Kiswahili Paper 2 Kenya High Post Mock Exams 2020 - Questions and Answers

Share via Whatsapp

MAAGIZO

  • Jibu maswali yote.
  1. UFAHAMU: (Alama 15)
    Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali yanayofuatia

    Mateso ya wanawakiwa ni suala la kijamii linalofaa kutazamwa kwa darubini kali. Hata hivyo wanaoathirika zaidi ni watoto ambao bado wako katika umri unaohitaji kulelewa na kupewa mahitaji ya msingi kama mavazi, malazi, elimu na mengine anuwai. Hali ya kuachwa na wazazi imekuwa ikizikumba jamii tangu enzi za mababu na kila itokeapo, wanajamii huipokea kwa mitazamo tofautitofauti, hivyo kuwafanya wanawakiwa kuathirika sana.

    Baadhi ya jamii zina imani za kijadi pamwe na mila zilizochakaa zinazozifanya kuamini kuwa baadhi ya vifo hutokana na laana. Wengine huchukulia kuwa mwendazake ameondolewa na ulozi. Imani kama hizi huifanya jamii kuwatia watoto walioachwa katika mkumbo ule ule, hivyo kuwaangalia kwa macho yasiyo ya kawaida. Hili husababisha dhana gande. Hali hii husababisha kuwachukulia watoto kama wanaotoka katika kizazi kilicholaaniwa. Jamii basi hukosa kuwapa watoto hawa stahiki yao. Hata wanapojitahidi kuiwania nafasi yao, waliowazunguka huwavunja mioyo. Jitihada zao huishia kuwa si chochote kwa kuwa jamii inawatazama kama waliolaaniwa.

    Punde baada ya mzazi mmoja au wote wawili waendapo wasikorudi, inatarajiwa kwamba aliyeachiwa mtoto, awe mzazi wake, mwanafamilia au jirani awajibike na kumtunza mwanamkiwa. Kunao kadha wa kadha wanaowajibika – ninawavulia kofia. Hata hivyo wengi hutelekeza jukumu hili walilopewa na Muumba. Si ajabu basi kuona kuwa idadi ya watoto wanaozurura mitaani inazidi kuongezeka kila uchao. Ukichunguza utakuta kuwa wengi wa watoto hawa ni waliopotelewa na wazazi wao. Inakera zaidi kugundua kuwa baadhi ya watoto hawa wana mzazi mmoja. Kwamba mke au mume wa mtu ameaga, au iwe kwamba mzazi mmoja alimzaa mtoto na kumwachia mwenzake mzigo wa ulezi, aliyeachiwa ana jukumu la kumpa mwanawe mahitaji ya msingi. Machoni pa Jalali, kila anayeupuuza wajibu huu ana hukumu yake siku ya kiama!

    Ni haki ya kila mtoto kupata elimu. Katika katiba ya Kenya mathalan, elimu ya msingi, yaani kuanzia shule ya chekechea had kidato cha nne ni ya lazima. Tangu hapo hata hivyo, jamii zimekuwa zikiwanyima wanawakiwa wengi elimu. Kwamba kunao wachache wanaowaelimisha baadhi ya wanawakiwa, ni kweli. Hata hivyo, wengi hukosa hata wa kuwapeleka katika shule ya chekechea, hivyo kuishia kutojua hata kuandika majina yao. Mfikirie mtu katika karne ya 21, asiyejua kusoma wala kuandika! Nani ajuaye, huenda huyo mwanamkiwa asiyepelekwa shuleni ndiye angalikuwa profesa, daktari, mwalimu, rubani au msomi mtajika na mtaalamu wa uwanja muhimu katika jamii!

