya mtu asitosheke. Anapopata nne, hutamani kuwangepata nane. Pale anapojaliwa kupata sita, huona kuwa ingekuwa afadhali kama angepewa tisa. Japo ni vyema kupiga hatua maishani, ni vyema hatua hizo zipigwe katika mipaka ya kisheria na kanuni zilizowekwa.

Isitoshe, wapo wengi walio na mazoea ya kupuuza sheria. Naam, hawa ni wale wenye hulka za kuenda kinyume na maagizo. Wao hufurahia sana wanapokiuka kanuni zilizowekwa. Yamkini, watu wa sampuli hii hutaka kuona lile litakalotokea baada ya kuvunja sheria. Nimewahi kusikia visa vya watu waliowapa sumu na kuwaua mifugo wa mwingine bila sababu. Furaha yao ni kuona maovu yakitokea na hasara kumpata mtu. Wengine hutembea na rungu na mijeledi usiku wa manane ili kuwacharaza wapitanjia bila sababu maalum. Ajabu ni kwamba wao hawawezi wakatamani kufanyiwa maovu kama hayo.

Aidha, kuna wengi ambao hukosa utt. Kukosa utu humfanya mtu asimjali mwenzake wala kumwonea huruma. Kukosa utu husababisha mtu asijiulize, "Je, nikifanyiwa hivyo nitahisi vipi?" Mwizi anayemwibia mtu pesa, simu, mkoba, kumpokonya mavazi na kisha kumpiga huwa anaongozwa na nini? Huo si unyama? Mtu anawezaje kumkatakata mume au mkewe kwa kigezo kuwa yeye ni mkizi? Je, haelewi kuwa hasira hasara?

Ili kupata suluhisho la kudumu, serikali na jamii kwa jumla ina jukumu la kubuni nafasi nyingi za kazi. Hili litachangia katika kupunguza gharama ya maisha. Matumizi ya dawa za kulevya nayo yanafaa kupigwa marufuku. Walevi au waraibu wa mihadarati husababisha maovu mara kwa mara. Zaidi ya yote, ni jambo la busara kuiombea nchi yetu kucha kutwa ili Mola aiauni.

  1. Kwa mujibu wa aya ya kwanza, ni kweli kuwa;
    1. Msomaji amekuwa akifanya uchunguzi kuhusu kutokea kwa maovu.
    2. Siku hata moja haiwezi ikapita bila visa vya kutokea kwa maovu kutangazwa. 
    3. Maovu yamekuwa yakitokea mara kwa mara katika jamii.
    4. Ni vigumu kusikia kuwa kumetokea maovu mbalimbali katika jamii yetu.
  2. Neno 'wakijisaili' lina maana gani jinsi lilivyotumika katika kifungu?
    1. wakishangaa
    2. wakijiuliza
    3. wakijirekebisha
    4. wakijituliza
  3. Yafuatayo ni maovu yaliyotajwa katika aya ya kwanza isipokuwa;
    1. ufisadi
    2. ubakaji
    3. mauaji
    4. anas
  4. Aya ya pili inadokeza kuwa,
    1. Kupanda kwa gharama ya maisha ndio msingi wa kutokea kwa maovu.
    2. Kila anayezidiwa na mzigo wa maisha hujiingiza katika maovu kama vile wizi.
    3. Baadhi ya watu hutekeleza maovu wanaposhindwa kutatua matatizo yanayowakumba.
    4. Mungu pekee na serikali ndio wenye mamlaka juu ya uhai wa mja yeyote.
  5. Kauli 'polisi huwafyatulia risasi na kuwaua raia wanaofaa kuwalinda' inaonyesha;
    1. kinaya
    2. majazi
    3. kejeli
    4. tabaini
  6. Msimulizi wa makala haya anaeleza kuwa mara nyingi ufisadi hutokana na;
    1. kutotosheka.
    2. kutamauka.
    3. kukosa utu.
    4. kuzoea kuvunja sheria.
  7. Msimulizi ana maana gani anaposema kuwa 'kumekuwa kama kumtafuta paka mweusi katika giza'?
    1. ni nadra
    2. ni muhali
    3. ni shani
    4. ni sahili
  8. Kauli 'wao hawawezi wakatamani kufanyiwa maovu kama hayo' inaashiria ukweli wa methali gani?
    1. Baniani mbaya kiatu chake dawa.
    2. Mkuki kwa nguruwe kwa binadamu uchungu.
    3. Ndugu mui heri kuwa naye.
    4. Mui huwa mwema.
  9. Maneno 'yeye ni mkizi' yana maana gani jinsi yalivyotumika katika kifungu?
    1. ana hasira
    2. ni mkali
    3. ni katili
    4. ni mwenye tovu
  10. Kulingana na kifungu, ubunifu wa nafasi za kazi:
    1. ndiyo njia bora zaidi ya kukabiliana na maovu katika jamii.
    2. ni jukumu la serikali ya nchi husika. 
    3. ndiyo njia kuu ya kupunguza maovu katika jamii.
    4. unaweza kuchangia katika upunguzaji wa maovu.

Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali yanayofuata.   

Wakazi wa Ihonje walikusanyika katika kikao cha kumpa heshima za mwisho Bwana Kapombe. Japo awali alijulikana na kila mmoja kama Adili, hulka zake za kukumbatia ulevi zilifanya akabatizwa jina la Kapombe. Jina halisi alilopewa na wazazi wake likayeyuka kama barafu kikaangoni na kupotea kama moshi hewani. Boma lao lilijaa watu kutoka janibu za mbali na karibu. Wapo waliolia na kulalamikia namna kifo kilivyoipokonya jamii mtu wa maana. Wengine waligalagala mchangani na kutishia kujitupa katika kaburi lililochimbwa ikiwa hapakujitokeza yeyote wa kuwazuia. Ukweli ni kuwa kijana wa watu alikuwa ameacha mkono kulingana na maoni ya wanajamii hao.

Japo mwili wake haukuwa umepatikana, ilikuwa wazi kuwa asingekuwa hai kwa namna yoyote ile. Kiwango chake cha ulevi kilikithiri na kupita mipaka. Walifahamu kuwa kama hakugongwa na gari, basi alianguka mtoni na kufa au alikunywa pombe kupita kiasi. Kijana huyo alikuwa ametoweka siku kadhaa zilizotangulia. Ndugu, jamaa na marafiki walimsaka kwa siku tatu mtawalia. Hata hivyo, juhudi zao hazikuzaa matunda. Msako huo ulilenga sehemu mbili kuu, vituo vya polisi na vituo vya kuuzia pombe haramu. Ilikuwa desturi kwake kupatikana katika makao ya wagema tangu macheo hadi machweo, kucha kutwa. Alifanya kibarua na kulipwa hela kidogo, zote zilikuwa zawadi kwa mgema. Alipokosa kibarua, aliiba kuku, shati la mtu au sufuria la mama yake na kuuza. Wakati mwingine hakupatikana akiwa kwa mgema. Huo ulikuwa wakati ule aliotiwa mbaroni ama kwa kupatikana akibugia pombe haramu au kushukiwa kwa wizi wa vitu vya wanajamii.

Alipokosekana katika maeneo hayo mawili, iliamuliwa kwa kauli moja kuwa alikuwa amefariki. Kwa mujibu wa mila na desturi za jamii hiyo, walilazimika kuuzika mgomba na kufanya matanga yake. Siku hiyo ya mazishi', boma la akina Kapombe lilijaa: si wake, si waume, si vijana, si wazee, si matajiri, si wachochole. Vyakula ainati viliandaliwa: ugali, nyama, pure, chai ya maziwa, chai ya mkandaa, kitoweo cha kuku miongoni mwa vyakula vingine.

Harakati za mazishi zilipokuwa zimenoga, mtu mmoja karibu na lango la boma alipiga ukelele wa hofu. Wengine walipoangalia, walimwunga mkono kwa kupiga unyande, kamsa, nduru na mayowe. Ya Mungu ni mengi! Kapombe alionekana akijikokota kurudi nyumbani kwao. Alikuwa mnyonge, mngonge kama utumbo. Alikuwa mchafu mithili ya kilihafu. Alinuka fee ungedhani kuwa ni fondogoo. Wapo waliopiga mbio kwa kasi ya umeme. Masufuria ya vyakula yaligongwa na kukimwaga chakula. Wengine nao walibeba chakula kicho hicho, hasa kuku. Palikuwa na hali ya kuchanganyikiwa katika boma lote. Wachache waliokuwa na ujasiri walitulia tuli kama maji mtungini. Utulivu uliporejea, Kapombe alipewa nafasi ya kujieleza. Kumbe hakuwa ameaga dunia. Mtoto wa watu alilewa chakari bin chordo. Maadamu hakuwa amekula kwa muda, pombe ilimzidi nguvu na kusababisha kuzimia kwake. Alinyooka twaa kando ya barabara kama mzoga.

