Kiswahili Paper 3 Questions and Answers - Kassu Jet Pre Mocks 2022

Share via Whatsapp

MAAGIZO

  1. Jibu maswali manne pekee.
  2. Swali la kwanza ni la lazima.
  3. Maswali mengine matatu yachaguliwe kutoka sehemu zilizozalia: Riwaya, Tamthilia, Hadithi Fupi na Fasihi Simulizi.
  4. Usijibu maswali mawili kutoka sehemu moja.
  5. Karatasi hii ina kurasa tano za maswali.

KWA MATUMIZI YA MTAHINI PEKEE

SWALI

UPEO

ALAMA

1

20

 

2

20

 

3

20

 

4

20

 

5

20

 

6

20

 

7

20

 

8

20

 

JUMLA

80

 


MASWALI

  1. LAZIMA

    USHAIRI
    Wafungwa wa kila mahali
    Niarifu zenu idhilali
    Maombolezo na machofu mlokabili

    Wavuvi wa kila bahari
    Leteni nyavu zilokumba hatari
    Na nguvu za mawimbi mlohimili

    Mafalahi wa kila jimbo duniani
    Nileteeni yenu matambara leteni
    Leteni hiyo mikono majuruhi
    Na yalonyauka matiti
    Na kucha zenu maiti
    Nyote leteni kwangu
    Leteni haraka leteni

    Naunda mikitaba yakini
    Ya dhiki za maskini
    Kumpelekea Manani
    Ishapotiwa saini
    na midomo ya wala njaa
    lakini, enyi mafukara wa dunia
    Hofu yangu kubwa namwambia
    Mungu huenda ikatukia
    Hajui kusoma ... hili nachelea