    Kila mtoto ana haki ya kulelewa hadi kufikia utu uzima kabla ya kupewa majukumu mazito. Katika katiba ya Kenya, utu uzima, ulio umri wa kuanza kufanya kazi huanzia miaka 18. Wanaohakikisha watoto hawa wametimiza utu uzima kabla ya kufanyishwa gange ngumu wanafaa pongezi. Hata hivyo wanawakiwa wamekuwa wakitumiwa na wengi kama punda wa huduma. Wanaaila wengine huwachukua wanawakiwa kwa machozi mengi wazazi wao waagapo nakuapa kuwahifadhi na kuwatunza wana wale wa ndugu zao, kumbe ni machozi ya simba kumlilia swara! Hata kabla ya mwili wa mzazi mhusika kuliwa na viwavi, mateso kwa mtoto yule huanza, akawa ndiye afanyaye kazi zote ngumu. Utakuta watoto wao wamekaa kama sultan bin jerehe huku mwanamkiwa yule akiwapikia, kuwafulia nguo, kudeki, karibu hata awaoshe miili! Kazi kama zile za shokoa huwa za sulubu na aghalabu husindikizwa kwa matusi yasiyoandikika.

    Baadhi ya waja walionyimwa huruma huwahadaa wanawakiwa na kuwapeleka ng’ambo wakitumia vyambo, kuwa wakifika kule watapata kazi za kifahari. Maskini wale hushia kushikwa shokoa, wakawa watumwa katika nyumba za waajiri wao, bila namna ya kujinasua. Wengine hushia kutumiwa kama watumwa wa ‘kimapenzi’ katika madanguro, miili yao ikawa ya kuuziwa makahaba waroho wasiojali utu. Kujinasua kule huwa sawa na kujitahidi kuokoa ukuni uliokwishageuka jivu, maadamu wanawakiwa aghalabu hukosa watu wenye mioyo ya huruma ya kuwashughulikia. Wengi huitumia methali ‘mwana wa ndugu kirugu mjukuu mwanangwa’ kuwapuuzilia mbali wanawakiwa ambao hukimbiliwa tu wabinafsi hawa wanapofaidika wenyewe.

    Maswali
    1. Ipe taarifa hii anwani mwafaka. (alama 1)
    2. Eleza dhana ya mwanamkiwa kwa mujibu wa kifungu. (alama 2)
    3. Eleza imani za kijadi kuhusiana na wanawakiwa. (alama 2)
    4. Jadili masaibu yanayowakumba wanawakiwa. (alama 4)
    5. Eleza haki mbili za kikatiba zilizokiukwa kuhusiana na wanawakiwa. (alama 4)
    6. Eleza maana ya msamiati ufuatao kulingana na kifungu. (alama 2)
      1. Inakera
      2. Majukumu
  2. UFUPISHO: (Alama 15)
    Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali

    Runinga kama kifaa kingine chochote cha mawasiliano kina manufaa yake. Kwanza kabisa, ni nyenzo mwafaka ya kufundishia. Vipindi vinavyopeperushwa katika runinga huwa na mafunzo kemkemu kwa mtu wa kila rika. Halikadhalika, runinga huweza kuleta vipindi ambavyo huwafahamisha watu mambo yanayoendelea katika mazingira yao na duniani. Aidha, runinga ikitumika pamoja na michezo ya video huauni katika ukuzaji na ustawishaji wa stadi ya kujifundisha au kujielimisha. Michezo ya video, hasa ya kielimu, huwafanya watu kujenga umakini pamoja na kuchua misuli ya ubongo na kuwafanya watu kuwa macho wanapofanya kazi.

    Fauka ya hayo, televisheni ni chemchemi bora ya kutumbuiza na kuchangamsha. Hakuna mtu asiyependa kuchangamshwa. Televisheni ni mojawapo ya vyombo mwafaka vya kutekeleza hayo kutokana na vipindi vyake. Uburudishaji huu huwa ni liwazo kutokana na shinikizo na migogoro tunayokabiliana nayo kila siku. Uburudishaji huu hupatikana kwa urahisi majumbani mwetu.

    Vivyo hivyo, runinga hutumika kama nyenzo ya kuendeleza utamaduni, kaida na amali za jamii. Vingi vya vipindi vya runinga huwa ni kioo ambacho huakisi mikakati na amali za jamii.