Alifafanua kuwa alizinduka na kujipata katika chumba kilichoogofya. Hali iliyokuwa mie ndani haikuelezeka kwa maneno yoyote. Alikata shauri kutoka nje. Alipoufungua mlango wa chumba, mabawabu waliokuwa pale nje walipiga mbio kwa hofu na woga wa kunguru. Kumbe alipopatikana akiwa amezimia njiani, alidhaniwa kwamba ameaga dunia, akapelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti. Msamaria mwema alimfanyia hisani na kumpeleka hospitalini alikolazwa kwa siku tatu akifanyiwa matibabu. Kapombe alikula yamini kuwa asingelewa tena. Asingemwamkua wala kumwangalia mgema. Asingewaza kuhusu pombe wala kileo chochote. Hewaa! Alikuwa amepata funzo la mwaka.

  1. Jina halisi ambalo kapombe alipewa na wazazi liliyeyushwa na nini?
    1. mazoea ya wakazi
    2. tabia zake za ulevi
    3. mabadiliko ya maisha
    4. dawa za kulevya
  2. Eleza maana ya 'janibu' jinsi lilivyotumika katika kifungu.
    1. matabaka
    2. sehemu
    3. viwango
    4. safari
  3. Kulingana na aya ya pili, ni kweli kuwa;
    1. wakazi walithibitisha kuwa Kapombe alikuwa amefariki.
    2. ilisemekana kuwa Kapombe alionekana katika kituo cha polisi na kituo cha kuuzia pombe haramu.
    3. ndugu, jamaa na marafiki walianza kumsaka baada ya siku tatu.
    4. Kapombe alitumia kila njia ili apate pesa za kununulia vileo.
  4. Ni kweli kuwa waliokuwa wakilia nyumbani kwa akina Kapombe walikuwa;
    1. wanafiki.
    2. waombolezaji.
    3. majirani.
    4. masahibu.
  5. Msimulizi anaposema kuwa juhudi zao hazikuzaa matunda', ana maana kuwa;
    1. ziligonga mwamba.
    2. zilifua dafu.
    3. zilishamiri.
    4. zilikuwa maarufu.
  6. Kapombe alifafanua jinsi;
    1. alivyozinduka.
    2. alivyolala.
    3. alivyozimia.
    4. alivyoshtua watu.
  7. Kwa maoni yako, kwa nini watu wengi walifika nyumbani kwa akina Kapombe wakati wa 'mazishi' yake?
    1. walitaka kumwona akirudi nyumbani.
    2. walijua kuwa hakuwa amekufa bali alikuwa tu hospitalini.
    3. walizingatia mila na desturi za jamii yao.
    4. walijua kuwa kungekuwa na chakula kingi cha kufurahia.
  8. Yawezekana kuwa Kapombe aliamua kuuacha ulevi kutokana na:
    1. kuogopa kushikwa na polisi mara kwa mara.
    2. kuchoshwa na hali ya kudharauliwa na wanakijiji kila wakati.
    3. ushauri aliopewa na madaktari alipokuwa hospitalini.
    4. dhiki nyingi alizopitia kutokana na ulevi wake.
  9. Wakazi walitarajia kuwa Kapombe angepatikana katika;
    1. kituo cha polisi, makao ya mgema 
    2. kituo cha polisi, hospitali
    3. chumba cha kuhifadhi maiti, makao ya mgema
    4. chumba cha kuhifadhi maiti, hospitali 
  10. Ujumbe katika kifungu hiki unaweza ukarejelewa kwa methali kuwa;
    1. Mgema akisifiwa tembo hulitia maji. 
    2. Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.
    3. Mtegemea cha nduguye hufa maskini. 
    4. Hakuna marefu yasiyokuwa na ncha.

INSHA   

Andika Insha ya kusisimua itakayoanzia kwa maneno yafuatayo

Niliposikia jina langu likiitwa, nilishangaa. Sikuyaamini masikio yangu. Moyoni nilijawa na ................................................



MARKING SCHEME

  1. D
  2. C
  3. D
  4. A
  5. A
  6. C
  7. B
  8. A
  9. A
  10. B
  11. B
  12. C
  13. D
  14. D
  15. A
  16. C
  17. B
  18. C
  19. D
  20. D
  21. D
  22. B
  23. D
  24. C
  25. C
  26. A
  27. C
  28. D
  29. D
  30. C
  31. C
  32. B
  33. A
  34. C
  35. A
  36. A
  37. B
  38. B
  39. A
  40. D
  41. B
  42. B
  43. D
  44. A
  45. A
  46. A
  47. C
  48. D
  49. A
  50. D
Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Questions and Answers - Class 8 Mid Term Exams Term 1 2023 Set 3.


Tap Here to Download for 30/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students