KCSE 2017 Kiswahili Paper 1 with Marking Scheme

Share via Whatsapp
  1. Lazima
    Shirika la kigeni la Tugawane limeanzisha kiwanda cha kutengenezea matofali katika eneobunge lenu. Mwandikie barua Mhariri wa Gazeti la Mzalendo ukitoa maoni yako kuhusu faida na changamoto zinazoweza kutokana na mradi huu.
  2. Andika insha kuhusu umuhimu wa mwanafunzi kujiunga na vyama mbalimbali shuleni.
  3. Tunga kisa kitakachodhihirisha maana ya methali ifuatayo:
    Papo kwa papo kamba hukata jiwe.
  4. Tunga kisa kitakachomalizika kwa maneno yafuatayo:
    Sikuupa moyo wangu nafasi ya kujutia niliyoyatenda. Nilikuwa nimeamua kuyajenga maisha yangu upya.


MARKING SCHEME

  1.  
    1. Hili ni swali ambalo linamhitaji mtahiniwa kuandika barua rasmi kwa mhariri.
    2. Kaida za uandishi wa barua rasmi zifuatwe.
    3. Vipengele viwili vya tungo za aina hii vishughulikiwe:
      1. Muundo na mtindo. 
        1. Sura ya barua kwa mhariri 
          1. Anwani mbili
            • ya mwandishi
            • ya Mhariri wa Gazeti la Mzalendo
          2. Tarehe- baada ya anwani ya mwandishi 
        2. Mwili 
          1. Utangulizi
            • Kongowezi/mtajo: Kwa Mhariri...
            • Kusudi-Kiini cha barua kijitokeze kwenye mada hii.
            • Aya ya kwanza iangazie kusudi la kuandika.
            • Hoja zijadiliwe kwa kupangwa kiaya. Kila hoja ijadiliwe na kukamilika kwenye aya mahsusi. 
          2. Hitimisho
            Mtahiniwa ahitimishe mawazo yake. Maoni yake kuhusu kiwanda hiki yajitokeze. 
          3. Kimalizio
            Sahihi, jina na cheo cha mwandishi kijitokeze.
        3. Mtindo
          Hii ni barua ya maoni wala si ya malalamishi. Hoja zijadiliwe kwa namna ambavyo msimamo wa mwandishi utajitokeza. Lahaja sanifu ya Kiswahili itumiwe. Urasmi udumishwe.

          Tanbihi
          Ikumbukwe kwamba barua hii bado haijachapishwa katika gazeti, hivyo sharti iwe na anwani zote mbili. Mhariri ndiye anayehariri baadaye na kutoa mojawapo. Mtahiniwa akiandika anwani moja atakuwa amepungukiwa kimuundo.
      2. Maudhui
        Mtahiniwa aonyeshe faida na hasara/matatizo yanayoweza kutokana na kiwanda hiki. Baadhi ya hoja ni:
        Faida
        1. Kusaidia katika ujenzi
        2. Kuboresha makazi 
        3. Kubuni nafasi za kazi 
        4. Riaia kindandaki kupata soko kwa bidhaa, kama vile chakula, zinazozalishwa humo 
        5. Kuchochea kuimarishwa kwa miundomsingi
        6. Husaidia ukuaji wa viwanda vingine vinavyosaidia shughuli za kiwanda hiki.
        7. Kukuza utangamano kati ya wageni na raia
        8. Kuwafunza//kuwarithisha raia stadi za ufyatuaji matofali kwa njia ya kisasa. 
        9. Kupunguza idadi ya vijana wanaohamia mijini kutafuta kazi
        10. Kudhibiti visa vya ukosefu wa usalama, kutokana na vijana/watu ambao hawana ajira. 
        11. Kuimarisha stadi ya utafiti- raia kutafuta njia endelevu za kuendeleza kiwanda hiki baada ya wageni kuondoka
        12. Kupalilia stahamala ya kijamii- raia na wageni kujifunza kutambua na kuheshimu tofauti zao za kitamaduni

          Hasara
          1. Huenda wageni wakaja na wafanyakazi wao, hivyo kutowafaidi wenyeji.
          2. Huenda kikaua viwanda vingine vya aina hii. 
          3. Kuzorota kwa maadili, hasa wafanyakazi wa kigeni wanapotagusana na wenyeji kwa njia isiyofaa. 
          4. Kupalilia ajira ya watoto, baadhi ya vijana kuvutiwa na pesa na kujiunga na shirika hili 
          5. Kukatishwa kwa masomo - vijana kuacha shule ili kufanya kazi 
          6. Ndoa za mapema- baadhi ya vijana huenda wakaacha masomo na kuolewa wakiwa wachanga.
          7. Kinaweza kupalilia ukosefu wa usalama- baadhi ya watu kutaka kuwaibia wenye kiwanda