    Kwa upande mwingine, hakuna kizuri kisichokuwa na dosari. Licha ya manufaa yake, televisheni imedhihirika kuwa na udhaifu wake. Kwanza, baadhi ya vipindi vya runinga na video hujumuisha ujumbe usio na maadili, kama vile matumizi ya nguvu za mabavu, ngono za kiholela, lugha isiyo ya adabu, ubaya wa kimavazi na maonevu ya rangi, dini, jinsia, kabila na utamaduni. Si ajabu kuwa baadhi ya vijana wetu wanaiga baadhi ya mambo haya. Vijana wetu siku hizi wameingilia ulevi wa pombe na afyuni, ngono za mapema kabla ya ndoa na mavazi yanaowaacha takribani uchi wa mnyama. Wengi wamekopa na kuyaiga haya kutoka katika runinga. Ukiwauliza wafanyacho, watakujibu kuwa ni ustaarabu kwani wameupata katika runinga.

    Matumizi ya runinga na michezo ya video yasiyodhibitiwa huweza kuwa kikwazo cha mawasiliano bora miongoni mwa familia. Matumizi kama haya huwapa wanafamilia fursa ya kujitenga. Imedhihirika kuwa runinga haichangii kujenga uhusiano bora wa kijamii. Ukilinganisha na vyombo vingine vya burudani ambavyo hutoa nafasi ya watu kutangamana na kujenga uhusiano bora, televisheni haichangii haya. Badala yake, tajriba ya televisheni huwa ya kibinafsi. Hali hii inapotokea katika kiwango cha familia, televisheni inaweza kutenganisha wazazi na watoto wao.

    Halikadhalika, runinga na video aghalabu hueneza maadili yasiyofaa. Mathalani, baadhi ya vipindi vya televisheni huendeleza hulka ya kuhadaa, ngono za kiholela, kuvunjika kwa ndoa, n.k. Hulka hizi zisizoendeleza maadili ya kijamii huchukuliwa kama zinazofaa na zinazofuatwa na waliostaarabika. Huu ni upotovu.

    Isitoshe, baadhi ya matangazo huhimiza matumizi ya dawa za kulevya kama tembo na sigara. Vitu hivi vinapotangazwa, hupambwa kwa hila na udanganyifu mwingi ambao huwavutia vijana na watoto wengi. Si ajabu mtu anapouliza wanaotumia vileo hivi walivyoanza, watajibu kutokana na athari za matangazo katika runinga na vyombo vingine.

    Utafiti umeonyesha kuwa vipindi vya runinga na video ni chanzo cha matumizi ya nguvu za mabavu miongoni mwa wanafunzi. Wazazi wengi huchukulia vibonzo katika televisheni kuwa vinalenga kuburudisha tu na havina ubaya wowote. Lakini ukweli ni kuwa vipindi vingi vya vibonzo hushirikisha matumizi ya hila na nguvu za mabavu. Haya huibusha hamu ya vijana na watoto huyaiga.