    Maswali

    1. Ainisha shairi hili. Toa sababu ya jibu lako. (alama 2)
    2. Tetea kwa kutoa hoja nne kauli kuwa utungo huu ni ushairi. (alama 4)
    3. Idhini ya mshairi inajitokeza vipi? (alama 3)
    4. Eleza ujumbe uliofumbatwa katika utungo huu. (alama 3)
    5. Ukitolea mifano, onyesha mbinu inayotawala katika shairi hili. (alama 2)
    6. Ubeti wa mwisho unakatisha tamaa. Thibitisha. (alama 3)
    7. Eleza muundo wa ubeti wa kwanza na wa pili. (alama 3)
  2. RIWAYA: CHOZI LA HERI - ASSUMPTA MATEI
    Jibu swali la pili au la tatu
    1. … haya imekuandama tangu usiku ukimtongoza fulani; siku za kuchora ramani ya Afrika kwa vyanda vya miguu, hadi sasa? Ama ni hizo mvi unaficha? Naskia ile mid-life crisis ikiwashika wazee ndiyo hivyo.
      1. Weka dondoo hili kwenye muktadha wake. (alama 4)
      2. Tambua mbinu zozote tatu za kimtindo kwenye dondoo hii (alama 3)
      3. Jadili sifa zozote tano za msemewa (alama 5)
    2. Thibitisha kauli kwamba ‘kweli jaza ya hisani ni madhila’ kwa kurejelea wahusika wanane kwenye riwaya ya Chozi la Heri. (alama 8)
  3. Hakuna marefu yasiyokuwa na ncha. Thibitisha ukweli wa methali kwa kurejele maudhui yoyote kumi katika Chozi la Heri (alama 20)
  4. TAMTHILIA: KIGOGO - PAULINE KEA
    Jibu swali la nne au la tano
    “Alizaliwa na meno mdomoni. Kisirani huyu! Wataka kuniharibia siku yangu nile nini? Wafikiri nauza nyonga kama huyo Tunu wako?”
    “ ... Boza, tusikoseane heshima. Nita...”
    “Jaribu uone! Ama unafikiri hao watu wenu, sijui watetezi wa nini watawatetea? Nanyi mheshimu uhuru wenu.”
    1. Bainisha vipengele sita vya kimtindo vilivyotumiwa kwenye dondoo. (alama 6)
    2. Yatambue mandhari ambamo mazungumzo haya yanafanyika. (alama 2)
    3. Onyesha jinsi mandhari uliyoyabainisha katika (b) yalivyotumiwa kuendeleza usimulizi wa hadithi. (alama 12)
  5. “Jukumu la kulinda uhai. Kulinda haki. Kulinda uhuru… Hujasahau mafanikio…”
    1. Weka dondoo hili katika muktadha wake. (alama 4)
    2. Fafanua hulka nne za msemewa zinazojitokeza ndani ya muktadha huu.(alama 4)
    3. Onyesha msemaji alivyofanikiwa katika azma yake ukirejelea tamthilia zima. (alama 4)
  6. HADITHI FUPI: TUMBO LISILOSHIBA NA HADITHI NYINGINE
    Jibu swali la sita au la saba
    Mame Bakari
    “Dunia we’ dunia. Dunia ya mwenye nguvu, si ya mimi dhaifu wa nguvu. Dunia ya msumari moto juu ya donda bichi. Hao watu je?”
    1. Eleza muktadha wa dondoo hili. (alama 4)
    2. Fafanua mbinu mbili za kimtindo zinazojitokeza katika dondoo hili. (alama 4)
    3. Thibitisha kauli “Dunia ya msumari moto juu ya donda bichi” ukirejelea Hadithi ya Mame Bakari. (alama 6)
    4. Fafanua jinsi mwanamke alivyosawiriwa katika hadithi hii. (alama 6)
  7. Tulipokutana Tena
    Nadhani kicheko chake kiliwaambukiza wenzangu maana vicheko vya nguvu viliwapasuka pamoja. Kama unavyoona, hivi vilikuwa vicheko vya mzaha na utani. Miongoni mwetu sote, Kazu alicheka zaidi. Alicheka kicheko mpaka mbavu zikamtafuna. Na alipocheka basi, alicheka kwa namna ya ajabu iliyonifurahisha sana. Alicheka huku ameviringa ngumi mbele ya kinywa kama ambaye anazuia hicho kicheko chenye nguvu za kutoa mwangwi uliosafiri robo dunia. Isitoshe, alipocheka namna hiyo, alijirusharusha kitini na kujivuta nyuma kwenye mgongo wa kiti na kuinua miguu yake mpaka soli za viatu vyake zikaonekak. Kumtazama Kazu akicheka ni namna ya kituko. Kila siku nikiwa naye, mimi huhakikisha kwamba namchekesha kwa mzaha huu na ule ili nimwone namna anavyocheka. Hata hivyo, yeye naye hakuwa mchekeshaji mdogo.
    “Aaa, hadithi za kichawi Kazu, ziko kila pahala duniani,” nilimwambia kwa kujitetea. “Unakumbuka mkasa maarufu hapa penu wa chatu lililotambaa kutoka Mashariki hadi Magharibi huku limemeza maelfu ya watu tumboni? Lilisafiri kwa masafa ya zaidi ya kilomita mia tano hivi na kuwatema watu hao huko Magharibi!”
    1. Tambua mbinu tano za kimtindo katika dondo hili. (alama 5)
    2. Eleza jinsi mwandishi alivyofaulu kutumia mbinu rejeshi katika kuijenga hadithi ya Tulipokutana Tena. (alama 5)
    3. Onyesha umuhimu wa mandhari ukirejelea Club Pogopogo. (alama 4)
    4. Hakiki matatizo aliyoyapitia Bogoa Bakari aushini mwake. (alama 6)
  8. FASIHI SIMULIZI
    Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali yanayofuata.

    Mabibi na mabwana, ndugu na marafiki hamjambo! Nimefika hapa leo kushuhudia sherehe za vijana hao wanaofuzu kuingia utu uzimani. Tangu jadi mababu zetu waliandaa sherehe kama hizi ili kuwaandaa vijana wao kukabiliana na maisha ya usoni. Wanangu, utu uzima hautokani tu na viviga au kisu cha ngariba. Ni matendo na tabia. Naam, ni matendo na tabia. Katika jamii ya sasa watu humpima mtu kutokana na ufanifu wake kiuchumi, kielimu na kijamii. Mtu asiye na mali yake hubezwa kwa kutofanya bidii inavyostahili. Hivyo basi, nawashauri vijana wanaofuzu leo kuwa, mnafaa kutia bidii masomoni ili mustakabali wenu uwe mzuri. Katika nyakati zetu, ubingwa wetu ulipimwa katika fani ya vita na ngoma. Ungewasikia wanaume wakijisifu kwa wimbo wakisema:
    Ooh ooh ooh!
    Mimi ni chuma inayoishi
    Ningiapo vitani, macho yangu tu huwafisha wengi.
    Viganja vyangu vimeiletea jamii yetu fahari
    Wananiita Ngao.
    Juzi ngomani niliwapiku wote
    Wanawali waliniangukia kwa kutaka uchumba
    Nani mwingine kama Ngao?

