Kiswahili Paper 2 Questions and Answers - Samia Joint Mock Examination 2023

Share via Whatsapp

MAAGIZO

  • Andika jina lakonanamba yako katika nafasi ulioachiwa hapo juu.
  • Jibu maswali yote.
  • Andika majibu yako katika nafasi ulizoachiwa katika kijitabu hiki cha maswali.
  1. UFAHAMU (ALAMA 15)
    Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali .
    Gari lake kuukuu lilikuwa linapambana na barabara yenye mashimo yaliyoshiba na kutapika maji ya mvua ambayo sasa ilikuwa inaanza kupusa . Japo daima alipambana na usukani kunako mashimo haya yaliyotosha kuitwa magenge , alishukuru kwa hali hii. Vipi angeweza kulidhibiti gari lake hili kwenye barabara iliyosakafiwa nayo ikahitimu . Magurudumu haya yaliyong’ara kama upara wa shaibu aliyekula chumvi hadi iikamwogopa yangeyii uelekezi wake . Mara ngapi gari hili limetaka kumwasi barabarani . Haya yalikuwa baadhi ya maswali yaliyompitikia akilini . Hakujitakilifu kutaka kuyapa mji maana mara ile mawazo yake yalitekwa na kubwagwa katika nchi ya mbali - nchi ambayo sasa aliiona kama sinema akilini mwake .

    Alipofika nyumbani aliliegesha gari lake na kufululiza ndani . Siku mbili zilikuwa zimepita akiwa pale kazini . Madaktari kama yeye hawakuwa wengi . Alikuwa miongoni mwa madktari wenye ujuzi katika hospitali hii ya kitaifa . Wenzake wengi walikuwa wamehamia ughaibuni walikokwenda kutafuta maisha . Mshahara wao wa mkia wa mbuzi uliwasukuma na kuwatema nje ya nchi yao . Wengi wa waliohamia ng’ambo waliona vigumu kubaki katika ajira ambayo kivuno chake kilishindwa kumvusha mtu hata nusu ya kwanza ya mwezi . Malalamishi ya kulilia ujira wa heshima yaligonga kwenye masikio yaliyotiwa zege . Na kweli wanavyosema , mwenye macho haambiwi tazama . Basi walitazama hapa na pale wakaona penye mianya ya matumaini , nao wakaiandama .

    Hadi leo hii hamna la mno lililofanyika . Ndiyo maana Daktari Tabibu anarudi nyumbani tangu kuingia kazini hiyo juzi alfajiri . Hafanyi kwa kuwa katosheka , maana pia yeye ana dukuduku . Ana shaka ya mustakabali wake ikiwa mazingira ni haya ya kumsoza , maana umri nao unazidi kumla . Japo anatia na kutoa , mizani ya hesabu yake imeasi ulinganifu .

    Daktari Tabibu waama ni mfungwa . Ametekwa na kuzuiwa katika kupenda na kuchukia mambo .

    Ni kama mti uliodumaa . Anatamani barabara nzuri za lami . Anatamani mshahara wa kumwezesha kukidhi mahitaji yake na kutimiza majukumu yake ya kimsingi . Jana amesema na rafiki yake aliye ng’ambo kwa simu ambayo sasa imetulia mkabala naye . Ingawaje mwenzake huyu alikuwa mchangamfu na kumdokolea hali ya maisha ya kuridhisha kule ugenini kama vile wanataaluma kuenziwa , yapo vilevile yaliyomtia unyonge moyoni . Upweke ndio uliomtia fukuto kuu . Licha ya hela zote hizo za kupigiwa mfano , watu hawana muda wa kutembeleana na kujuliana hali au hata kukutana tu mkahawani wakashiriki mlo . Eti ni kila mtu na hamsini zake . Halafu ipo changamoto ya hali ya hewa . Baridi ya ng’ambo haifanyi mzaha katika kumtafuna mtu . Ni hali tofauti na ile aliyoizoea .

    Daktari Tabibu alizitia kauli za rafiki yake kwenye mizani ya moyo wake . Akawaza ikiwa kweli si bora kulemazwa na mzizimo ugenini badala ya kuishi katika kinamasi cha kuumbuliwa nyumbani . Kisha punde lilimjia wazo la marehemu nyanyake na wengine kama yeye waliofadhili masomo yake kupitia kwa serikali na njia ya kodi . Je , si usaliti huu . Vipi aikimbie nchi kabla ya kuihudumia ilhali imemjenga hadi kuwa daktari . Na je , wafanyakazi wake wa nyumbani watakwenda wapi . Atawaambia kuwa sasa hahitaji huduma zao kwa kuwa anakimbia nchi yake .