    Kwa hivyo, ni muhimu wazazi na jamii kutambua madhara ya televisheni. Utambuzi huu utawafanya wawaelekeze vijana na watoto jinsi ya kutumia televisheni na video ili kuepukana na madhara yake.
    1. Fupisha aya tatu za kwanza za (maneno 70 – 75) (alama 7, 2 za utiririko)
      Matayarisho
      _______________________________________________________________________
      Jibu
      _______________________________________________________________________
    2. Eleza udhaifu wa runinga na video. (maneno 50 – 51) (alama 5, 1 ya utiririko)
      Matayarisho
      _______________________________________________________________________
      Jibu
      _______________________________________________________________________
  3. MATUMIZI YA LUGHA: (alama 40)
    1. Taja aina mbili kuu za ala za kutamkia sauti (alama 2)
    2. Taja mfano mmoja mmoja wa sauti zifuatazo (alama 2)
      1. Kimadende
      2. Kipasuo kwamizo
    3. Huku ukitoa mfano, eleza maana ya sentensi sahili (alama 2)
    4. Ainisha mofimu katika neno lifuatalo (alama 3)
      Tulimpikia
    5. Ainisha vitenzi katika sentensi: Kitabu anachotaka kusoma ki mezani (alama 3)
    6. Tunga sentensi moja ukitumia kiunganishi kiteuzi (alama 2)
    7. Nomino zifuatazo zimo katika ngeli gani? (alama 2)
      1. Uzi____________________________
      2. Muda__________________________
    8. Tumia ‘o’ rejeshi ya kati katika sentensi ifuatayo (alama 2)
      Watu ambao walifika jana ni wale ambao walitoka mbali
    9. Onyesha shamirisho kipozi na ala katika sentensi ifuatayo (alama 2)
      Mwindaji haramu alimuua ndovu kwa bunduki
    10. Changanua sentensi ifuatayo ukitumia mistari au mishale (alama 3)
      Kilipikwa jana jioni
    11. Andika sentensi ifuatayo katika hali yakinishi (alama 2)
      Msingesoma kwa bidii, msingepita
    12. Tunga sentensi moja kudhihirisha dhamira/jukumu hili (alama 2)
      Rai/ombi
    13. Ainisha vishazi katika sentensi ifuatayo (alama 2)
      Mtoto ambaye alianguka jana ana maumivu mengi
    14. Onyesha matumizi yoyote mawili ya kiwakifishi: koma/kituo (alama 2)
    15. Tumia neno ‘Nairobi’ kama (alama 2)
      1. Nomino
      2. Kielezi
    16. Tunga sentensi moja kutofautisha maana ya kuku na gugu (alama 2)
    17. Onyesha matumizi ya kiambishi -ji- katika sentensi (alama 2)
      Mwogeleaji stadi anajishaua sana.
    18. Andika katika usemi wa taarifa (alama 2)
      “Wageni wangu watafika saa ngapi? Mama aliuliza
    19. Unda nomino kutokana na kitenzi (alama 1)
      Safari
  4. ISIMUJAMII: (alama 10)
    Nipe chai, andazi mbili na egg moja………….
    1. Taja sajili inayorejelewa na maneno haya (alama 2)
    2. Fafanua sifa nne zinazohusishwa na sajili hiyo (alama 8)