    Hata hivyo, hali katika jamii ya sasa ni tofauti. Ngoma imekuwa nyenzo ya burudani tu. Navyo vita vya kikabila vimepitwa na wakati. Wanaopigana aghalabu huchukiliwa hatua kali za kisheria. Elimu ni silaha ya pekee. Elimu itawafungulia milango ya heri. Ndugu na marafiki, nawaomba nyote muwasisitizie vijana hao umuhimu wa kuwatii walimu wao na kutia bidii masomoni watakaporudi shuleni. Msisite kuwaadhibu wanapokosea. Ni muhimu kukumbuka kuwa, mchelea mwana kulia hulia mwenyewe. Tulisimuliwa na bibi kuwa, hapo zamani za kale mwanamke fulani alificha mnyama hatari aliyekuwa akifukuzwa na mashujaa wa jamii. Baada ya mashujaa hao kuondoka, mnyama huyo alimla mwanamke huyo. Ingawa ni hadithi, kisa hicho kinatufunzwa kuwa, hatufai kuficha matendo mabaya ya wanetu. Tuwarekebishe mapema.
    Nikimaliza naomba kuwajuza vijana hawa kuwa, tohara siyo ufunguo wa ulevi. Inahuzunisha kuwakuta vijana wadogo wamelala matopeni kwa kushindwa kutembea kutokana na ulevi. Wengine hubaki pale hadi asubuhi wakitumbuizwa na milio ya vyura. Nina matumaini kuwa, kundi hili litakuwa tofauti. Asanteni kwa kunisikiliza.
    Maswali

    1. Tambua kipera katika dondoo. (alama 1)
    2. Eleza sifa za kipera ulichotaja katika (i) (alama 4)
    3. Eleza dhima zozote mbili za kipera ulichotaja katika (i) (alama 2)
    4. Tanzu za fasihi huingiliana na kutegemeana. Thibitisha kauli hii kwa kurejelea kifungu hiki. (alama 5)
    5. Eleza toni iliyobainika katika kifungu. (alama 2)
    6. Fafanua mbinu za kimtindo zinazodhihirika katika kifungu hiki. (alama 6)