    Mawazo yake yalikatizwa na simu iliyolia na kumshtua . Alipoitazama aliiona imeng’ara kwa mwangaza ulioweka wazi jina la mpigaji . Alifahamu kuwa leo hii tena dharura nyingine ilikuwa inamwalika hospitalini . Mwili wake ulimsaliti ingawa moyo wake ulimkumbusha kuwa lisilo budi hutendwa . Hapo ndipo alipoiinua ile simu tayari kusema na mwenzake upande wa pili .

    “Haloo ! ‘ Sauti nyororo kutoka upande wa pili iliita .
    “Haloo ! “
    “Naam ! Dharura nyingine tena daktari . Unaombwa kuokoa maisha mengine tena ! “
    “Haya . Ila mwanzo nitahitaji kujimwagia maji ,’ na pale pale akaikata ile simu .

    Daktari Tabibu aliingia hamamuni huku kajifunga taulo kiunoni tayari kuoga . Aliyafungulia maji lakini ule mfereji uligoma kutapika maji . Ulikuwa umekauka kabisa . Daktari Tabibu aliduwaa pale . Aliufunga ule mfereji kabla ya kuiaga bafu .
    Maswali
    1. Eleza sababu nne zinazowafanya wataalamu kuhamia nchi za nje .( alama 4 )
    2. ‘Hakuna masika yasiyokuwa na mbu” . Thibitisha kauli hii kwa kurejelea hali ya waliohamia ng’ambo . [alama 3]
    3. Fafanua athari tatu zinazoikumba nchi ya msimulizi kutokana na uhamiaji wa wataalamu. [alama 3]
    4. Eleza mchango wa teknologia kwa kurejelea kifungu . [alama 3]
    5. Eleza maana ya msamiati ufuatao kulingana na taarifa . [ alama 2]
      1. kuyapa mji 
      2. fukuto
  2. UFUPISHO (ALAMA 15)
    Soma kifungu kifuatacho kasha ujibu maswali.
    Kila msanii anacho kifaa chake ambacho anakitumia, ambacho kinakuwa alama ya usanii wake. Mchoraji anategemea sana kalamu au rangi zake na mchongaji anao ubao au mti wake.

    Vivyo hivyo mwanafasihi naye anategemea lugha katika usanii wake. Matumizi ya lugha ni miongoni mwa mambo muhimu yanayotofautisha kazi ya fasihi na kazi isiyo ya fasihi. Jinsi ambavyo mwandishi anavyoitumia lugha yake na kiwango cha usanii anachofuraia ndivyo alama muhimu inayomtofautisha na mwandishi mwingine wa fasihi.

    Katika uhakiki wa kazi za fasihi za hivi karibuni, hasa katika Kiswahili, kumekuwa na msisitizo mkubwa katika maudhui ya kazi hizo au kwa lugha rahisi, ujumbe unaotolewa na mwandishi. Hivyo maswali yanayoulizwa ni kama kazi hii ina umuhimu gani katika jamii ya leo? Inajengaje tabia, mwenendo na mwelekeo wa jamii? Ina maadili gani?

    Mara nyingi, wahakiki hawaulizi mwandishi alivyofaulu kisanaa isipokuwa kama jambo la ziada tu mwishoni uhakiki wa namna hii hasa umehusu kazi za fasihi zisizo za ushauri kwa sababu imekubalika kwa muda mrefu kuwa mshauri lazima aitawale lugha yake vizuri ndipo aweze kuleta ule mvuto maalum unaotakiwa na kufikia viwango vinavyokubalika katika fani hii.

    Haiwezekani kutenganisha maudhui na usanii katika kazi yoyote ile ya fasihi ujumbe unaoletwa katika kazi ya fasihi unaweza kutolewa na mtu mwingine yeyote kwa njia nyingine. Ujumbe huo unaweza kutolewa kwa njia ya hotuba, vitabu au maongezi ya kawaida.

    Katika isimu ya lugha , tunaposema ya kwamba mwanadamu anajua lugha yake, tuna maana kuwa “amemeza” mfumo wa lugha yake wa matamshi, muundo wa maneno, muundo wa sentensi na maana zinazokusudiwa. Ujuzi alio nao mwanadamu huyu ni sawa, na ujuzi walionao wanadamu wengine wa jamii yake wanaozungumza lugha moja. Hivyo tukisema kuwa mwanadamu aongee lugha hatuna maana tu ya kule kumeza mfumo wake wa lugha bali ni uwezo wake wa kuitumia katika mahusiano yake na wanajamii wengine. Katika lugha yoyote ile kuna mitindo mingi inayotumika kutegemea kile kinachozungumziwa.Hivyo, tunaweza kuwa na mtindo wa siasa, sheria dini na kadhalalika pia upo mtindo wa kawaida unaotumika.