            Tanbihi
            1. Mtahiniwa aangazie angaa changamoto mbili. 
            2. Hitimisho ionyeshe msimamo wa mwandishi. Pengine aonyeshe kwamba japo kuna hasara natija inazidi hasara hii. Anaweza kuipongeza serikali kwa kiwanda hiki. 
            3. Kaida nyingine zote za usahihishaji wa insha zizingatiwe kama ilivyo kwenye mwongozo  wa kudumu.
  2. Umuhimu wa vyama vya wanafunzi
    Huwezesha wanafunzi:
    1. Kupalilia vipawa vya uongozi - kwa mfano kupitia vyama vya riadha ambapo kuna mwanafunzi ambaye ni kinara.
    2. Kukabilina na changamoto - kwa mfano Chama cha Washauri Marika ambacho huelekeza wenzao kuhusu namna na kutatua matatizo. 
    3. Kupalilia maadili ya kidini- kwa mfano kupitia vyama vya kidini kama vile CU, YCS, CA 
    4. Kukuza utangamano- wanafunzi wanapokuja pamoja katika shughuli za chama 
    5. Huimarisha mbinu za kushawishi, kwa mfano kupitia Chama cha Mjadala. 
    6. Kujiimarisha kielimu - kupitia Chama cha Mjadala/Mdahalo ambapo wanafunzi hub adilishana maarifa. 
    7. Kutumia nishati kwa njia chanya-Badala ya kuingilia vitendo viovu wanaweza kujiunga na vyama kama vile vya kuhifadhi mazingira shuleni. 
    8. Kuimarisha ubunifu - kwa mfano kupitia Chama cha Waandishi/Uchapishaji. 
    9. Kuelekezwa kitaaluma - kwa mfano kupitia Chama cha Viongozi Chipukizi na Chama cha Wakulima ambavyo hushughulikia masuala ya kitaaluma. 
    10. Kujenga ukakamavu na kujiamini - Chama cha Drama
    11. Kujipumbuza - Chama cha Drama 
    12. Kujenga stahamala- hali ya kuwakubali wengine jinsi walivyo- kupitia mitagusano yao katika shughuli za chama.
    13. Humwezesha mwanafunzi kuratibu muda wake ipasavyo ili kukabiliana na majukumu ya vyama hivi pamoja na mahitaji ya masomo.
  3. Kisa kidhihirishe maana ifuatavo:
    Jambo, hata likawa gumu vipi, likifanywa kwa kurudiwarudiwa mwishowe hufaulu.
    Hata mtu akikabiliwa na hali gumu vipi, na atie bidii kuitatua hali hiyo; asikate tamaa katika kuitatua, mwishowe hufanikiwa.
    Ruwaza zifuatazo zinaweza kujitokeza: 
    1. Mhusika/msimulizi azaliwe katika familia maskini, apate tatizo la karo, asikate tamaa, ajitahidi masomoni na mwishowe kufanikiwa. 
    2. Mzazi awe na mtoto aliyepotoka kimaadili. Ajaribu kumrekebisha. Hali iwe ngumu, asikate tamaa, mwishowe afanikiwe kumrekebisha. 
    3. Nchi ikabiliwe na tatizo la mkurupuko wa ugonjwa, madaktari wajaribu kwa udi na uvumba kupata tiba, mwishowe wafanikiwe.
    4. Msimulizi/mhusika awe mwenye mahitaji maalum, ajaribu kukabiliana na adha zake, abaguliwe, asikate tamaa, mwishowe afanikiwe maishani/kitaaluma,
    5. Mwanasiasa ajaribukupata kiti cha ubunge, akose mara mbili au tatu, asikate tamaa, awanie mara kwa mara, mwishowe achaguliwe.
    6. Mhusika atafute kazi kwa muda, asipate, ajaribu bila kukata tamaaa, mwishowe afanikiwe.

      Tanbihi
      Kwa vyovyote vile insha lazima ionyeshe pande zote mbili za methali. Ugumu wa jambo ujitokeze, bidii au juhudi za kulishughulikia/ kutokata tamaaa kujitokeze, hatimaye mafanikio yaonekane.
  4.  
    1. Hii ni insha ya mdokezo.
    2. Inadokeza kwamba msimulizi ameyatenda makosa ambayo yanastahili kumfanya ajute.
    3. Hata hivyo amekata shauri kujirekebisha.
      Hali zifuatazo zaweza kujitokeza:
      1. Msimulizi azembee masomo, asifikie lengo la kielimu, atake kujuta lakini ajiase.
      2. Msimulizi atoroke kwao, ajiingize kwenye anasa. Pengine atunge mimba au aingilie matumizi mabaya ya dawa. Afikie mporomoko, lakini aamue kujirekebisha.
      3. Mhusika ajiingize katika ugaidi bila kujua. Ang'amue baadaye kuwa kapoteza utu wake. Atake kujuta, ajiase na kujirekebisha
      4. Mwanafunzi atoroke shule, apatikane na mwalimu, aadhibiwe, pengine afukuzwe shule. Ateseke. Atake kujuta lakini ajikanye nakuamua kuyajenga maisha upya.
      5. Mhusika ashiriki mauaji, asijulikane. Aishi kwa kusumbuliwa na dhamiri, anyong'onyee kihali na kimwili, afikie uamuzi wa kujirekebisha. 
      6. Mhusika awe mraibu wa vileo, azembee kazi, afutwe, ateseke, lakini awe na azima ya kujirekebisha.
      7. Mtahiniwa adanganye katika mtihani, agunduliwe, ibidi arudie masomo katika kiwango hicho, lakini awe na nia ya kujirekebisha.

        Tanbihi
        1. Kisa kioane na mwisho aliopewa.
        2. Asichopeke tu mwisho huu.
        3. Kisa kidhihirishe tatizo/matatizo ambayo yanasababisha mhusika/msimulizi kufikia kilele cha   kuvunjikiwa au kuteseka. 
        4. Anapofikia hali hii ndipo moyo unapomwelekeza kukata tamaa. Hata hivyo, anataka kurekebisha   mambo, Ndipo anahitimisha kwa kauli hii.
        5. Kisa sharti kiwe katika nafsi ya kwanza, umoja. Hata hivyo, msimulizi anaweza kutumia dayolojia za wahusika kuendeleza kisa. Katika hali hii nafsi ya tatu inaweza pia kutumiwa.
Join our whatsapp group for latest updates

Download KCSE 2017 Kiswahili Paper 1 with Marking Scheme.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?

Join our community on:

  • easyelimu app
  • Telegram
  • facebook page
  • twitter page
  • Pinterest