MWONGOZO WA KUSAHIHISHIA

  1. USHAIRI
    1. Shairi huru (kimapinduzi). Halizingatii arudhi za utunzi.
    2.                      
      1. kuwepo kwa mishororo
      2. kuwepo kwa beti
      3. matumizi ya lugha ya mkato
      4. vina vinajitokeza kwa kiwango fulani
    3.                      
      1.  inkisari (kufupisha kwa maneno) km. Mlokabili badala ya mliokabili, zilokumba badala ya zilizokumba, mlohimili badala ya mliohimili
      2. kuboronga sarufi/kufinyanga sarufi – niarifu zenu idhilali badala ya niarifu idhilali zenu,, nileteeni yenu matambara – nilteeni matambara yenu
      3. tabdila – mikitaba – mikataba, majutuhi - majeruhi
    4. Mateso na dhiki zinazowakumba maskini –ya dhiki ya maskini kumpelekea Manani
      Hali duni ya maisha licha ya kujibidiisha kazini – matambara
      Hatari katika kufanya kazi – nyavu zilizokumba hatari, na nguvu za mawimbi mlohimili
    5. Takriri- leteni nyavu ..., nileteni yenu matambara leteni
    6. Msimulizi anasema anaunda mikataba ya dhiki za maskini ili amplekee Mungu, lakini hofu yake kubwa ni kuwa huenda ikatukia kuwa Mungu hajui kusema – anachelea hilo
    7. Mizani
      Ubeti wa kwanza            ubeti wa pili
      9                                          9
      10                                       12
      14                                       12
      Mishororo mitatu katika kila ubeti
      Vina
      Vina vya mwisho
      Ubeti wa 1
      -li
      - li
      - li
      Ubeti wa 2
      -ri
      - ri
      - li
  2. CHOZI LA HERI
    1. haya imekuandama tangu usiku ukimtongoza fulani; siku za kuchora ramani ya Afrika kwa vyanda vya miguu, hadi sasa? Ama ni hizo mvi unaficha? Naskia ile mid-life crisis ikiwashika wazee ndiyo hivyo;
      1. Weka dondoo hili kwenye muktadha wake. (Alama 4)
        • Msemaji ni Terry mawazoni mwa Ridhaa
        • Msemewa ni Ridhaa
        • Ridhaa yuko kwenye mawazoni uwanjani wa ndege wa Rubaa
        • Anakumbuka Maisha yake mkewe na aila yake huku akimgojea mwanawe mwangeka anayetoka ng’ambo
      2. Tambua mbinu zozote tatu za kimtindo kwenye dondoo hii (alama 3)
        • Taswira(mwono) kuchora ramani ya Afrika
        • Maswali ya balagha. Hadi sasa? Ama ni hizo mvi unaficha?
        • Kuchanganya ndimi. Mid-life crisis
        • Mbinu rejeshi/Kisengere nyuma – Ridhaa kukumbuka yaliyopita
      3. Jadili sifa zozote tano za msemewa (alama 5)
        • Sifa za Ridhaa
          • mwenye bidi- alifanya kazi zake kwa bidi hospitalini
          • mvumilivu- hata baada ya familia yake kufa na mali kupotea, alizidi kuvumilia hali hiyo mpya ya ukiwa
          • mwenye mapenzi- anaipenda aila yake na hata selume rafikiye.
          • Mshauri mwema- anaonekana kumshauri mwangeka mwanawe aoe na ajenge Maisha yake upya
          • Kadiria hoja ya mwanafunzi hapa. 1 x 5
      4. Dhibitisha kauli kwamba ‘kweli jaza ya hisani ni madhila’ kwa kurejelea wahusika wanane kwenye riwaya ya chozi la heri. (Alama 8)
        • Ridhaa aliwatendea hisani wahafidhina kwa kupanda miti kwenye Kijiji na kusambaza maji ya mabomba, hatimaye alichukuliwa kama mgeni mahali hapo hata kuchomewa mali yake na familia yake kuuawa.
        • Selume hata baada ya kumpenda mumewe na kuishi vyema na wakweze, anafukuzwa nyumbani kwa kutofautiana nao kwa misingi ya kisiasa na kujipata kwenye msitu wa mamba.
        • Makaa- alijitolea mhanga kuwaokoa wananchi waliokuwa wakifyonza mafuta kwenye lori iliyoanguka. Mshahara wake ulikuwa kifo cha uchungu.
        • Lunga alitetea haki za wananchi wasije wakanunuliwa mahindi mabovu na muishowe akapigwa kalamu kazini.