    Katika mawasiliano ya kila siku ya wanajamii moja Katika mtindo huu kuna matumizi ya aina mbalimbali kihusiana na nyanja tofauti za maisha. Matumizi haya yanaitwa rejesta kwa lugha ya kitaalam. Rejesta yoyote ile inategemea nani anazungumza nini na nani, wapi kuhusu nini na kwa sababu gani.

    Mtu anayejua lugha yake vizuri tunategemea aweze kuitumia katika mitindo iliyobadilika na aweze kujua mazingira anayopaswa kutumia mtindo mmoja badala ya mwingine katika mahusiano ya kawaida, mtumiaji wa lugha anapaswa kujua ni rejesta gani anapaswa kutumia kila wakati. Mwandishi wa habari lazima awe “amefuzu” kuliko kuweka haya matumizi tofauti ya lugha.

    Mwandishi huyu anatakiwa kuwa mtafiti ili ajue Yale matumizi ambayo yeye hana haja nayo katika mahusiano yake ya kawaida na huyo aweze kuchora jamii yake inayostahili katika kazi yake. Sababu kubwa ya kumtaka mwanafasihi kuyajua kinaganaga matumizi tofauti ni ule ukweli kuwa kazi ya fasihi haina mpaka na utumizi wa lugha.
    Maswali.
    1. Eleza vipengele muhimu vya lugha katika uwasilishaji wa fasihi (maneno 70-80) (al.8)
      MATAYARISHO
      JIBU
    2. Fupisha aya tatu za mwisho(maneno 75-85) (al.7)
      MATAYARISHO
      JIBU
  3. MATUMIZI YA LUGHA ( al 40)
    1. Andika tofauti moja kati ya sauti zifuatazo: ( al 2)
      1. /ny/ na /y/
      2. /d/ na /t/
      3. /mb/ na /nd/
      4. /s/ na /z/
    2. Onyesha muundo wa silabi katika maneno yafuatayo ( al 2)
      1. Mtu
      2. Ngoma
      3. Embe
      4. Chai
    3. Tunga sentensi mbili kuonyesha matumizi mawili ya kiambishi a ( al 2)
    4. Tumia neno ngali katika sentensi kuonyesha : ( al 3)
      1. Tendo halikutendeka na hakuna uwezekano
      2. Kitenzi kishirikishi kikamilifu
      3. Kitenzi kisaidizi
    5. Onyesha miundo miwili ya nomino katika ngeli ya LI-YA (al 2)
    6. Tunga sentensi katika wakati uliopita hali timilifu ( al 1)
    7. Andika sentensi ifuatayo katika hali ya ukubwa ( al 2)
      Viti vingine huundwa kwa vijijiti vinene
    8. Akifisha sentensi ifuatayo ( al 3)
      Halima aliamka akiwa na joto jingi mwilini Pamela nenda busia ukamununulie dawa alimwambia
    9. Kando na kuonyesha urejeshi katika sentensi , eleza matumizi mengine matatu ya kiambishi ji ( al 3)
    10. Andika sentensi ifuatayo katika usemi wa taarifa ( al 2)
      “Tutakapofuata maagizo ya wizara, janga la korona litasahaulika kabla ya mwaka ujao.” Waziri wa afya aliahidi.
    11. Tunga sentensi zifuatazo: ( al 2)
      1. Amrishi
      2. Changamano
    12. Tunga sentensi iliyo na kirai kihusishi kisha ukibadilishe kiwe kielezi kimoja ( al 2)
    13. Ainisha vishazi katika sentensi ifuatayo ( al 2)
      Iwapo utapita mtihani utaenda chuo kikuu.
    14. Bainisha shamirisho na chagizo katika sentensi ifuatayo: ( al 3)
      Sabina alimnunulia Nyaboke nguo nzuri kwa senti zake.
    15. Andika sentensi ifuatayo upya kulingana na maagizo ( al 1)
      Kasisi alikariri sala ya Bwana baada ya waumini.
      Anza kwa:
      Waumini
    16. Changanua sentensi ifuatayo kwa kielelezo cha visaduku ( al 4)
      Halima atamtembelea shangazi Nakuru kisha ampelekee mama mahindi.
    17. Andika sentensi ifuatayo upya ukitumia kinyume cha sehemu iliyopigiwa mstari :( al 1)
      Wanajeshi watapiga kambi juma lijalo.
    18. Andika sentensi yenye muundo ufuatayo ( al 2)
      KN( V+N+V)+KT(Ts+T+E)
    19. Bainisha maana mbili zinazojitokeza katika sentensi ifuatayo: ( al 2)
      Mwalimu alimsomesha mwanafunzi
    20. Chakula ni kwa mlo, barabara ni kwa………………………….na afya ni kwa…………………( al 2)
  4. ISIMUJAMII ( al 10)
    Mirima : Sasa Mangwasha
    Mangwasha : Poa
    Mirima : Kesho utakuja kunitembelea ?
    Mangwasha : Naam ! Nitajaribu
    Mirima : Wewe acha. Kujaribu kwako kila mara. Jana uliniambia hivyo tena. Utasema ukweli when?
    Mangwasha: Usoichukulie vibaya my dear , ninajiandaa kwa birthday ya bro wangu.
    Mirima: Ukikosa hata mimi…
    Mangwasha: La! La si hivyo buddy…
    Maswali
    1. Haya ni mazungumzo ya aina gani ? ( al 2)
    2. Tambua sifa za lugha hii kama zinavyojitokeza katika mazungumzo haya ( al 4)
    3. Taja sifa zingine zinazohusishwa na sajili ( al 4)