MARKING SCHEME

  1.  
    1. Wanawakiwa/mateso ya wanawakiwa. (alama 1)
    2. Ni mtoto aliyefiwa na mzazi mmoja au wote. (alama 1)
    3.  
      1. Baadhi ya vifo hutokana na laana.
      2. Mwendazake ameondolewa na ulozi. 2x1=2
    4.  
      1. Wanatelekezwa na walioachiwa jukumu la kuwatunza hivyo kuishia kuwa watoto    wanaozurura mitaani.
      2. Hawapelekwi shuleni
      3. Fanyishwa kazi ngumu
      4. Wanadaiwa na kupelekwa ng’ambo kuwa watapata kazi za kifahari lakini wanaishia kuwa watumwa wa kimapenzi
        4x1=4
    5.  
      1. Haki ya elimu ya msingi
      2. Kulelewa hadi kufikia utu uzima kabla ya kupewa majukumu mazito 
        za kwanza 2x2=4
    6.  
      1. Inaudhi/inakasirisha
      2. Kazi/wadhifa 2x1=2
        Adhabu
        Sarufi - ½ x 6 s=3
        Hijai - ½ x 6 h=3
  2.  
    1.  
      1. Runinga ina manufaa yake
      2. Ni nyenzo mwafaka ya kufundishia
      3. Vipindi vinayopeperushwa huwa na mafunzo kwa kila mtu
      4. Huleta vipindi ambayo huwafahamisha watu mambo ambayo yanaendelea katika mazingira yao
      5. Ikitumika pamoja na michezo ya video husaidia katika ukuzaji na ustawishaji wa stadi ya kujifundisha/kujielimisha
      6. Michoro ya video huwafanya watu kujenga umakini pamoja na kuwafanya watu kuwa makini wanapofanya kazi
      7. Ni chemchemi bora ya kutumbuiza na kuchangamsha
      8. Uburudishaji huu huwa ni liwazo kutokana na shinikizo na migogoro
      9. Hupatikana kwa urahisi majumbani mwetu
      10. Hutumika kama nyenzo ya kuendeleza utamaduni, kaida na amali za jami
        zozote 7x1=7
    2.  
      1. Baadhi ya vipindi hujumuisha ujumbe usio na maadili
      2. Vijana mengi wamekopa na kuyaiga wanayoyaona katika runinga
      3. Matumizi yasiyodhibitiwa huweza kuwa kikwazo cha mawasiliano bora miongoni mwa familia
      4. Aghalabu hueneza maadili yasiyofaa
      5. Baadhi ya matangazo huhimiza matumizi ya dawa za kulevya
      6. Ni chanzo cha matumizi ya nguvu za mabavu miongoni mwa wanafunzi
        zozote 5 x 1 =5
        M
        a - 07 
        b– 05
        ut – 03
        Adhabu
        Sarufi - ½ x 6 s =3
        Hujai- ½ x 6 h=3
        Ziada – maneno 10 ondoa alama 1 na kila maneno 5 ya ziada ondoa ½
  3.  
    1. Tuli
      Sogezi   2 x 1=2
    2.  
      1. [r]
      2. [ch]     2 x1=2
    3. Ni sentensi iliyo na nomino (kiima) na kitenzi au kitenzi kikuu kimoja/sentensi inayobeba wazo moja tu.
      k.m. Mama anapika chakula
      Maelezo 1
      Mfano 1
    4.  Tu      –     li        –      m        - pik – i     – a               ½ x6=3
      Nafasi      wakati      mtendwa    mzizi       Kauli
    5. anachotaka –Ts (kitenzi kisaidizi)
      kusoma – T (kitenzi kikuu)
      ki - t (kishirikishi kipungufu)
      3x1=3
    6. Kadiria jibu
      Ni viunganishi kama: au, ama, wala n.k   (alama 2)
    7.  
      1. U –ZI
      2. U - U      2x1=2
    8. Watu waliofika jana ni wale waliotoka mbali      (alama 2)
    9.  
      • Ndovu – shamirisho kipozi
      • Bunduki – shamirisho ala         2x1=2
    10. S → KN+ KT
      KN → O
      KT + E + E
      T → Kilipikwa
      E → jana
      E → jioni        ¼ x12=3
    11. Mngesoma kwa bidii, mngepita sana         2x1=2
    12. Kadiria jibu
      Maneno kama: naomba, tafadhali n.k. yatumike (alama 2)
    13. Mtoto ambaye alianguka jana/ana maumivu mengi
                                 tegemezi / huru
    14.  
      1. Hutumika pale msomaji anapohitaji kutua au kupumua
      2. Kutenganisha maneno katika orodha
      3. Katika tarakwimu zaidi ya elfu moja
      4. Katika kuandika anwani za kwanza              2x1=2
    15. Kadiria jibu k.m.
      1. Nairobi ni mji mkuu wa Kenya.
      2. Wanafunzi walienda ziara Nairobi          2x1=2
    16.  
      1. Kuku – ndege wa jamii ya kanga lakini mkubwa na anayefugwa
      2. Gugu – majani yasiyohitajika katika shamba
        ( Kadiria sentensi) 2x1=2
    17.  
      1. Onyesha mtu anayefanya kitendo
      2. Rejelea nafsi                                 2x1=2
    18. Mama alitaka kujua wageni wake wangefika saa ngapi? 2x1=2
    19. Safari/kusafiri/msafiri/msafara 1x1=1

      SARUFI
      Adhibu kila kosa la kisarufi litokeapo kwa mara ya kwanza hadi nusu ya alama mtahiniwa alizopata katika kila kisehemu
      Kila kosa ni nusu alama
      HIJAI
      Ondoa nusu alama kwa kila kosa la hijai litokeapo kwa mara ya kwanza hadi makosa 3
      ½ x6=3
  4.  
    1. Hotelini/mkahawani
    2.  
      1. Lugha si sanifu
      2. Kuchanganya ndimi
      3. Utohozi
      4. Sentensi fupi
      5. Lugha ya heshima
      6. Lugha ya biashara
      7. Lugha ya ucheshi
      8. Matumizi ya jazanda
      9. Msamiati maalum k.m. menu n.k.       
        za kwanza 4x2=8

        Adhabu
        1/2x4s=2
        1/2x4h=2
Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Paper 2 Kenya High Post Mock Exams 2020 - Questions and Answers.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?

Join our community on:

  • easyelimu app
  • Telegram
  • facebook page
  • twitter page
  • Pinterest