        • Mwekevu aliwajengea wanachi visima katika sehemu zilizokuwa na ukame. Hatimaye walimsaliti kwa kusema hawawezi kuongozwa na mwanamke na nuishowe kupigana na kusababisha maangamizi makubwa.
        • Kiriri alijizatiti kuwasomesha wanawe ugaibuni na hata mkewe, baadaye familia hiyo walikataa kurejea nyumbani na kumsabaishia kihoro akafa.
        • Billy alimjengea Sally kijumba ili waishi raha mstarehe, alipompeleka aone jumba, aliambiwa kuwa nyumba hiyo ilikuwa kama kiota cha ndege.
        • Babake Tuama alimshauri bintiye kutokeketwa na badala yake Tuama alikeketwa na kujipata katika hali mbaya hospitalini na kumsabishia aibu babake.
        • Zohari- baada ya wazazi wake kumkimu kwa mahitaji yake yote hadi kumpeleka shuleni, alijiingiza kwa mapenzi ya kiholela na kusababisha mimba ya mapema. Baadaye anaalifukuzwa shuleni na akatoroka nyumbani.
        • Kadiria majibu. (Hoja moja kwa kila mhusika) 8 x 1
  3.                          
    1. Vita: baada ya vita vya baada ya uchaguzi, mapigano hayo yalifika mwisho na watu wakaishi Maisha mapya.
    2. Elimu. Ridhaa alighadhabika alipoitwa mfuata mvua shuleni na mwizi wa kalamu, hatimaye aliweza kusoma hadi kiwango cha chou kikuu.
    3. Ukosefu wa ajira- shamsi alisoma na kuwa jogoo wa kwanza musomi kwenye Kijiji chao, hatimaye anasikika akinungunikia kutoajiriwa kwenye wimbo wake.
    4. Changamoto za ndoa- Naomi hata baada ya kuishi na mumewe na kujaliwa Watoto, hatimaye anawaacha na kupotea asijulikane aliko.
    5. Ubakaji- wanawe kaizari lime na mwanaheri wanabakwa huku babake akiona na mwishowe wanayajenga upya Maisha yao.
    6. Dhulma za wanadamu- Dick anabadilika baada ya kutekwa nyara na kutumiwa kuuza dawa za kulevya.
    7. Mauaji- familia ya ridhaa wanauawa kw na kuchomeka kiasi cha kutoatambulika kwa sababu ya ukabila.
    8. Uharibifu wa mali- waandamanaji walipora maduka na vijana wakachoma magari kwa mabomu ya petroli kwa gadhabu waliokuwa nayo baada ya uchaguzi. Yote yakaisha na watu wakarudi sawa.
    9. Utengano – Dick, Umu na Mwaliko walikutana mwishowe.
    10. Ukiukaji wa haki za Watoto- Sauna anawauza Dick na Mwaliko kwa Buda badala ya kuwatunza. Buda anawafundisha namna ya kuuza dawa za kulevya. Sauna akashikwa na kufungwa.
    11. Umaskini; Kangata na mke wake Ndarine waliishi msitu wa mamba kwa muda murefu kwani hawakuwa na makwao. Waliishi kwa shamba ya mwajiri wao aliyeishi mjini. Mwishowe wakamiliki ardhi.
      Hakiki Hoja zozote 10 x 2 = 20
      Tamthilia
  4.                    
    1. Vipengele vya kimtindo
      • Chuku- alizaliwa na meno mdomoni
      • Siyahi/nidaa- Kisirani huyu!
      • Balagha- wataka kuniharibia siku yangu nile nini?
      • Tashbihi- wadhani nauza nyonga kama huyo Tunu wako?
      • Ulinganuzi- kuna hali ya kulinganua watu wawili mfano: Wafikiri nauza nyonga kama huyo Tunu wako?
      • Mdokezo- Nita...
      • Kejeli- sijui watetezi wa nini watawatetea
      • Kinaya- Nanyi mheshimu uhuru wenu- ni kinyume cha matarajio kwa vile watu hawana uhuru unaorejelewa bali wanatawaliwa kiimla na Majoka.
      • (Hoja za kwanza 6x1=6)
    2.  Mandhari
      • Mangweni- hapa ni mahali shughuli za utengenezaji na unywaji wa pombe haramu zinafanyika. (1x2=2)
    3. Jinsi mandhari yanaendeleza usimulizi wa hadithi. (alama 12)
      • Kuonyesha jinsi baadhi ya wanajamii walivyozamia katika shughuli za anasa.
      • Kuonyesha madhara ya ulevi. Sudi anasema, “Hatujaja hapa kuchoma mafigo yetu bwana” uk 57. Aidha pombe inasababisha upofu na vifo.