MWONGOZO WA KUSAHIHISHA

  1. UFAHAMU
    1.  
      • Kuharibika kwa miundo msingi
      • Mishahara duni
      • Malalamishi yao kutosikilizwa
      • Kukosa huduma za kimsingi
      • Kuvutiwa na maisha ya kuridhisha huko ng`ambo (hoja 4 za kwanza)
    2.  
      • Ng’ambo kuna maisha yakuridhisha kama kuthaminiwa kwa wanataaluma(alama 1)
      • Hata hivyo kuna dosari (mbu) kamaupweke, ubinafsi na baridi.(alama 2)
    3.  
      • Umma kutofaidika kutokana na huduma za wataalamu wake licha ya kuwafadhili.
      • kuwaachia mzigo wa kazi wataalamu
      • Kulazimika kufanya kazi kwa saa nyingi
      • Maisha ya watu wengi huwa hatarini.
      • Hasara kwa taifa baada ya wataalamu kutoroka
      • Kuwapo kariziki wafanyakazi (hoja 3 za kwanza)
    4.  
      • Huwezesha kuwasiliana na jamaa walio mbali
      • Huwezesha kuwafikia watoajihuduma patokeapo dharura
      • Hurahisisha usafiri
      • Hurahisisha kupata huduma ya karibu ya maji (alamazozote 3)
    5.  
      1. kuyapamji - kuyawazia, kufikiria, kuyatafakari.
      2. Fukuto- wasiwasi,mashaka, shida, dukuduku (Alama 2)
    1. UFUPISHO
      • Lugha hutofautisha kazi ya fasihi na isiyo ya fasihi.
      • Jinsi anavyotumia lugha na kiwango cha usanii ndiyo alama inayomtofautisha.
      • Msisitizo mkubwa katikamaudhui .
      • Uhakiki kuonyesha mshairi alivyotawala lugha yake vizuri.
      • Haiwezekani kutofautisha maudhui na usanii.
      • Mwanadamu kujua lugha yake ni kumeza” mfumo wa lugha yake.
      • Katika lugha kuna mitindo inayotumika kutegemea Nyanja tofauti.
      • Mtu anayejua lugha vizuri aweze kutumia inavyokubalika.
      • Mwandishi awe mtafiti ili ajue yale matumizi asiyokuwa na haya nayo.                    Zozote 7x1 (utiririko 1)
    2.  
      • Mwanadamu kujua lugha ni kumeza mfumo wa lughayake.
      • Ujuzi alionao ni sawa na wengine wanaozungumza lugha moja.
      • Aweze kutumia katika mahusiano ya kena wanajamii wengine.
      • Kuna mitindo mingi inayotumika siasa, sharia ,dini.
      • Mtindo wa kawaida unaotuka katika mawasiliano ya kila siku(rejesta)
      • Anayejua lugha vizuri aweze kuitumia katika mitindo iliyokubalika.
      • Mwandishi wa habari awe “amefuzu” kuelewa matumizi tofauti ya lugha.
      • Mwandishi awe mtafiti ili achore jamii yake inavyostahili.          ( Zozote 6x1) (utiririko 1)
    3. Matumizi ya Lugha
      1.  
        1. /ny/ ni king’ong’oilhali /y/ kiyeyusho
        2. /d/ ni ghunailhali /t/ sighuna
        3. /mb/ ni sauti ya midomo ilhali /nd/ ni yaufizi
        4. /s/ ni sighuna ilhali /z/ ni ghuna     ½ x4=2
      2.  
        1. mtu- K-KI
        2. ngoma- KKI-KI
        3. embe-I-KKI
        4. chai-KI-I        ½ X4=2
      3.  
        1. Anasoma- nafsi
        2. Aimba- haliisi yodhihirika
        3. Mtoto wa rais amefika ( a- unganifu)
        4. Anaimba       1x2=2
      4.  
        1. Ningaliimba kwa sauti ningalituzwa.
        2. Mama angali shambani.
        3. Wazee wangali wanasuluhisha mgogoro tata.  1x3=3
      5.  
        • JI-MA –Jiwe-mame
        • JI-ME-Jino-meno
        • JA-MA-Jambo-mambo
        • O-MA- embe-maembe    1x2=2
      6. Malenga alikuwa ametunga shairi 1x1=1
      7. Majiti mengine huundwa kwa majijiti manene.  2/0
      8. “Halima aliamka akiwa na joto jingi mwilini, Pamela nenda Busia ukanunue dawa,” alimwambia.  6x ½ =3
      9.  
        1. Kiambishi cha ukubwa / dharau
          • jidege, jilango
        2. Kiambishi cha unominoshaji
          • cheza-mchezaji
        3. Kiambishi awali cha baadhi ya nomino katika ngeli ya LI-YA
          • jiwe, jino
        4. Kuweka nomino katika udogo zilizo katika ngeli ya KI-VI
          • Kitabu-kijitabu, kikapu-kijitapu  1x2=2
      10. Waziri wa afya aliahidi kuwa wangefuata maagizo ya wizara, janga la korona lingesahaulika kabla ya mwaka ambao ungefuata. 4x ½ =2
      11.  
        1. Fungua mlango ! ( atumiekihisishi)
        2. Wanafunzi waliofuzu vyema watatuzwa zawadi.  (sentensiiwenakishazi)  1x2=2
      12.  
        • Paka ameingia ndani ya shimo.
        • Paka ameingia shimoni.   1x2=2
      13.  
        • Iwapo utapita mtihani – kishazitegemezi
        • Utaenda chuo kikuu- kishazihuru    1x2=2
      14.  
        • Nguo nzuri - shamirishokipozi
        • Nyaboke - shamirishokitondo
        • Senti zake - shamirishoala
        • Kwa senti - chagizo  1x3=3
      15. Waumini walikariri sala ya bwana kabla ya Kasili.  1/0
      16.  
                                    EngMocks2023Q3
                                                                                                                                                                         16x ½ =4
      17. Wanajeshi watavunja kambi juma lijalo.   1/0
      18. Mwenye nyumba kubwa atakuwa akiishi hapa. 2/0
      19.  
        1. Alimfunza
        2. Alimfanya kusoma   2x1=2
      20.  
        • baraste/ sawasawa
        • ahueni/siha     2x1=2
  2. ISIMUJAMII
    1. Mazungumzoyawanahirimu 1x2=2
    2.  
      1. Matumizi ya lugha legevu - poa
      2. Kuchanganya ndimi – birthday ya bro wangu
      3. Lugha ya mkato - bro
      4. Maswali na majibu
      5. maswali ya balagha - lini utasema ukweli ?    4x1=4
    3.  
      1. Lugha huwa haina urasmi bali utani hutawala –kwa sababu, wao ni wanahirimu na huzungumza ili kujenga uhusiano wao.
      2. Maudhui ya mazungumzo huwa si maalum bali huwategemea wanaozungumza.
      3. Lugha inayotumiwa huhusisha kukatizana kauli wakati wa mazungumzo kwa sababu kila mmoja anataka kuonyesha kuwa anafaham uzaidi.
      4. Mbinu rejeshi hutawala mazungumzo yao ili kuthibitisha wasemayo ni sahihi.
      5. Matumizi ya misemo na mafumbokama vile sheng’ ambayo yanaeleweka na vijana katika muktadha huo.
      6. Ni lugha iliyojaa chuku na utani ili kukuza uhusiano mwema baina yao. 4x1=4
Join our whatsapp group for latest updates

Download Kiswahili Paper 2 Questions and Answers - Samia Joint Mock Examination 2023.


Tap Here to Download for 50/-




Why download?

  • ✔ To read offline at any time.
  • ✔ To Print at your convenience
  • ✔ Share Easily with Friends / Students


Get on WhatsApp Download as PDF
.
Subscribe now

access all the content at an affordable rate
or
Buy any individual paper or notes as a pdf via MPESA
and get it sent to you via WhatsApp

 

What does our community say about us?