      • Kuashiria mabadiliko katika maisha ya mhusika- Tunaelezwa kuwa awali, Siti alikuwa mnywaji wa pombe haramu. (uk. 58)
      • Kuonyesha jinsi uongozi unatolewa kwa misingi ya kinasaba. Ngurumo anamuuliza Tunu yeye ni nani, babake au babuye walikuwa nani Sagamoyo.
      • Kuonyesha juhudi za wapiganiaji uhuru. Sudi anasema mashujaa halisi ni wale waliowahangaisha wakoloni hata wakawatimua. (uk. 58)
      • Kuonyesha utepetevu masomoni- Ngurumo anasema hakulipenda somo la Historia.
      • Kuonyesha ubarakala- Ngurumo anasema kura yake hampi tunu heri ampe paka.
      • Kuonyesha jitihada za wakombozi. Tunu anawaeleza walevi pale mangweni kuwa wamefika hapo ili kuwaalika kuhudhuria mkutano nje ya lango la soko la Chapakazi. (uk. 59)
      • Unywaji wa pombe unasababisha utegemezi- Ngurumo anasema watu wa kigogo wao wakipitia mangweni hawakosi kuwapa kitu kidogo. (uk. 60)
      • Kuonyesha kutamauka- baada ya soko kufungwa, watu wanahamia mangweni ili kujiliwaza. (uk. 61)
      • Utawala kuidhinisha utengenezaji na ulanguzi wa pombe haramu. Kwa kufanya hivi ni kwenda kinyume na sheria za jimbo lao. (uk. 61)
      • Kuonyesha uzinifu. Ngurumo ana uhusiano wa kimapenzi na Asiya ambaye ni mkewe Boza. (uk. 64)
      • Kudhalilishwa kwa mwanamke- Ngurumo anawaongoza walevi wengine kuimba wimbo wa kumkejeli Tunu. (uk. 65)
        (Hoja zozote 6x2= 12)
  5.                        
    1. Weka dondoo katika muktadha wake. (Alama 4)
      1. Msemaji ni Tunu.
      2. Msemewa ni Sudi.
      3. Wako nyumbani kwa Sudi (barazani).
      4. Tunu anajaribu kumshawishi Sudi waendelee na harakati za ukombozi Sagamoyo.
    2. Fafanua hulka nne za msemewa zinazojitokeza ndani ya muktadha huu. (Alama 4)
      1. Bidii – Licha ya kufungwa kwa soko la Chapakazi walikofanyia kazi, anaendeleza juhudi za uchongaji vinyago barazani mwake.
      2. Mzalendo –Anaitikia wito wa Siti kwenda kwenye shughuli za maandamano walikouawa vijana tano. Anahimiza waende bila kuchelewa.
      3. Ni mlezi mwema – Anamtuliza mwanawe Pili na kumhakikishia kuwa atampa chakula.
      4. Ni mwenye mapenzi kwa wanawe – Anaijali hali ya wanawe. Anamkumbatia Pili na kumpa ahadi ya kumpa chakula.
      5. Ni mwenye kukata tamaa – Anaelekea kukata tamaa ya kushiriki kwenye harakati za ukombozi. Anaona kama hili linamzuia kuwajibikia riziki ya familia yake.
    3. Onyesha msemaji alivyofanikiwa katika azma yake ukirejelea tamthilia zima. (Alama 12)
      (Alikuwa na azma ya Kulinda uhai. Kulinda haki. Kulinda uhuru n.k )
      1. Anafaulu kutoa suluhu kwa njaa iliyowakaba wanawe Sudi. Anasema wapelekwe kwao mama yake angewalisha na kuwatunza.
      2. Anafanikiwa kumshawishi Sudi waendelee na harakati za ukombozo wa Sagamoyo. Hii ni licha ya Sudi kutaka kukata tamaa.
      3. Akiwa chuoni, alipata mafaniko katika mapambano ya kutetea haki akiwa kiongozi wa wanafunzi.
      4. Aliazimia kusomea sheria chuoni na akafanikiwa kusoma hadi kiwango cha uzamifu.
      5. Anafaulu kumkabili Majoka ana kwa ana ofisini mwake. Anatumika fursa hiyo kumwambia Majoka kuhusu mapungufu ya uongozi wake k.v kuendeleza mauaji.
      6. Anafaulu kupinga ujenzi wa hoteli ya kibanafsi kwenye Soko la Chapakazi. Majoka alinuia kujenga hoteli hiyo baada ya kuvibomoa vibanda vya soko.
      7. Anafanikiwa katika juhudi za kutaka soko lifunguliwe. Anaongoza mkutano unaokuwa kilele cha kulirejesha soko mikononi mwa wanasagamoyo.
      8. Azma yake ya kukutana majangili waliomshambulia inatimia anapompata Ngurumo mangweni na kukemea kitendo chake cha kikatili.
      9. Anatimiza lengo lake la kuwazindua wanasagamoyo waliozamia ulevini. Anawahimiza kuijali kesho yao.
      10. Anafanikiwa katika kulaani uuzaji wa pombe haramu. Akirejelea katiba ya nchi, anamkumbusha Asiya kuwa ni hatia kuuza pombe haramu.
      11. Anaukemea uasherati katika jamii. Anakejeli ‘keki za uroda’ zilizookwa na Asiya aliyepata kandarasi kwa kumpa ngurumo uroda.
      12. Anafanikiwa kuongoza maandamano pamoja na wanaharakati. Maandamano hayo yalichapishwa kwenye gazeti.
      13. Anafanikiwa kuwahutubia waandishi wa habari kuhusu kufujwa kwa pesa za kusafisha soko, kunyimwa haki kwa wauzaji n.k
      14. Anafaulu kuwa na wafadhili wanaofadhili gazeti linaloandika taarifa kuhusu harakati na kuendeleza harakati za ukombozi Sagamoyo.
      15. Tunu anafikiwa kuzipeperusha habari za uanaharakati moja kwa moja kupitia runinga ya mzalendo na katika mitandao ya kijamii.
      16. Anafaulu kuwaleta wanasagamoyo pamoja dhidi ya uongozi wa Majoka. Watu waliususia mkutano wa Majoka wakaenda mkutano wa Tunu nje ya lango la soko.
      17. Anapata nafasi ya kuwatolea hotuba wanasagamoyo nje ya lango la soko. Anawakumbusha wanasagamoyo kuhusu maana halisi ya uhuru wao.
      18. Anapata mafanikio baada ya kupata uungwaji mkono na mkuu wa polisi Bwana Kingi. Anakubali kuulinda usalama wa waliohudhuria mkutano nje ya lango la soko.
      19. Azma yake ya kupinga kuchaguliwa kwa viongozi wabaya inafaulu. Wanasagamoyo wanaahidi kutowachagua viongozi wa aina hiyo tena.
      20. Tunu anafaulu katika kuinua hadhi ya wanawake Sagamoyo. Anatambuliwa kwa juhudi zake za kuleta ukombozi; Sudi anazindua kinyago chake kusherehekea uhuru wa kweli.
        HADITHI FUPI
  6. MAME BAKARI
    1.                        
      • Muktadha wa dondoo
      • Haya ni maneno ya Sara katika uzungumzi nafsia.
      • Anawaza akiwa nyumbani kwao
      • Anawazia dhuluma ambazo angepata baada ya kubakwa na janadume.
    2.                      
      • Mbinu za kimtindo katika dondoo
      • Uradidi/takriri …dunia dunia
      • Jazanda…dunia ya msumari moto juu ya kidonda
      • Balagha…hao watu je?
      • Kadiria. Zozote 2x2=4
    3. Kudhibitisha kauli “Dunia ya msumari moto juu ya donda mbichi”
      1. Sara angetengwa,kusutwa na kukashifiwa kwa kosa lisilo lake
      2. Babake ‘angemchinja’au amfukuze nyumbani
      3. Kukosa kuaminika.Sara anahofia babake huenda asimwamini
      4. Kufukuzwa shuleni. Sara anahofia kuwa angefukuzwa shuleni
      5. Kupata ujauzito. Sara anaambulia ujauzito baada ya kubakwa na janadume
      6. Dhiki za kisaikolojia
      7. Janadume linapatikana likijaribu kumbaka msichana mwingine,baada ya kumnajisi Sara
        Tanbihi .Hoja zizingatie masaibu ya Sara baada ya kubakwa. Zozote 6x1=6
    4. Mwanamke alivyosawiriwa katika hadithi.
      1. Anadhulumiwa kimapenzi –Sara
      2. Anatumiwa kama chombo cha kumridhisha mwanamme
      3. Msiri -Sara
      4. Mwenye kuwajibika – Beluwa
      5. Mwenye busara –mamake Sara
      6. Kiumbe dhaifu –Sara baada ya kubakwa
        Kadiria zozote 6x1=6
      7. TULIPOKUTANA TENA
  7.                    
    1. Mbinu za mtindo
      1. Tashhisi/uhuishi …mbavu zikamtafuna
      2. Takriri/uradidi…alicheka kicheko
      3. Chuku…uliosafiri robo dunia
      4. Utohozi… soli
      5. Nidaa…magharibi!
      6. Taswira.. kicheko cha Kazu
    2. Matumizi ya mbinu rejeshi
      1. Sebu anakumbuka habari za rafiki yake Bogoa aliyaletwa kijijini mwao uk108
      2. Bogoa alivyopelekwa mjini na babake kuishi na rafiki uk 115
      3. Bogoa alivyoishi kwa shida kwa Bi. Sinai uk 118
      4. Sebu anakimbuka maisha ya ujana wao na Bogoa uk 119
      5. Sebu ankimbuka akimuuliza Bogoa kilichofanyika kwa viganja vyake uk119
      6. Jinsi Bogoa na Sebu walivyokuwa wakicheza densi uk 119
        Kadiria zozote 5x1=5
    3. Umuhimu wa Club Pogopogo
      1. Eneo la mkutano wa kina Kazu na Bogoa
      2. Kazu anakutana na mke wa Bogoa – Sakina
      3. Hali ya kiuchumi ya Kazu na wenzake inabainika ( Club ni maarufu kwa watu wa kipato cha chini uk111)
      4. Tunafahamu alivyofika mjini Bogoa
      5. Ukatili wa Bi Sinai
      6. Kifo cha wazazi wa Bogoa na Bi Sinai
      7. Kutoroka kwa Bogoa kutoka kwa Bi Sinai
      8. Eneo la burudani
        Kadiria zozote 4x4=4
    4.  Matatizo ya Bogoa
      1. Kutengana na wazazi katika umri mdogo
      2. Kukosa elimu
      3. Kufanyishwa kazi za kitumwa(mtahinwa anaweza kuorodhesha zile kazi kama hoja inayojisimamia)
      4. Kunyimwa muda wa kucheza na watoto wenzake
      5. Kunyimwa chakula na kupewa makombo
      6. Kulia sufuria
      7. Kuchomwa viganja
        Kadiria zozote 6x1=6
  8. FASIHI SIMULIZI
    1. Tambua kipera katika dondoo. (alama 1)
      hotuba
    2. Eleza sifa za kipera ulichotaja katika (i) (alama 4)
      1. Hutolewa na watu maalum walioteuliwa kuzungumza.
      2. Watu wanaotoa hotuba aghalabu huwa na umilisi mkubwa wa lugha.
      3. Hotolewa kwa nafsi ya kwanza.
      4. Mtoaji hotuba anaweza kutumia viziada lugha kama vile ishara za mikono.
      5. Hotuba huteuliwa mada mahususi wala haizungumzii jambo lolote.
        Zozote 4 x 1 = 4
    3. Eleza dhima zozote mbili za kipera ulichotaja katika (i) (alama 2)
      1. Kuwaelimisha wanajamii kwa kuwapa maarifa ya kukabiliana na maisha.
      2. Kuadilisha na kutoa nasaha hadharani.
      3. Huimarisha ukakamavu wa kuzungumza kadiri watu wanavyotoa hotuba hadharani.
      4. Kukuza ufasaha na umilisi wa lugha.
      5. Kupalilia kipawa cha uongozi. Zozote 2 x 2 = 2
    4. Tanzu za fasihi huingiliana na kutegemeana. Thibitisha kauli hii kwa kurejelea kifungu hiki. (alama 6)
      Kifungu hiki ni cha hotuba. Hata hivyo, hotuba yenyewe imejumuisha tanzu nyingine za fasihi simulizi kama vile:
      1. Kuna matumizi wa nyimbo – wimbo uliotumika unaonyesha jinsi watu walivyojisifu kwa uhodari wao vitani na ngomani.
      2. Hadithi – hadithi inayohusu mwanamke na nyama inarejelewa.
      3. Semi – kifungu hiki kimejumuisha methali na nahau. Kwa mfano, mchelea mwana kulia hulia mwenyewe.
      4. Miviga – msimulizi anadokeza kuhusu tohara kwa vijana kwa kutaja kisu cha ngariba.
        Zozote 3 x 2 = 6
    5.  Eleza toni iliyobainika katika kifungu. (alama 2)
      Toni ya kushauri – nafsi neni anawashauri vijana waliopashwa tohari na walezi wao.
      Kutaja 1, kueleza 1
    6. Fafanua mbinu za kimtindo zinazodhihirika katika kifungu hiki. (alama 5)
      1. Methali – mchelea mwana kulia hulia mwenyewe.
      2. Nahau – kutia bidii
      3. Mbinu rejeshi – nafsi neni anarejelea simulizi ya bibi.
      4. Takriri – ni matendo na tabia
      5. Taswira – vijana wadogo wamelala matopeni; wakitumbuizwa na milio ya vyura
      6. Tashihisi – elimu itawafungulia milango ya heri
      7. Sitiari – elimu ni silaha ya pekee
        Zozote 5 x 1 = 5
Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Paper 3 Questions and Answers - Kassu Jet Pre Mocks 2022.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?

Join our community on:

  • easyelimu app
  • Telegram
  • facebook page
  • twitter page
  • Pinterest